Saturday 3 April 2010

Chelsea washika hatamu!
  • Man United 1 Chelsea 2
  • Arsenal 1 Wolves 0
Chelsea leo wameifunga Manchester United Uwanjani Old Trafford bao 2-1 na kushika uongozi wa Ligi Kuu wakiwa na pointi 74, wakifuata Man United pointi 72 na Arsenal pointi 71.
Mabao ya Chelsea yalifungwa na Joe Cole na Drogba na lile la Man United alifunga Kiko Macheda.
Hata hivyo baada ya mechi, Meneja Msaidizi wa Man United Mike Phelan alilalamikia uamuzi na wengi waliona bao la pili la Chelsea likifungwa na Drogba akiwa wazi wazi ofsaidi.
Katika mechi iliyofuata baadae, Arsenal walimudu kupata bao dakika ya mwisho ya mchezo Mfungaji akiwa Niklas Bendtner na kuishinda Wolves bao 1-0.
MATOKEO KAMILI:
Arsenal 1 Wolves 0
Bolton 0 Aston Villa 1
Man Utd 1 Chelsea 2
Portsmouth 0 Blackburn 0
Stoke 2 Hull 0
Sunderland 3 Tottenham 1
MSIMAMO:
[Kwa Timu za juu]
1 Chelsea mechi 33 pointi 74
2 Man United mechi 33 pointi 72
3 Arsenal mechi 33 pointi 71
4 Tottenham mechi 32 pointi 58
5 Man City mechi 32 pointi 57
6 Liverpool mechi 32 pointi 54
Wenger lawamani!!
• Kuumia kwa Gallas, Fabregas kwamtia matatani!!
Meneja wa Ufaransa, Raymond Domenech, amelaumu uamuzi wa kumchezesha William Gallas kwenye mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI kati ya Arsenal na Barcelona siku ya Jumatano na kusababisha ajitoneshe musuli za mguu ambazo kabla zilimweka nja miezi miwili.
Lakini Meneja wa Klabu ya Gallas, Arsenal, Arsene Wenger, ameutetea uamuzi wa Gallas kucheza mechi hiyo na kusema ulikuwa sahihi kwa vile alipona na kufanya mazoezi siku 10 kabla.
Raymond Domenech, akiongea kwenye Mkutano wa Shirikisho la Soka la Ufaransa, alisema: “Nimeudhika! Ilikuwa mapema mno kumchezesha Mchezaji alietoka kwenye maumivu! Sasa huenda akalikosa Kombe la Dunia!”
Domenech anataka Wachezaji wa Kikosi cha Ufaransa wakusanyike Mei 18 tayari kwenda kambini kwa Fainali za Kombe la Dunia zinazoanza Juni 11 huko Afrika Kusini.
Domenech alikuwepo Uwanjani Emirates Jumatano kushuhudia pambano la Arsenal na Barcelona lakini Wenger alisema: “Sikuongea nae! Nina majukumu na Arsenal. Timu ya Taifa ya Ufaransa ni muhimu lakini kwa Gallas kwanza ni Arsenal kwa sababu wanamlipa mshahara! Wachezaji wakiwa fiti tunawatumia!”
Mbali ya kupata kibano kuhusu uteuzi wake wa Gallas, Wenger pia anaonja joto ya jiwe kwa kumchezesha Nahodha Cesc Fabregas katika mechi na Barcelona huku kukiwa na madai alikuwa na ufa kwenye mfupa wake wa mguu na tatizo hilo likazidishwa kwa kucheza mechi hiyo na sasa yuko nje Msimu wote uliobaki na huenda akalikosa Kombe la Dunia.
Wenger mwenyewe ametoboa kuwa wanafanya uchunguzi wa mkasa wa Fabregas ingawa amedokeza kuwa kabla ya mechi na Barcelona walikuwa na ripoti toka kwa Madaktari wawili tofauti waliochunguza eksirei za Fabregas na kutamka mfupa ulikuwa umechubuka tu na si kuwa na ufa.
Wakati huohuo, Arsenal imethibitisha Andrey Arshavin atakuwa nje kwa wiki mbili akijiuguza musuli ya mguu.
Arshavin alianza mechi na Barcelona lakini ilibidi abadilishwe kipindi cha kwanza baada ya kuumia.
Kwa Wadau wa La LIGA……………………………..
• EL CLASICO ni Aprili 10!!!!
Mechi za wikiendi hii ni za mwisho kwa Vigogo wa Spain, Real Madrid na Barcelona, kabla hawajakumbana hapo Aprili 10 Estadio Bernabeau katika lile pambano murua na tamu linalobatizwa jina la “ El Clasico” na safari hii, El Clasico, ni ngoma ngumu mno hasa kwa vile Timu hizi zinafukuzana na ziko pointi sawa kileleni ingawa Real ndie kinara kwa tofauti ya magoli.
Kila Timu ina pointi 74 na zipo pointi 21 mbele ya Timu ya 3 Valencia huku Timu ya 4 Mallorca ikiwa na pointi 47 tu.
Katika mechi ya kwanza ya La Liga kati ya Timu hizi Msimu huu huko Nou Camp, Barcelona iliibuka mshindi kwa bao la Zlatan Ibrahimovic.
Msimu uliokwisha katika mechi iliyochezwa Bernabeau, Barca waliwafumua Real mabao 6-2.
Wikiendi hii, Barcelona wako kwao Nou Camp kucheza na Athletic Bilbao na Real Madrid wako ugenini kucheza na Racing Santander.
Mbali ya mechi ya La Liga wikiendi hii, Jumanne ijayo ndani ya Nou Campa Barca wanarudiana na Arsenal kwenye mechi ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI baada ya kutoka sare 2-2 na Arsenal Jumatano iliyopita huko Emirates.
Bila ya Rooney, ushindi upo, adai Fergie!
Wakati akiwahakikishia Waingereza kuwa Rooney hakuumia vibaya, Sir Alex Ferguson pia ameionya Chelsea na Timu nyingine za Ligi Kuu kuwa Manchester United ina uwezo mkubwa wa kushinda bila ya Mfungaji wao huyo bora.
Fergie alisema: “Rooney hakuvunjika mfupa na hakuumia vibaya musuli za enka na hilo ni jambo zuri! Hivyo Taifa liache kusali! Sisi kazi yetu ni kuchagua Timu bila Rooney!”
Ingawa Chelsea wanaona faraja kubwa kupambana na Manchester United Uwanja wa Old Trafford Jumamosi bila Rooney, Fergie amewaonya na kutamka kuwa Timu yake ina uwezo mkubwa wa kushinda mechi hiyo bila ya Rooney.
Fergie amesema: “Nina hakika Wachezaji hawana wasiwasi kumkosa Rooney. Ni pigo kumkosa lakini sisi kuna wakati tuliikosa Defensi yetu yote na tukachechemea na kuongoza Ligi kwa pointi moja!”
Kuhusu Chelsea kutokuwa na mechi wiki nzima wakati wao walicheza Jumanne tena safarini huko Ujerumani, Sir Alex Ferguson amesema hawaoni hilo kama mzigo kwao kwani wao wamezoea kucheza Jumamosi na Jumatano na safari hii wamepata siku 4 kupumzika.
Fergie amesema: “Chelsea wataona ni faida kwao kupumzika wiki nzima. Wakati mwingine inasaidia na wakati mwingine ni hasara kwa vile unaukosa ule mtiririko wa mechi mfululizo na kiwango cha utendaji hushuka.”
Katika mechi ya leo kumekuwa na uvumi mkubwa kuwa Owen Hargreaves ambae amekuwa nje ya uwanja kwa miezi 18, mechi yake ya mwisho ikiwa Stamford Bridge Septemba 2008 Man United walipotoka sare 1-1 na Chelsea, huenda akawepo benchi.
Vikosi vinavyotegemewa kuanza:
Manchester United: Van der Sar, Neville, Vidic, Ferdinand, Evra, Fletcher, Nani, Carrick, Park, Giggs, Berbatov.
Chelsea: Cech, Ferreria, Alex, Terry, Zhirkov, Mikel, Lampard, Malouda, Ballack, Anelka, Drogba.

Friday 2 April 2010

West Ham walalamika Ligi Kuu kuhusu Fulham
• Ni kwa kupanga Timu dhaifu dhidi ya Hull City
Wasimamizi wa Ligi Kuu wamethibitisha kupokea malalamiko ya West Ham kuhusu uamuzi wa Meneja wa Fulham, Roy Hodgson, wa kupanga Kikosi dhaifu dhidi ya Hull City Jumamosi iliyopita kilichofungwa na Hull City bao 2-0.
