Monday 2 February 2009

Dirisha la Uhamisho Wachezaji halifungwi leo saa 2 usiku [saa za bongo]!!!

Uongozi wa LIGI KUU England umetangaza kuwa Vilabu vitaruhusiwa kukamilisha taratibu za uhamisho hata baada ya Dirisha la Uhamisho Wachezaji kufungwa leo saa 2 usiku saa za bongo ikiwa ni kuvisaidia Vilabu hasa baada ya Uingereza yote kukumbwa na kuanguka kwa barafu nyingi iliyoleta matatizo nchi nzima hasa kwenye usafiri ambako barabara, reli na viwanja vya ndege kufungwa [Tizama picha kushoto Polisi akiwa barabarani alivyoganda kwa barafu!!].
Uongozi wa LIGI KUU umetamka kuwa baada ya kujadiliana na FA pamoja na FIFA wameruhusiwa kuongeza muda ili Klabu zikamilishe makubaliano na Vilabu vingine pamoja na Wachezaji husika ili mradi tu Vilabu vinavyohusika kwenye uhamisho vinatuma barua pepe kwa LIGI KUU kwamba Vilabu hivyo vina makubaliano na vilevile Klabu inayomnunua Mchezaji iwaridhishe kuwa hali ya hewa ndio imechelewesha kutosainiwa Mchezaji kabla ya saa 2 usiku saa za bongo.
Wakati kuna taarifa hizo za kuongeza muda, tayari Klabu kadhaa zimekamilisha uhamisho wa Wachezaji kabla ya dirisha kufungwa kama tunavyowaletea hapa chini.

Jo ahamia Everton kwa mkopo

Klabu ya Everton imemsaini Mbrazil wa Manchester City Jo kwa mkopo hadi mwishoni mwa msimu huu.
Jo mwenye umri wa miaka 21 alitua Man City akitokea CSKA Moscow Julai 2008 ingawa mpaka sasa anashindwa kupata namba ya kudumu hapo Man City alikochezea mechi 18 na kufunga magoli matatu tu.
Everton kwa sasa ina uhaba mkubwa wa Washambuliaji baada ya Mastraika wao wote, wakiwemo
Ayegbeni Yakubu, Louis Saha na James Vaughan kuumia.
Jo, ambae ana urefu wa Futi 6 Inchi 3 na jina lake kamili ni Joao Alves de Assis Silva, alifunga magoli 44 katika mechi 77 alizochezea CSKA Moscow.

Portsmouth wamsaini Kiungo Basinas

Mgiriki aliekuwemo kwenye Timu ya Ugiriki iliyoshinda Kombe la Mataifa ya Ulaya mwaka 2004 na anaechezea Klabu ya Ugiriki AEK Athens, Angelos Basinas [33] amejiunga na Portsmouth kwa mkataba wa miezi 18.
Huyo ni Mgiriki wa pili kuchukuliwa na Portsmouth kwenye Dirisha hili la Uhamisho mwingine akiwa Theofanis Gekas ambae kachukuliwa kwa mkopo kutoka Bayer Leverkusen ya Ujerumani hadi mwishoni mwa msimu huu.

Camara yuko Stoke kwa mkopo

Mshambuliaji kutoka Senegal, Henri Camara [31], amehamia Stoke kwa mkopo hadi mwishoni mwa msimu akitokea Klabu yake Wigan.
Camara msimu huu amefunga goli 6 akiwa na Wigan.

Mechi ya marudiano Kombe la FA Arsenal v Cardiff hapo kesho yaahirishwa

Ile mechi ya marudiano ya Kombe la FA kati ya Arsenal v Cardiff iliyokuwa ichezwe kesho Emirates Stadium imeahirishwa kwa sababu ya hali ya hewa mbaya iliyoandamana na kuanguka barafu nyingi iliyoikumba England na hasa Jiji la London.
Ingawa kiwanja cha Emirates kinachezeka kwa kuwa kina hita chini ya ardhi zinazoyeyusha barafu mechi hii itapangwa baadae kwa hofu ya usalama wa Washabiki na vilevile wasiwasi pengine usafiri utakuwa mgumu.
Timu hizi zilitoka suluhu 0-0 zilipocheza Januari 25.

No comments:

Powered By Blogger