Saturday 26 December 2009

LIGI KUU England: MATOKEO MECHI ZA LEO Jumamosi, 26 Desemba 2009:
Birmingham 0 v Chelsea 0
Fulham 0 v Tottenham 0
West Ham 2 v Portsmouth 0
Burnley 1 v Bolton 1
Man City 2 v Stoke 0
Sunderland 1 v Everton 1
Wigan 1 v Blackburn 1
[MECHI INAANZA saa 2 na nusu usiku saa za bongo]
Liverpool v Wolves
MECHI ZA KESHO Jumapili, 27 Desemba 2009
[saa 10 na nusu jioni]
Arsenal v Aston Villa
[saa 1 usiku]
Hull v Man U
Chelsea wakwaa kisiki kwa Mtakatifu Andrews!!!
Timu vinara wa Ligi Kuu, Chelsea, leo Boksingi Dei Desemba 26, wameambulia pointi moja tu ugenini uwanja wa Mtakatifu Andrews walipotoka suluhu 0-0 na Wenyeji Birmigham.
Mchezaji wa Chelsea, Florent Malouda, alipewa Kadi Nyekundu na Mwamuzi Peter Walton baada ya kupewa Kadi 2 za Njano.
Kwa matokeo hayo Chelsea sasa wamecheza mechi 19 na wana pointi 42, Man U wakifuatia kwa mechi 18 pointi 37, Arsenal ni wa 3 mechi 17 pointi 35 na Aston Villa ni wa 4 mechi 18 pointi 35. 
Zote, Man U, Arsenal na Aston Villa zitacheza kesho huku Man U akiwa mgeni wa Hull City na Arsenal na Aston Villa zikipambana zenyewe huko Emirates Stadium.
VIKOSI:
Birmingham: Hart, Carr, Roger Johnson, Dann, Ridgewell, Larsson, Ferguson, Bowyer, McFadden, Jerome, Benitez.
AKIBA: Maik Taylor, Phillips, Fahey, McSheffrey, Damien Johnson, Carsley, Vignal.
Chelsea: Cech, Ivanovic, Terry, Alex, Ashley Cole, Belletti, Mikel, Malouda, Lampard, Drogba, Sturridge.
AKIBA: Hilario, Carvalho, Joe Cole, Ballack, Zhirkov, Paulo Ferreira, Kalou.
Katika mechi nyingine za leo zilizoanza mapema MATOKEO NI:
Fulham 0 Tottenham 0
West Ham 2 Portsmouth 0
Benitez aungama: “Torres hayuko fiti!!!!”
Meneja wa Liverpool Rafa Benitez amekubali kuwa Mshambuliaji wake nyota Fernando Torres hayuko fiti kucheza kila mechi na wanalazimika kumchunguza kwanza na halafu waamue kama acheze au la.
Msimu huu, Torres amekuwa nje mara kwa mara na kuna uvumi kuwa inabidi afanyiwe operesheni ya kutibu ngiri [hernia].
Katika mechi ya mwisho waliyocheza Liverpool na kufungwa 2-0 na Portsmouth kwenye Ligi Kuu, Torres alicheza chini ya kiwango lakini katika mechi ya leo ya Desemba 26 watakapocheza na Wolves kwenye Ligi Kuu, Mchezaji huyo anategemewa kuanza.
Liverpool, ambao wako pointi 8 nyuma ya Timu 4 za juu, wanakabiliwa na mechi ngumu 3 mfululizo baada ya mechi ya leo, kwenye Ligi Kuu, watacheza na Aston Villa, iliyo nafasi ya 4 kwenye Ligi, kisha watacheza na Reading kwenye Kombe la FA na baada ya hapo watapambana kwenye Ligi Kuu na Timu ya 5 kwenye Ligi, Tottenham.
Benitez anahaha kuhakikisha Straika wake yuko fiti lakini amekiri: “Ni lazima tumwangalie na kuhakikisha anacheza akiwa fiti tu!