Ushindi huo wa Hull City, ambao ni moja ya Timu 3 zilizo mkiani, uliifanya Hull iwe sawa kwa pointi na West Ham zote zikiwa na pointi 27 ingawa West Ham wako juu kwa idadi ya magoli.
Hogson aliwapumzisha Wachezaji Bobby Zamora, Danny Murphy, Damien Duff, Aaron Hughes na Dickson Etuhu katika mechi hiyo na Hull lakini wote walirudi Kikosini Fiulham ilipoifunga Wolfsburg 2-1 kwenye EUROPA LIGI Alhamisi Aprili 1.
Msemaji wa Ligi Kuu amethibitisha kupokea malalamiko ya West Ham na amesema wao watawasiliana na Fulham ili kupata maoni yao kisha Bodi ya Ligi Kuu itakaa kutoa uamuzi.
Sheria za Ligi Kuu zinatamka kila Timu inatakiwa kupanga Kikosi chao bora kilichopo wakati huo.
Wakipatikana na hatia, Fulham wanaweza kupigwa Faini ya Pauni 25,000 sawa na Wolves ambao walipatikana na hatia ya kupanga Kikosi dhaifu walipocheza na Manchester United Septemba mwaka jana.
Kocha wa Wolves, Mick McCarthy, aliwapumzisha Wachezaji 9 kati mechi hiyo na Man United.
Hata hivyo,Hodgson amesisitiza Fulham haikufanya kosa lolote na amesema yeye atakuwa akibadilisha Wachezaji ikibidi.
Hodgson ametamka: “Hakika, West Ham hawatakiwa kutupangia Timu! Sisi hatuna kesi ya kujibu! Tulipocheza na Hull, nilimpanga Mchezaji ambae kauzwa Pauni Milioni 10 kwa Man United [akimaanisha Chris Smalling], Kagisho Dikgacoi, ni Mchezaji wa Kimataifa wa Afrika Kusini na nilimbadili Zamora kwa kumchezesha Dempsey ambae ni Mchezaji wa Kimataifa wa USA!”
Hodgson aliongeza kwa kusema Liverpool, Man United na Chelsea zikibadili Wachezaji hakuna anaelalamika.
Nae Meneja wa Wigan, Roberto Martinez, amemsapoti Hodgson kwa kuiita hatua West Ham kuishtaki Fulham ni upuuzi.
Ligi Kuu: Ni uhondo wikiendi hii!
Jumamosi, 3 Aprili 2010 [saa za kibongo]
[saa 8 dak 45 mchana]
Man United v Chelsea
[saa 11 jioni]
Arsenal v Wolves
Bolton v Aston Villa
Portsmouth v Blackburn
Stoke v Hull
Sunderland v Tottenham
[saa 1 na nusu usiku]
Burnley v Man City
________________________________________
Jumapili, 4 Aprili 2010
[saa 11 jioni]
Birmingham v Liverpool
Fulham v Wigan
[saa 12 jioni]
Everton v West Ham
---------------------------------------------------------
Man United v Chelsea
Ingawa hii ni Bigi Mechi lakini kimahesabu siyo itakayoamua nani ni Bingwa ila itaamua nani mwenye nafasi kubwa ya kutwaa huo Ubingwa.
Mechi hii ndiyo ya kwanza kuchezwa kwa wikiendi hii na itaanza saa 8 dakika 45 saa za bongo Uwanjani Old Trafford.
Ushindi kwa Man United, watakaocheza bila Mfungaji wao Bora Wayne Rooney ambae ni majeruhi, utawafanya wawe pointi 4 mbele ya Chelsea.
Mwanzoni mwa msimu, Chelsea waliishinda Man United kwa bao 1-0, bao ambalo lilizua mzozo na mjadala mkubwa kuhusu uhalali wake.
Katika mechi kama hii Msimu uliokwisha, Man United waliikung’uta Chelsea bao 3-0.
Arsenal v Wolves
Baada ya kazi nzito ya Jumatano walipotoka sare 2-2 na Mabingwa wa Ulaya Barcelona kwenye UEFA CHAMPIONS LIGI, Arsenal wapo nyumbani Emirates kucheza na Wolves bila ya Wachezaji wao Cesc Fabregas, Gallas na Arshavin ambao wote waliumia kwenye mechi hiyo na Barcelona.
Wolves wapo kwenye wimbi la kutokufungwa katika mechi 4 na hilo limewafanya wajiwekee tabaka la pointi 5 kati yao na Timu zilizo eneo la kushuka Daraja
Sunderland v Tottenham
Tottenham wapo nafasi ya 4 kwenye Ligi, nafasi ambayo pia inawaniwa na Man City, Liverpool na Aston Villa, na kila mmoja anaitaka nafasi hiyo ili acheze UEFA Msimu ujao.
Lakini wapinzani wa Tottenham, Sunderland, watakuwa nyumbani Uwanja wa Stadium of Light na wao wanapigania kujinusuru kutoshuka Daraja huku Meneja wao Steve Bruce akitaka wajizolee pointi 40 ambazo anahisi ndizo zitawapa usalama.
Sunderland wamebakisha mechi 6 na wapo pointi 5 pungufu ya hizo 40 anazotaka Steve Bruce.
Bolton v Aston Villa
Baada ya kutandikwa na Chelsea 7-1 Jumamosi iliyopita na kukumbwa na uvumi mkubwa kuwa Meneja wao Martin O’Neill anaondoka, Aston Villa wanarudi uwanjani huko Reebok kucheza na Bolton ambayo inapigana kujilimbikizia pointi ili wasivutwe kwenye zile Timu 3 za mkiani ambazo hushuka Daraja.
Stoke City v Hull City
Hull City wanawania ushindi wao wa pili mfululizo baada ya wiki iliyopita kuitungua West Ham lakini Uwanja wa Britannia ni mgumu kupata ushindi.
Msimu huu, Hull hawajahi kushinda mechi mbili mfululizo.
Portsmouth v Blackburn
Portsmouth wako mkiani wakiwa pointi 14 nje ya usalama wa kutoshushwa Daraja na wamebakiza mechi 6.
Kimahesabu, Portsmouth wanaweza kutangazwa wameshuka Daraja wikiendi hii endapo watafungwa na Blackburn na matokeo ya mechi nyingine yakaenda vibaya kwao.
Blackburn wao wameshajihakikishia kubaki Ligi Kuu waliposhinda wiki iliyopita kwa kuifunga Burnley 1-0 na kuzipita pointi 40 ambayo ndiyo Wataalam wanadai ni alama ya usalama.
Burnley v Man City
Wiki iliyopita, Burnley walifungwa hapohapo kwao Turf Moor kwa bao la penalti ya utata mkubwa walipocheza na Blackburn na sasa wanaikaribisha Man City ambao wako kwenye vita ya kuiwania nafasi ya 4.
Birmingham City v Liverpool
Baada ya kupigwa 2-1 na Benfica huko Ureno kwenye EUROPA LIGI, Jumapili Liverpool wanasafiri hadi kwenye Uwanja wa Mtakatifu Andrew kuikwaa Birmingham ambayo ni kigaga wakiwa hapo na hawajafungwa hapo tangu Septemba.
Fulham v Wigan
Fulham waling’ara Alhamisi walipoichapa Wolfsburg 2-1 kwenye EUROPA LIGI na Jumapili wanarudi tena Craven Cottage kucheza na Wigan.
Fulham wako nafasi ya 12 lakini wamefungwa mechi zao 3 za mwisho za Ligi na watataka kubadilisha hali hiyo.
Wigan nao wako chini ingawa si katika zile Timu 3 za mkiani na matokeo mazuri katika mechi zilizosalia zitawapa ahueni zaidi.
Everton v West Ham
Baada ya vipigo 6 mfululizo, uvumi ulizagaa Kocha Gianfranco Zola yuko mguu nje hapo West Ham lakini Zola akauzima uvumi huo na kuipa Timu yake ofu ya siku 3 ili watulize akili.
Everton hawajafungwa katika mechi 5 na wapo nafasi ya 8.
Fergie: “Rooney kurudi baada ya Wiki 3”
Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, leo amethibitisha kuwa Staa Wayne Rooney atakuwa nje kwa wiki 2 hadi 3 akiuguza enka yake aliyoumia kwenye mechi na Bayern Munich siku ya Jumanne huko Ujerumani.
Ferguson, akiongea leo, amesema: Taifa lipumue sasa! Tumepata nafuu kwani ingekuwa vibaya sana!”
England yote ilikumbwa na wasiwasi kuwa Wayne Rooney ameumia vibaya na huenda akaikosa Fainali za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini zinazoanza Juni 11.
Ferguson akaongeza: “Atazikosa mechi zetu muhimu lakini cha muhimu ni kuwa atarudi kabla ya Msimu kwisha na kutusaidia mechi za Ligi zilizobaki.”
Rooney, ambae amefunga mabao 34 Msimu huu, ataikosa mechi ya kesho na Chelsea na ile ya Jumatano ijayo ya marudiano na Bayern Munich.
Mechi nyingine atakayoikosa ni ile ya ugenini ya Ligi Man United watakapocheza na Blackburn lakini ikiwa atapona haraka na vizuri anaweza kuingia dimbani kuivaa Man City hapo Aprili 17
BIGI MECHI: Manchester United v Chelsea—Refa ni Mike Dean!!!
• Meneja Burnley aita uteuzi wa Dean ni ‘wehu!”
Uteuzi wa Refa Mike Dean kuchezesha lile pambano la Vigogo wa Ligi Kuu, Manchester United v Chelsea, la kesho Jumamosi huko Old Trafford ambalo Wadau wanaamini Mshindi ndie Bingwa, umeitwa ni wehu na Meneja wa Burnley Brian Laws kufuatia uchezeshaji wa Refa huyo wiki iliyopita katika mechi ya Ligi Kuu kati ya Burnley na Blackburn ambapo Mike Dean aliipa Blackburn penalti tata waliyofunga bao lao la ushindi.
Uteuzi wa Refa Mike Dean, ambae ni Refa wa FIFA tangu 2002, umefanywa na Kampuni inayosimamia Marefa wa Kulipwa inayoitwa ‘Professional Game Match Officials Ltd (PGMOL)’.
Mike Dean, miaka 41, mara ya mwisho kuchezesha mechi ya Man United v Chelsea ni Septemba 2007 na alimpa Kadi Nyekundu Jon-Obi Mikel na pia kuwapa Man United penalti dakika za mwisho na Man United walishinda mechi hiyo 2-0 Uwanjani Old Trafford.
Meneja huyo wa Burnley, Brian Laws, amedai Refa Mike Dean alihadaiwa na Mchezaji wa Blackburn Martin Olsson aliejidondosha kusudi akivunga Kipa wa Burnley Brian Jensen alimgusa.
Marudio ya mikanda ya video yalionyesha waziwazi Olsson hakuguswa na Jensen.
Mwenyewe Olsson alikiri baadae “uongo” wake na kusema alifanya hivyo kwa vile wanajua Refa Dean ndie anaongoza kwa kutoa penalti nyingi Ligi Kuu.
Laws amestushwa na uteuzi wa Mike Dean kuchezesha pambano kubwa na muhimu la Man United v Chelsea na amesema: “Ni wehu kumpa Refa huyu mechi hiyo kubwa!”
Laws aliongeza kwa kusema kwa kuwa kumekuwa na malamiko makubwa kuhusu penalti hiyo waliyopewa Blackburn ambayo hawakustahili kuna hatari Dean akaingia kwenye hiyo BIGI MECHI huku akiwa na mawazo ya kutokutoa penalti na hilo huenda likainyimaTimu penalti ya wazi na kweli.
Kutolewa Chelsea UEFA nafuu kwao, Man United na Arsenal waumizwa UEFA!!
Rooney, Fabregas majeruhi!!!!
Huenda Chelsea walipofumuliwa 2-1 na 1-0 na Inter Milan na kubwagwa nje ya UEFA CHAMPIONS LIGI waliona ni balaa kubwa na kuwaacha wenzao Manchester United na Arsenal wakipeta kuingia Robo Fainali ya Mashindano hayo makubwa kwa Klabu huko Ulaya lakini ushiriki wa Manchester United na Arsenal ambako juzi Man United walifungwa 2-1 na Bayern Munich huko Ujerumani na Arsenal kutoka sare 2-2 na Barcelona Uwanjani Emirates, umeleta hasara kubwa na athari kubwa kwa Klabu hizo mbili zinazofukuzana na Chelsea kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu.
Manchester United, ambao kesho Uwanjani kwao Old Trafford wanaivaa Chelsea katika BIGI MECHI ambayo Wadau wanaamini mshindi ndie Bingwa, wataingia Uwanjani bila ya Nyota wao Wayne Rooney alieumia katika mechi na Bayern Munich Jumanne iliyopita.
Arsenal, ambao wapo pointi 4 nyuma ya vinara Man United na pointi 3 nyuma ya Timu ya pili Chelsea, nao walipata pigo kubwa pale Nahodha wao Cesc Fabregas alipovunjika mfupa mmoja wa mguu wake alipogongana na Nahodha wa Barcelona Carles Puyol Timu hizo zilipocheza Jumatano.
Wakati Rooney anategemewa kupona na kurudi Uwanjani ndani ya Wiki 4 na hivyo kuwahi mechi za mwisho za Ligi Kuu inayomalizika Mei 9, Fabregas inaaminika Msimu wake ndio umekwisha na ushiriki wake kwenye Timu ya kwao Spain inayocheza Fainali za Kombe la Dunia litakaloanza Afrika Kusini Juni 11 pia una hatihati.
Mbali ya Fabregas, Arsenal pia waliathirika mno katika mechi hiyo na Barcelona pale William Gallas na Andrey Arshavin kuumia na inasadikiwa wawili hao watakuwa nje kwa kipindi kirefu na huenda Msimu kwao ukawa umekwisha.
EUROPA LIGI: Liverpool chali Ureno, Fulham yapeta nyumbani!!
Benfica 2 Liverpool 1
Fulham 2 v Wolfsburg 1
Hamburg 2 v Standard Liege 1
Valencia 2 v Atletico Madrid 2
================================
Benfica 2 Liverpool 1
Penalti mbili zilizopigwa na Oscar Cardozo wa Benfica ndizo zilizoiua Liverpool kwenye mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya EUROPA LIGI iliyochezwa Estadio da Luz huko Lisbon, Ureno.
Liverpool walikuwa ndio wa kwanza kupata bao baada ya frikiki ya Steven Gerrard kumaliziwa kifundi na Daniel Agger aliebetua mpira na kufunga hiyo ikiwa dakika ya 9 tu ya mchezo.
Katika dakika ya 30, Liverpool wakajikuta wako mtu 10 pale Babel alipofanya ujinga wa kumsukuma Luisao usoni na Refa Jonas Eriksson kutoka Sweden akamtwanga Babel Kadi Nyekundu.
Babel alikuwa amechukizwa na kitendo cha Luisao kumkata Fernando Fernando Torres kwa nyuma tukio ambalo Refa aliamua ni faulo na kumpa Kadi ya Njano Luisao.
Hadi mapumziko Benfica o Liverpool 1.
Kipindi cha pili Benfica walipata bao la kusawazisha lililioanzia kwa frikiki ya Cardozo nje ya boksi kugonga mwamba na katika kizaazaa golini mwa Liverpool, Beki Insua akamkata Aimar na penalti ikatolewa.
Cardozo akapiga penalti ya chini iliompita Kipa Pepe Reina na kufanya mechi iwe 1-1 katika dakika ya 59.
Kwenye dakika ya 79 krosi ya Di Maria ilimkuta Mlinzi Carragher akiwa mikono mbele na kuucheze mpira huo kwa mkono na Msaidizi wa Refa akamwashiria Refa Eriksson kuwa ni penalti.
Alikuwa Cardozo tena mpigaji wa penalti na alimchambua Kipa Reina kwa mara ya pili na kuandika bao la ushindi kwa Benfica.
Katika mechi ya marudio, Liverpool itamkosa Insua, ambae tayari alikuwa na Kadi ya Njano kabla ya mechi, jana alilambwa tena Kadi ya Njano na hivyo atafungiwa mechi hiyo ya Aprili 8.
Vikosi vilivyoanza:
Benfica: Julio Cesar, Luisao, Pereira, David Luiz, Javi Garcia, Ramires, Aimar, Carlos Martins, Fabio Centrao, Di Maria, Cardozo
Liverpool: Reina, Jonhson, Agger, Carragher, Insua, Gerrard, Mascherano, Lucas,Torres, Kuyt, Babel
Fulham 2 Wolfsburg 1
Fulham wakiwa kwao Craven Cottage walifanikiwa kuifunga Wolfsburg bao 2-1 katika mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya EUROPA LIGI.
Mechii hii ilikuwa ngumu na ngome zote zilisimama imara na kufanya nafasi kwa kila upande kuwa nadra sana.
Lakini alikuwa Mshambuliaji anaeng’ara ambae wengi wamepiga mbiu awemo Kikosi cha England cha Kombe la Dunia, Bobby Zamora, alieipatia Fulham bao la kwanza katika dakika ya 59 kwa shuti la kupinda akiwa mita kama 20 nje ya goli.
Dakika 4 baadae, Damien Duff akapachika bao la pili kufuatia Beki wa kushoto Konchesky kupanda juu na kumtilia krosi Zamora alieubembeleza mpira kwenye njia ya Duff aliefunga kwa kujiamini.
Lakini Mabingwa wa Ujerumani, Wolfsburg, wamejipa matumaini pale walipopata goli la ugenini lililofungwa na Madlung dakika ya 89.
Vikosi vilivyoanza:
Fulham: Schwarzer, Hughes, Hangeland, Konchesky, Danny Murphy, Simon Davies, Dickson Etuhu, Bobby Zamora, Damien Duff, Zoltan Gera, Dempsey.
Wolfsburg: Benaglio, Madlung, Barzaqli, Schafer, Pekarik, Josue, Misimovic, Gentner, Edin Dzeko, Grafite

Thursday 1 April 2010

Leo ni EUROPA LIGI!
Leo Ulaya, kuanzia saa 4 dakika 5, saa za bongo, kutakuwa na mechi 4 za kwanza za Robo Fainali ya Kombe la EUROPA LIGI na Timu mbili za England, Liverpool na Fulham, bado zipo kwenye mtanange huo. 
Wakati Liverpool yuko ugenini kuivaa Benfica, Fulham yuko nyumbani na atacheza na Wolfsburg.
Mechi nyingine za leo ni Hamburg v Standard Liege na Valencia v Atletico Madrid ikiwa ni mechi ya Timu za Hispania tu.
TATHMINI: 
Benfica v Liverpool
Liverpool leo wapo Estadio da Luz huko Ureno kuchuana na Benfica katika mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya EUROPA LIGI na Timu hizi zitarudiana Anfield hapo Aprili 8.
Katika Msimu wa Mwaka 2005/6, Benfica waliibwaga Liverpool nje ya UEFA CHAMPIONS LIGI katika Raundi ya Mtoano ya Timu 16 pale walipoipiga nje na ndani na leo watataka kurudia historia hiyo.
Msimu huu, Benfica iliwatandika Mahasimu wa Liverpool, Everton, katika mechi zote mbili za Makundi ya EUROPA LIGI na Benfica wanaingia kwenye mechi ya leo kwa kujiamini kwa vile wao ndio vinara wa Ligi yao huko Ureno wakiwa mbele kwa pointi 6 dhidi ya Timu inayowafuata.
Kwa Liverpool, EUROPA LIGI ndie mkombozi wao pekee wa Msimu ulioparaganya kwao baada ya kutupwa nje katika kila Kombe na kwenye Ligi Kuu wanachopigania ni, pengine, nafasi ya 4 ambayo hata hiyo haimo mikononi mwao.
Hivyo matokeo mazuri kwa Liverpool katika mechi ya leo ni jambo wanalotaka ili wawe katika nafasi nzuri hapo Aprili 8 watakaporudiana na Benfica huko Anfield.
Katika Kikosi chao, Wachezaji watakaokosekana kwa Liverpool ni Kiungo Alberto Aquilani ambae aliumia enka mazoezini na Maxi Rodriguez ambae haruhusiwi kucheza kwani awali alichezea Klabu nyingine kwenye Mashindano haya.
Wengine ni Martin Skrtel na Fabio Aurelio ambao ni majeruhi wa muda mrefu.
Albert Riera nae ameachwa kabisa kwa matatizo ya nidhamu baada ya kumkashifu Meneja Rafa Benitez.
Nae Staa wa Liverpool, Fernando Torres, ataicheza mechi ya leo kwa tahadhari kubwa kwani anayo Kadi ya Njano na akipewa nyingine leo hataruhusiwa kucheza mechi ya marudiano kati ya Timu hizi mbili.
Nao Benfica watamkosa Mchezaji toka Argentina Javier Saviola ambae ameumia mguu lakini Mfungaji wao bora, Oscar Cardozo, anategemewa kuwepo kilingeni.
Fulham v Wolfsburg
Fulham wapo nyumbani Craven Cottage kucheza na Mabingwa wa Ujerumani na wataombea mwendo wao mzuri kwenye Kombe hili uendelee hasa baada ya kuwabwaga Mabingwa Watetezi wa Kombe hili Shakhtar Donetsk na Vigogo wa Italia Juventus.
Ingawa Woflsburg hawapo timamu msimu huu kwenye Bundesliga na hawategemewa kuutetea vyema Ubingwa wao, Timu hii imeshinda mechi yao ya mwisho huku Fulham wakiwa wametandikwa mechi 3 mfululizo tangu waibwage Juventus bao 4-1.
Fulham watawakosa Nicky Shorey na Stefano Okaka ambao hawaruhusiwi kucheza kwa vile awali walichezea Timu nyingine.
Pia Wachezaji Andrew Johnson na John Paintsil wako nje kwa kuwa ni majeruhi.
Kwa Wolfsburg wasiwasi wao mkubwa ni kama Muuaji wao mkuu Edin Dzeko atakuwa fiti kwani aliumia mazoezini.
Fabregas nje Msimu wote!!
Nahodha wa Arsenal Cesc Fabregas ataukosa Msimu wote uliobaki baada ya kuvunjika mfupa wa mguu wake katika mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI siku ya Jumatano Uwanjani Emirates Arsenal walipotoka droo ya 2-2 na Barcelona.
Fabregas alivunjika mguu huo alipogongana na Carles Puyol na kupata penalti kwa tukio hilo.
Uchunguzi wa Madaktari umethibitisha Fabregas anahitaji si chini ya wiki 6 ili kupona na Msimu wa Ligi Kuu unakwisha Mei 9.
Mchezaji mwingine wa Arsenal ambae huenda akawa nje hadi Msimu unakwisha ni Beki William Gallas ambae alijitonesha musuli ya mguu ambayo ilimweka nje kwa muda mrefu kabla ya kucheza mechi hiyo na Barcelona na kujiumiza tena.
Pia, inasemekana Fowadi Andrey Arshavin, ambae pia aliumia kwenye mechi na Barcelona, huenda akawa nje muda mrefu ingawa ufafanuzi haukutolewa.
Rooney hakuumia sana! 
Mshambuliaji wa England Wayne Rooney atakuwa fiti kucheza Fainali za Kombe la Dunia baada ya uchunguzi wa Madaktari kuthibitisha hakuvunjika mfupa na wala hakuumia vibaya sana.
Habari hizo zimetolewa na Klabu yake Manchester United ingawa ufafanuzi zaidi haukutolewa na inategemewa Meneja wa Klabu hiyo, Sir Alex Ferguson, atazungumzia suala la Rooney kesho Ijumaa.
Rooney aliumia kwenye mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI huko Ujerumani ambako Bayern Munich waliifunga Man United bao 2-1 siku ya Jumanne.
Baada ya kuumia Rooney England yote ilikuwa na wasiwasi kuwa Mchezaji huyo huenda ameumia vibaya na hivyo kuikosa Fainali ya Kombe la Dunia itakayoanza Juni 11.
Msimu huu Rooney ameifungia Manchester United bao 34 na pia amefunga bao 9 kwa England katika mechi za mchujo za Kombe la Dunia.
UEFA CHAMPIONS LIGI:
Arsenal 2 Barcelona 2
Ni mechi waliyotawala Barcelona hasa kipindi cha kwanza na kama si ushujaa wa Kipa Manuel Almunia basi Barca wangekuwa mbele hata goli 5.
Lakini hadi mapumziko bao zilikuwa 0-0.
Kipindi cha pili kuanza tu, Shujaa Almunia akageuka kuwa mkosaji mkubwa pale alipotoka golini bila sababu ya msingi na kumpa mwanya Zlatan Ibrahimovic kumvika ‘kanzu’ na kupachika bao sekunde 30 tu tangu mpira uanze.
Alikuwa Ibrahimovic tena alieipa Barca bao la pili na kumfanya kila mtu ajue Barca wataondoka Emirates na lundo la migoli.
Lakini Arsene Wenger akafanya mabadiliko yaliyobadilisha mchezo pale alipomtoa Beki Bacary Sagna na kumuingiza Theo Walcott na Walcott hakufanya ajizi akaifungia Arsenal bao moja dakika ya 69 na kuwapa uhai.
Kwenye dakika ya 85, Refa Busacca akaipa Arsenal penalti baada ya kuamua Nahodha wa Barca Puyol alimchezea rafu Fabregas na pia kumpa Puyol Kadi Nyekundu.
Marudio ya tukio hilo yalionyesha ni uamuzi wa makosa.
Fabregas akafunga penalti hiyo na kuifanya ngoma iwe sare 2-2.
Timu hizi zitarudiana Nou Camp Aprili 6 huku Barcelona ikihitaji sare ya 0-0 au 1-1 ili ipite kwa vile wana magoli mawili ya ugenini.
Mechi hiyo ya marudio itachezwa huku kila Timu ikiwa haina Nahodha kwa vile Fabregas alipewa Kadi ya Njano ikiwa ni ya pili na Puyol alipata Kadi Nyekundu.
Vile vile Beki wa Barca Gerrard Pique ataikosa mechi hiyo kwa kupewa Kadi ya Njano ikiwa ni ya pili.
Hivyo, Barcelona watacheza mechi hiyo ya marudiano bila ya Masentahafu wao wa kawaida Puyol na Pique.
Vikosi vilivyoanza:
Arsenal: Almunia, Sagna, Gallas, Vermaelen, Clichy, Song, Fabregas, Diaby, Nasri, Bendtner, Arshavin
Barcelona: Valdes, Dani Alves, Pique, Puyol, Maxwell, Messi, Keita, Busquets, Xavi, Pedro, Ibrahimovic.
Refa: Massimo Busacca [Switzerland]
Inter Milan 1 CSKA Moscow 0
Ndani ya San Siro, Mshambuliaji Milito aliipa Inter Milan ushindi wa bao 1-0 alipofunga goli hilo dakika ya 65 ya Kipindi cha Pili.
Timu hizi zitarudiana huko Moscow Aprili 6.
Vikosi vilivyoanza:
Inter Milan: Julio Cesar, Maicon, Materazzi, Samuel, Zanetti, Stankovic, Cambiasso, Eto’o, Sneijder, Pandev, Milito.
CSKA Moscow: Akinfeev, Vasili Berezutsky, Alexei Berezutsky, Ignashevich, Shchennikov, Krasic, Aldonin, Semberas, Mamaev, Honda, Necid.
Refa: Howard Webb [England]

Wednesday 31 March 2010

Wenger hatishiki na Barca
Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, amesema wao hawaiogopi Barcelona ambayo leo wanapambana nayo Uwanja wa Emirates kwenye mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Wenger ametamka: “Lazima tuwe Mashujaa na kupigana! Unachotaka toka Timu yako ni kutojali ubora wa Barcelona na kukazania ubora wetu! Ni kweli wao ni Timu nzuri lakini hata sisi ni Timu bora!”
Barcelona ni tishio hasa kwa vile wanae mmoja wa Wachezaji bora duniani, Lionel Messi, anaesaidiwa na kina Zlatan Ibrahimovic, Andreas Iniesta, Xavi na Mchezaji wa zamani wa Arsenal, Thiery Henry.
Katika mechi ya leo huenda Arsenal wakamkosa Nahodha wao, Cesc Fabregas, ambae ni majeruhi ingawa upo uwezekano mdogo akacheza.
Lisi ya FIFA ya Ubora Duniani: Spain vinara, Brazil wa pili na Bongo ni 108!!!
Katika Listi ya FIFA ya Ubora Duniani kwa mwezi huu iliyotolewa leo, Spain bado nambari wani, Brazil ni wa pili, Uholanzi ni nambari 3 na England ni wa 7.
Tanzania ipo nafasi ya 108 na imeporomoka nafasi 2.
Timu ambayo imepata mafanikio makubwa ni Senegal iliyopanda nafasi 22 na kushika ya 72.
EUROPA LIGI: Kesho Viwanja Ulaya kundirima Robo Fainali!!
Alhamisi, Aprili 1
[saa 4 dak 5 usiku]
Benfica v Liverpool
Fulham v Wolfsburg
Hamburg v Standard Liege
Valencia v Atletico Madrid
Alhamisi, Aprili 8
Atletico Madrid v Valencia
Liverpool v Benfica
Standard Liege v Hamburg
Wolfsburg v Fulham
Kesho Viwanja mbalimbali Ulaya vitawaka moto kwa mechi za kwanza za Robo Fainali ya EUROPA LIGI na Liverpool na Fulham ndio Timu toka Ligi Kuu England ambazo bado zimo kwenye hatua hii.
Liverpool watakuwa ugenini huko Ureno kuwakwaa Benfica na hii ni mechi kubwa mno kwa Liverpool kwani Mashindano haya ndio pekee yanayoweza kuwapa Kombe Liverpool msimu huu.
Wenzao Fulham wako nyumbani Craven Cottage na wataumana na Mabingwa Watetezi wa Bundesliga Wolfsburg.
Marudiano ya mechi za Robo Fainali ni wiki ijayo Aprili 8.
Mourinho achoshwa na Wataliana!
Meneja machachari na mwenye vituko na mbwembwe, Jose Mourinho, ameibua mjadala kuhusu hatima yake katika Soka la Italia baada ya kutamka kuhusu Soka huko Italia: “Silipendi na halinipendi”
Mourinho, ambae ni Meneja wa Inter Milan, amegoma kuongea na Waandishi wa Habari baada ya kupigwa Faini Pauni 35,000 na kufungiwa na Chama cha Soka cha Italia kwa kuwakandya Marefa.
Mourinho amesema: “Nina furaha na Inter lakini sina furaha na Soka la Italia!”
Mourinho, miaka 47, ameongeza: “Siku zote nazungumza toka moyoni lakini nikizungumza yaliyo moyoni kuhusu Soka ya Serie A watanifungia!’
Inter Milan leo usiku inacheza na CSKA Moscow kwenye mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI na kwenye hatua iliyopita Inter waliibwaga Klabu ya zamani ya Mourinho, Chelsea.
Kuna uvumi mkubwa kuwa Mourinho yuko mbioni kurudi Uingereza kuiongoza mojawapo ya Klabu za Ligi Kuu ingawa si Klabu yeyote wala yeye mwenyewe aliethibitisha hilo.
Rooney nje wiki 4!
Wayne Rooney huenda akawa nje ya uwanja kwa wiki hadi nne baada ya kuteguka enka kwenye mechi ya jana ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI ambayo Manchester United walifungwa na Bayern Munich bao 2-1 kwenye Uwanja wa Allianz Arena huko Munich, Ujerumani.
Ingawa inasemekana maumivu ya Rooney si makubwa sana na ya kutisha lakini ni wazi atazikosa mechi za Man United na Chelsea ya Ligi Kuu siku ya Jumamosi na marudio ya Man United na Bayern Munich Jumatano ijayo.
ROBO FAINALI UEFA CHAMPIONS LIGI: Na leo tena!!!
Arsenal v Barcelona
UWANJA: Emirates Saa: 3 dakika 45 usiku [Bongo]
Hili ni pambano ambalo wengi wanalingojea kwa hamu kubwa hasa kwa vile Timu zote zinasifika kwa kucheza ‘Soka tamu’.
Wakati Arsenal walitoka droo 1-1 na Birmngham kwenye mechi yao ya mwisho ya LIgi Kuu, Barcelona wao wameshinda mechi zao 4 za mwisho za La Liga.
Timu zote hucheza mchezo wa kushambulia na kumiliki mpira na mara nyingi mechi zao huwa na mabao mengi.
Nahodha wa Arsenal, Cesc Fabregas, huenda asicheze mechi hii kwa vile ameumia na kutocheza kwake ni pengo kubwa mno kwa Arsenal.
Hata hivyo Arsenal ina uhakika wa kina Sami Nasri, Andrey Arshavin, Eduardo na Nicklas Bendtner kucheza.
Hata Beki wao wa kutumainiwa, William Gallas, huenda akawa dimbani baada ya kupona na kuanza mazoezi.
Barcelona ni moja ya Timu zinazotegemewa kutwaa Kombe la UEFA CHAMPIONS LIGI hasa kwa vile wao ndio Mabingwa Watetezi.
Barca wanamtegemea sana mmoja wa Wachezaji wanaosifika kuwa ni Bora Duniani-Lionel Messi.
Messi msimu huu amefunga bao 4 kwenye Mashindano haya ya Ulaya na ana jumla ya bao 32 Msimu huu.
Ingawa Messi ndie hatari kubwa ya Barcelona, lakini ukweli ni kuwa bila ya Viungo Andres Iniesta na Xavi, Barca ni Timu ya kawaida tu.
Hata hivyo Iniesta ni majeruhi na huenda asionekane kabisa.
Kwa staili zao za uchezaji, hii ni mechi inayonukia bao nyingi.
Inter Milan v CSKA Moscow
UWANJA: San Siro Saa: 3 dakika 45 usiku [Bongo]
CSKA Moscow wamekuwa na Msimu mzuri kwenye UEFA na wametinga Robo Fainali baada ya kuitandika Sevilla 2-1 huko Spain.
Inter Milan, chini ya Kocha wa zamani wa Chelsea Jose Mourinho, waliipiga Chelsea nje ndani, 2-1 Uwanjani San Siro na 1-0 huko Stamford Bridge, na kujikita Robo Fainali.
Inter Milan wanaingia kwenye mechi hii huku wakiwa wanayumba kidogo kwenye Serie A ingawa bado vinara kwani katika mechi zao 5 za mwisho wameshinda moja, suluhu 2 na wamefungwa 2.
CSKA Moscow ndio kwanza wako freshi kwani Ligi ya Urusi ndio kwanza imeanza tu huku CSKA wakiwa wamecheza mechi 3 tu na kushinda mbili, suluhu 1.
Katika Mashindano haya ya UEFA, Wafungaji wa CSKA ni Milos Krasic na Alan Dzagoev.
Inter Milan wamepata mabao yao kwenye UEFA kupitia Samuel Eto’o, Alberto Diego Milito na Dejan Stankovic.
Ushindi kwa Inter Milan wakiwa kwao San Siro ni muhimu hasa ukizingatia marudio ni Moscow ambako ni pagumu mno kushinda hasa kwa vile mechi inachezwa kwenye uwanja wenye nyasi bandia ambazo ni taabu kuchezea kama hujazizoea.

Tuesday 30 March 2010

Bayern 2 Man United 1
Bayern Munich wakiwa kwao Allianz Arena wameifunga Manchester United bao 2-1 katika Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI.
Man United ndio waliokuwa wa kwanza kupata bao dakika ya pili tu baada ya frikiki ya Nani kuparazwa na Beki wa Bayern kwa kichwa na kumkuta Wayne Rooney aliefunga kifundi.
Bayern walisawazisha kwenye dakika ya 77 baada ya frikiki ya Frank Ribery kumbabatiza Rooney na kumbabaisha Kipa Van der Sar.
Huku mechi ikielekea kuwa sare, Bayern walipata bao dakika ya mwisho Mfungaji akiwa Ivica Olic.
Timu hizi zitarudiana Old Trafford Aprili 7.
Vikosi vilivyoanza:
Bayern Munich: Butt, Lahm, Van Buyten, Demichelis, Badstuber, Altintop, Van Bommel, Pranjic, Ribery, Muller, Olic
Man United: Van der Sar, Neville, Evra, Ferdinand, Vidic, Nani, Carrick, Fletcher, Schole, Park, Rooney
Refa: Frank De Bleeckere [Ubelgiji]
Lyon 3 Bordeaux 1
Lyon wameanza vyema Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI baada ya kuwafunga Wafaransa wenzao Bordeaux bao 3-1 Uwanjani Stade Gerland.
Marudio ni Aprili 7.
Vikosi vilivyoanza:
Lyon: Lloris, Reveillere, Cris, Bodme, Cissokho, Makoun, Toulalan, Delgado, Pjanic, Michel Bastos, Lopez.
Bordeaux: Carrasso, Chalme, Sane, Ciani, Tremoulinas, Gouffran, Plasil, Menegazzo, Wendell, Gourcuff, Chamakh.
Drogba kifungo mechi 2 UEFA!
Mshambuliaji wa Chelsea, Didier Drogba, ameadhibiwa kufungiwa mechi 2 za Mashindano ya UEFA baada ya kupewa Kadi Nyekundu katika mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI kati ya Chelsea na Inter Milan Uwanjani Stamford Bridge ambayo Chelsea alifungwa 1-0.
Drogba alipewa Kadi hiyo dakika ya 87 kwa kumtimba Mchezaji wa Inter Milan Thiago Motta.
Msimu uliokwisha katika mechi ya Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI uwanjani Stamford Bridge kati ya Chelsea na Barcelona ambayo Barcelona walisawazisha bao dakika za majeruhi na kufanya mechi iwe 1-1 na hivyo kutinga Fainali kwa goli la ugenini, Drogba alimvaa Refa Tom Henning Ovrebo na kumtolea maneno makali mara tu baada ya filimbi ya mwisho.
Kwa kitendo hicho, Drogba alifungiwa mechi 4 lakini zikapunguzwa hadi 3 na mechi mbili zikawekwa kiporo kuchunguza mwenendo wake.
Safari hii, kwa kosa hilo la kutolewa kwenye mechi na Inter Milan, UEFA ingeweza kumfungia mechi 2 na kuziongeza hizo mechi mbili alizowekewa kiporo lakini UEFA imeamua kumfungia mechi mbili 2 na kuongeza muda wake wa kuwa chini ya uangalizi uwe hadi miezi 24 na hivyo utaisha Julai 2013.
Drogba amepewa siku 3 kukata rufaa adhabu hizo.
Martinez alaumu Refa kwa kufungwa!
Man City 3 Wigan 0
Bosi wa Wigan Roberto Martinez amemlaumu Refa Stuart Attwell, miaka 27, kwa kumpa Kadi Nyekundu Mchezaji wake Gary Caldwell huku mechi ya Ligi Kuu kati ya Manchester City na Wigan ikiwa 0-0 na hivyo kutoa mwanya kwa Man City kushinda 3-0, bao zote zikiingizwa na Carlos Tevez katika kipindi cha pili katika muda uliochukua dakika 12 tu kwa bao zote kutinga.
Martinez amedai Refa Stuart Atwell, ambae ndie Refa mwenye umri mdogo kupita Refa yeyote kwenye Ligi Kuu, hakuiona rafu aliyotenda Caldwell kwa Tevez na hivyo hakustahili kutoa Kadi.
Martinez alifoka: “Kutoa Kadi Nyekundu ni lazima uwe na uhakika. Ukiangalia marudio ya tukio la rafu utaona ile si rafu! Refa hakuona, hivyo kutoa uamuzi kwa kitu usichoona ni udanganyifu!”
Kauli hizo za Martinez sasa zimefika kwenye ofisi za FA na wamesema wanachunguza na watatoa uamuzi wao wa kumchukulia hatua muda si mrefu ujao.
Bayern yaahidi kumdhibiti Rooney
Kocha wa Bayern Munich Loius van Gaal amesema ana uhakika Timu yake ina uwezo wa kumdhibiti Wayne Rooney leo watakapocheza na Manchester United Uwanja wa Allianz Arena, nyumbani kwa Bayern, kwenye mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI.
Van Gaal amedai ingawa Rooney ni Mchezaji bora sana wao wana uwezo wa kumkontroli na kushinda mechi hiyo.
Van Gaal amesema: “Tuna uwezo wa kuishangaza Timu yeyote! Bayern si Timu kubwa kama Man United lakini uwezo upo wa kufikia gemu yao!”
Nae Sir Alex Ferguson amesema wao wameongezeka ubora wa kucheza mechi za Ulaya na sasa wana ujuzi, uvumilivu na utulivu wa kushinda ugenini.
Mpaka sasa Man United, kwenye Mashindano ya UEFA CHAMPIONS LIGI, wameshinda mechi zao 7 za mwisho, hawajafungwa katika mechi 17 za ugenini na wameshinda mechi zao zote 4 walizocheza ugenini Msimu huu.
Newcastle wapiga hodi Ligi Kuu
Newcastle ambayo iliporomoshwa Daraja kutoka Ligi Kuu msimu uliokwisha huenda wikiendi hii inayokuja wakajihakikishia kurudi tena Ligi Kuu ikiwa wataifunga Peterborough kwenye Ligi ya Coca Cola Championship na Notingham Forest kufungwa na Bristol City.
Katika Ligi hiyo ya Championship, Newcastle ndio vinara wakiwa na pointi 83 kwa mechi 39, wa pili ni West Bromwich wakiwa na pointi 79 kwa mechi 40 na wa tatu ni Notingham Forest na wana pointi 70 kwa mechi 40.
Kila Timu inatakiwa icheze jumla ya mechi 46 na Timu mbili za juu ndizo zinapanda moja kwa moja kwenda Ligi Kuu.
Timu za nafasi ya 3 hadi ya 6 huandaliwa Mashindano maalum kuipata Timu moja itakayoungana na hizo mbili za juu kuingia Ligi Kuu.
ROBO FAINALI UEFA CHAMPIONS LIGI: Ni leo kindumbwembwe!!!
Bayern Munich v Manchester United
UWANJA: Allianz Arena Saa: 3 dakika 45 usiku [Bongo]
Hili ni pambano ambalo wengi linawakumbusha ile Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI mwaka 1999 ambayo Manchester United wakiwa nyuma bao 1-0 hadi dakika ya 90 walifanikiwa kuiliza Bayern Munich walipopachika bao 2 katika dakika 3 za nyongeza kwa bao za Teddy Sheringham na Ole Gunnar Solksjaer.
Lakini safari hii, hili ni pambano la Robo Fainali na hii ni mechi ya kwanza tu na marudio yake ni Aprili 7 huko Old Trafford nyumbani kwa Manchester United.
Man United wanatinga dimbani wakiwa katika fomu nzuri tu wakiwa wameshinda mechi 8 mfululizo na ya mwisho ikiwa ni ile ya Jumamosi walipoitandika Bolton bao 4-0.
Katika mechi hizo 8 Man United wamefunga jumla ya goli 19 na kufungwa 2 tu huku Rooney akifunga goli 8 na kufanya idadi yake ya magoli msimu huu iwe 33.
Man United wapo kileleni mwa Ligi Kuu.
Bayern Munich, baada ya kuanza Msimu wao kwa kusuasua, waliongeza kasi na nguvu na kuongoza Bundesliga lakini hivi karibuni mambo yameanza kwenda mrama.
Wikiendi hii iliyopita Bayern wameporwa uongozi wao wa Bundesliga na FC Schalke 04 walipotwangwa 2-1 wakiwa uwanja wao nyumbani na Stuttgart.
Kabla ya kipigo hicho, Bayern walipata ushindi mwembamba wa dakika za nyongeza wa bao 1-0 kwenye Kombe la DFB walipoifunga Schalke.
Na kabla ya ushindi huo, katika mechi zao 4 za mwisho, walishinda moja, suluhu moja na kupigwa mbili.
Katika mechi hii na Man United, Bayern huenda wakamkosa Staa wao Arjen Robben alieumia kwenye mechi na Stuttgart.
Lyon v Bordeaux
UWANJA: Stade Gerland Saa: 3 dakika 45 usiku [Bongo]
Hii ni mechi kati ya Klabu za Ufaransa Lyon wakiwa chini ya Kocha Claude Puel na Bordeaux wako chini ya Nahodha wa zamani wa Ufaransa Laurent Blanc ambae aliwahi kuichezea Manchester United.
Wakati Lyon inaingia dimbani ikiwa na Kikosi chake chote bila ya kuwa na majeruhi, Bordeaux watacheza bila Kiungo Alou Diarra ambae amefungiwa baada ya kutolewa kwa Kadi Nyekundu kwenye mechi iliyopita ya UEFA CHAMPIONS LIGI Bordeaux walipoibwaga Olympiakos.
Lyon walinyakua Ubingwa wa Ufaransa mara 7 mfululizo kabla ya kubwagwa na Bordeaux Msimu uliokwisha.
Lyon Msimu huu wamejizolea sifa kubwa walipoitoa Klabu Kubwa,Tajiri na yenye Wachezaji wa bei mbaya kina Ronaldo, Kaka na Benzema, Real Madrid, katika Raundi iliyopita ya UEFA CHAMPIONS LIGI.
Kipa wa Lyon, Hugo Lloris, amejigamba: “Hatushindani na Bordeaux, tunashindana sisi wenyewe! Lazima tuwafunge mechi hii ili tusonge mbele!”
Bordeaux ndio kwanza wametoka kwenye pigo kuu baada ya kufungwa kwenye Fainali ya Kombe la Ligi la Ufaransa na Olympique Marseille bao 3-1 hapo Jumamosi na Meneja Laurent Blanc amenena: “Si rahisi lakini ni bora tunacheza mapema Jumanne na hii ni nafasi kubwa kufuta majonzi yetu!”
Bordeaux msimu huu wameshaifunga Lyon wakiwa kwao Uwanja wao Stade Gerland bao 1-0 mwezi Desemba kwenye mechi ya Ligue 1.

Monday 29 March 2010

LIGI KUU leo: Man City v Wigan
• Adebayor kuwa na Tevez!
Straika wa Manchester City Emmanuel Adebayor leo anarudi uwanjani baada ya kutumikia kifungo chake cha mechi 4 na Kocha Roberto Mancini amesema atampanga acheze pamoja na Carlos Tevez ili kuleta nguvu mbele na kupata ushindi dhidi ya Wigan katika mechi ya Ligi Kuu leo Uwanjani City of Manchester.
Man City walipoteza mechi yao ya mwisho ya Ligi walipofungwa na Everton 2-0 hapo hapo nyumbani Uwanjani City of Manchester.
Mwaka huu, Tevez na Adebayor wamecheza pamoja mara 3 tu kati ya mechi 17 ambazo wangeweza kuwa pamoja kwa vile kwanza Adebayor alikuwa Angola kwenye Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kisha Tevez akapata udhuru wa kifamilia na kurudi kwao Argentina na aliporudi tu, Adebayor akafungiwa mechi 4 baada ya kutolewa kwa Kadi Nyekundu katika mechi na Stoke City.
Man City, pamoja na Tottenham, Liverpool na Aston Villa, wamo kwenye vita kati yao kuwania nafasi ya 4 ili kufuzu kucheza UEFA msimu ujao.
Tottenham ndie yuko nafasi hiyo ya 4 akiwa na pointi 58 kwa mechi 31, anafuata Liverpool mwenye pointi 54 kwa mechi 32, kisha Man City pointi 53 mechi 30 na wa 7 ni Aston Villa mwenye pointi 51 kwa mechi 31.
Vidic akwepa rungu la FA!
Beki wa Manchester United hatachukuliwa hatua yeyote na FA kufuatia tukio la yeye kumpasua kwa kiwiko Mchezaji wa Bolton Johan Elmander siku ya Jumamosi Man United ilipoifunga Bolton 4-0.
FA imethibitisha uamuzi huo kwa sababu Refa Martin Atkinson aliliona tukio hilo na kuamua ni bahati mbaya.
Meneja Bolton Owen Coyle alidai Elmander aliumizwa kusudi.
Eriksson kuongoza Tembo!!
Kocha wa zamani wa England Sven-Goran Eriksson ameteuliwa kuwa Kocha mpya wa Ivory Coast kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia lakini Shirikisho la Soka la Nchi hiyo halikutaja wadhifa huo utakuwa wa muda gani.
Mwezi uliokwisha Ivory Coast walimtimua Kocha wao kutoka Bosnia Vahid Halihodzic kwa kile kilichodaiwa kushindwa kuifikisha Nchi hiyo, maarufu kama ‘Tembo’, Nusu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika lililochezwa Angola mwezi Januari.
Tembo hao, wanaoongozwa na Mchezaji Bora wa Afrika anaechezea Chelsea Didier Drogba, wako Kundi G pamoja na Brazil, Ureno na Korea Kaskazini kwenye Fainali za Kombe la Dunia zitakazoanza huko Afrika Kusini Juni 11.
Eriksson alikuwa Kocha wa England kati ya mwaka 2001 na 2006 na aliiwezesha England kufika Robo Fainali za Kombe la Dunia mara mbili.
Baada ya kuiacha England, Eriksson alikuwa Meneja wa Manchester City na Mexico.
Hivi karibuni alikuwa Mkurugenzi wa Soka wa Klabu ya Notts County.
Kikosi imara chakwaa pipa kwenda Ujerumani
Rio Ferdinand na Wayne Rooney, ambao hawakucheza mechi ya Ligi Kuu ya Jumamosi ambayo Manchester United waliikung’uta Bolton 4-0, ni miongoni mwa Wachezaji 22 waliopanda ndege kwenda Ujerumani ambako Jumanne watacheza mechi ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI na Bayern Munich.
Sir Alex Ferguson amethibitisha Wachezaji hao wako fiti na watacheza Jumanne.
Kikosi kamili kilichosafiri ni: Edwin van der Sar, Ben Foster, Tomasz Kuszczak, Gary Neville, Rafael, Nemanja Vidic, Jonny Evans, Rio Ferdinand, Patrice Evra, Ritchie De Laet, Michael Carrick, Darren Fletcher, Darron Gibson, Paul Scholes, Gabriel Obertan, Nani, Antonio Valencia, Ji-sung Park, Ryan Giggs, Wayne Rooney, Dimitar Berbatov, Federico Macheda.

Sunday 28 March 2010

Liverpool 3 Sunderland 0
Wakiwa kwao Anfield, leo Liverpool wameipiga Sunderland mabao 3-0 katika mechi ya Ligi Kuu na kuchukua nafasi ya 5 kwenye Ligi.
Hadi mapumziko Liverpool walikuwa mbele kwa bao 2 zilizofungwa na Fernando Torres na Glen Johnson.
Kipindi cha pili Torres akapachika bao moja zaidi na kufanya bao ziwe 3-0.
MSIMAMO LIGI KUU England baada ya mechi za leo kwa Timu 10 za juu:
1. Man United mechi 32 pointi 72
2. Chelsea mechi 32 pointi 71
3. Arsenal mechi 32 pointi 68
4. Tottenham mechi 31 pointi 58
5. Liverpool mechi 32 pointi 54
6. Man City mechi 30 pointi 53
7. Aston Villa mechi 31 pointi 51
8. Everton mechi 32 pointi 49
9. Birminghma mechi 32 pointi 45
10. Blackburn mechi 32 pointi 41
RATIBA
[SAA ZA BONGO]
Jumatatu, 29 Machi 2010
LIGI KUU
[saa 4 usiku]
Man City v Wigan
Jumanne, 30 Machi 2010
UEFA CHAMPIONS LIGI
[saa 3 dak 45 usiku]
Bayern Munich v Man United
Lyon v Bordeaux
Jumatano, 31 Machi 2010
UEFA CHAMPIONS LIGI
Arsenal v Barcelona
Inter Milan v CSKA Moscow
Injini ya Barca nje mechi na Gunners!!
Kiungo mahiri wa Barcelona Andres Iniesta ataikosa mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI Barca watapokuwa Uwanja wa Emirates kucheza na Arsenal siku ya Jumatano Machi 31 baada ya kuumia paja Jumamosi katika mechi ya La Liga ambayo Barcelona waliifunga Real Mallorca bao 1-0.
Ilibidi Iniesta atolewe nje mapema kipindi cha pili na nafasi yake kuchukuliwa na Lionel Messi aliepumzishwa kwa mechi hiyo.
Uchunguzi wa Madaktari umebaini Iniesta anatakiwa awe nje kwa siku 10.
Barcelona wataikaribisha Arsenal Nou Camp kwa mechi ya marudiano hapo Aprili 6.
Ribery na Robben ndio nguvu ya Bayern!!
Sir Alex Ferguson amesema Franck Ribery na Arjen Robben ndio tishio kubwa kwa Manchester United watakapoikwaa Bayern Munich siku ya Jumanne Uwanja wa Allianz Arena huko Ujerumani katika mechi ya kwanza ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI.
Ingawa Ferguson amekiri Ribery ni kipaji lakini amesema hawezi kuwapata Wayne Rooney na Lionel Messi.
Kuhusu Robben, Ferguson amesema Winga huyo ambae ni Mdachi ni hatari kwani hucheza Winga ya kulia ingawa mguu wake bora ni wa kushoto hivyo akipenya kuingia kati huachia mikwaju na guu lake la kushoto.
Hata hivyo, Ferguson amesema anaamini anao Mafulbeki wazuri wanaoweza kumdhibiti Robben.
Akikumbushia Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI ya mwaka 1999 Manchester United walipoibwaga Bayern Munich 2-1 na bao zote hizo mbili zikifungwa katika dakika3 za nyongeza za majeruhi, Fergie amesema: “Ile ilikuwa Fainali kiboko! Haiwezekani ikatokea tena! Kila wakati Timu ikiwa mbele 1-0 na zimebaki dakika 3 wataikumbuka Man United! Tulishindaje? Hata leo sijui, ni kudra tu! Lakini usisahau, Timu ile ilikuwa ikifunga magoli mengi mwaka ule dakika za majeruhi sasa hilo si bahati tu! Lakini ukiwa nyuma 1-0 na Refa wa Akiba anainua bango kuashiria dakika 3 za nyongeza, huwezi ukategemea utashinda mechi!”
Burnley 0 Blackburn 1
Leo katika mechi ya Ligi Kuu iliyoanza mapema, Blackburn Rovers wakiwa ugenini Uwanja wa Turf Moor wameitungua Burnley bao 1-0 kwa bao la penalti yenye utata iliyotolewa na Refa Mike Dean kwa madai Kipa wa Burnley Brian Jensen alimwangusha Martin Olsson wa Blackburn.
David Dunn ndie aliefunga bao hilo kwa penalti hiyo kwenye dakika ya 20.
Kipigo hicho kimeifanya Burnley ibaki nafasi ya pili toka mkiani na hivyo kuandamwa na balaa la kuporomoka Daraja.
Ushindi huu unazidi kuwakikishia Blackburn uhai wao kwenye Ligi Kuu.
Mechi ya Ligi Kuu inayofuata baadae leo ni ile mechi ya kumbukumbu ya goli la ‘Bichi Boli’ kati ya Liverpool na Sunderland.
Katika mechi ya kwanza, Sunderland waliifunga Liverpool bao 1-0 lililofungwa na Darren Bent ambae shuti lake liliugonga mpira wa Bichi uliotupwa uwanjani na Shabiki wa Liverpool na kumbabaisha Kipa Reina na kutinga wavuni.
Wenger awaka baada ya droo!
Baada ya jana Timu yake kubanwa na Birmingham na kutoka sare 1-1 Uwanja wa Mtakatifu Andrew, Meneja wa Arsenal Arsene Wenger aliwawakia Waandishi wa Habari waliokuwa wakimhoji baada ya mechi hiyo ya Ligi Kuu hapo jana.
Sare hiyo imewafanya Arsenal warudi nafasi ya 3 wakiwa pointi 4 nyuma ya vinara Manchester United na pointi 3 nyuma ya Timu ya pili Chelsea huku Timu zote zikiwa zimecheza mechi 32 na kubakisha 6.
Wenger alifoka baada ya Waandishi kumuuliza ikiwa anadhani Timu yake inachezewa rafu kusudi, Wenger alijibu kwa hasira: “Mnadhani nadai tunachezewa rafu kusudi? Hebu niacheni! Nikitoa maoni kuhusu mechi nyie mnatafuta utata tu!”
Waandishi hao walitaka kujua maoni ya Wenger baada ya Nahodha wake Cesc Fabregas kuumizwa na Craig Gardner hasa wakikumbuka hiyo ilikuwa ni mechi ya kwanza kwa Arsenal kurudi Uwanja wa Mtakatifu Andrew tangu miaka miwili iliyopita alipoumizwa Mchezaji wao Eduardo alievunjwa mguu na Mchezaji wa Birmingham Martin Taylor.
Katika mechi hiyo, huku Arsenal wakitafuta ushindi ili kujizatiti kuwania Ubingwa, Birmingham walisawazisha dakika za mwisho na kuyavunja matumaini ya Arsenal na hivyo ndivyo ilivyokuwa tena hapo jana wakati Mchezaji alietoka bench Kevin Phillips aliposawazisha kwa Birmingham kwenye dakika ya 92.
Nae Meneja wa Birmingham, Alex McLeish amepinga madai ya kwamba Arsenal wanachezewa rafu kusudi kwa kusema: “Sidhani hilo ni kweli! Hata wao Arsenal wanacheza rafu na ndio maana Refa kawapa Kadi Song na Clichy.”
Fergie asema ilikuwa vita kuwafunga Bolton!
Sir Alex Ferguson amesisitiza Manchester United iko tayari kujibu mapigo yoyote toka kwa Chelsea kufuatia Timu yake kuinyuka Bolton Wanderers bao 4-0 na ushindi huo ulifuata baada ya mapema jana Chelsea kuwafumua Aston Villa 7-1.
Siku ya Jumatano, Chelsea waliichabanga Portsmouth bao 5-0.
Hata hivyo Manchester United ndie anaeongoza Ligi akiwa na pointi 72 na Chelsea wana pointi 71.
Man United na Chelsea watakutana kwenye Ligi wikiendi ijayo Aprili 3 huko Old Trafford.
Kuhusu ushindi wa 4-0 juu ya Bolton waliokuwa wakicheza kwa miguvu na kukamia, Ferguson amesema: “Ilikuwa vita! Haftaimu nilimwambia Refa Martin Atkinson hii ni Soka sio vita! Refa alichezesha vizuri tu! Walitusakama kwa mipira ya juu na Vidic alikuwa na kazi kubwa kuokoa kwa kichwa!”
Hata hivyo katika moja ya mipira hiyo iliyookolewa na Vidic alimuumiza Straika wa Bolton Johan Elmander kwa kiwiko na ikabidi Straika huyo ashonwe nyuzi tano kichwani.
Meneja wa Bolton Owen Coyle amelalamikia kuumia kwa Elmander na kudai ilikuwa ni rafu na anadhani kama Refa angeona angemchukulia hatua Vidic.
Tukio hilo linaweza kumletea matatizo Vidic kwani endapo Refa hataliandika kwenye ripoti yake basi FA inaweza ikalichukulia hatua na kumfanya Vidic aikose mechi ya Jumamosi na Chelsea. Lakini Refa akisema kaliona basi hamna kitu anachoweza kufanywa Vidic.
Powered By Blogger