Wakati huohuo, Benitez amekanusha taarifa kuwa alifanya mazungumzo na Nahodha wake Steven Gerrard ili kujadili kushuka kwa kiwango chake na kutojiamini kwake.
Mwenyekiti Arsenal aishambulia Barca!!!
Mwenyekiti wa Arsenal Peter Hill-Wood ameishambulia vikali Barcelona kwa kuwandama Nahodha wao Cesc Fabrega, miaka 22, na kujaribu kumrubuni ajiunge na Barcelona.
Mara kwa mara Barcelona imekuwa ikihusishwa na kumnunua Fabregas ambae alianza mpira akiwa kwenye Timu ya Vijana ya Barcelona na kisha kujiunga Arsenal.
Ingawa Real Madrid nao wanatajwa kutaka kumnunua Fabregas lakini ni Barcelona wakiongozwa na Rais wao Joan Laporta ndio vinara wa kumrubuni Kiungo huyo wa Arsenal mwenye asili ya Spain.
Na kauli za hivi karibuni za Joan Laporta zimemkera mno Mwenyekiti wa Arsenal, Peter Hill-Wood, aliefoka: “Nimechoka na uhuni huu wa Barcelona na upumbavu wao! Cesc ana Mkataba wa muda mrefu na mzuri na sisi! Yuko na sisi miaka 7 sasa na hana nia ya kuondoka! Hatuwezi kuwazuia kuongea ovyo lakini huu ni upuuzi uliokithiri!!”
LIGI KUU England: Yafikia Nusu, Uhamisho kufunguliwa Januari, je nini kitegemewe?
Ligi Kuu England wikiendi hii inafikia hatua muhimu ya Timu kufikia kucheza mechi 19 ambazo ni nusu ya mechi zote na vita kileleni iko wazi huku kuna Timu 8 zikigombea Ubingwa na nafasi 4 za kucheza UEFA CHAMPIONS LEAGUE msimu ujao na huko mkiani, ukitoa Timu hizo 8 zilizo fungu la kugombea Ubingwa, Timu zote zilizobaki, kimahesabu, zipo kwenye vita ya kukwepa kushuka Daraja.
Mwezi Januari dirisha la uhamisho litafunguliwa na kufungwa Januari 31 na kila Timu, pengine, itakuwa ikifikiria kuingia sokoni na kuimarisha Vikosi vyao. Lakini, kikawaida, biashara ya Wachezaji mwezi Januari ni ngumu na vile vile Klabu nyingi kwa sasa zinakabiliwa na matatizo ya kifedha.
Ifuatayo ni tathmini ya kila Klabu ie, nini kinahitajika, uwezo kifedha na Wachezaji gani walengwa:
ARSENAL
WANAHITAJI: Sentafowadi mwenye nguvu hasa baada ya kuumia kwa Robin van Persie na Nicklas Bendtner ambao wako nje kwa muda mrefu.
FEDHA: Arsenal wanasisitiza pesa wanazo ila tatizo ni kumlazimisha Arsene Wenger jinsi ya kuzitumia.
WALENGWA: Straika wa Wolfsburg Edin Dzeko ambae thamani yake ni Pauni Milioni 20 na mwingine ni Mchezaji wa Bordeaux Marouane Chamakh ambae Wenger amesita kumsaka kwa ajili ya bei yake.
ZIADA: Beki kutokaUswisi Philippe Senderos huenda akahamia Atletico Madrid.
ASTON VILLA
WANAHITAJI: Meneja Martin O'Neill anafurahishwa na mwenendo wa Klabu yake lakini anataka kusajili Straika mmoja.
FEDHA: Villa haijafuja pesa kama Klabu nyingine, hivyo, bila shaka, mfuko wao wa ununuzi wa Wachezaji bado umetuna.
WALENGWA:Kuna tetesi kuwa endapo Spurs wataamua kumuuza Nahodha wao Robbie Keane, Villa watamdaka.
ZIADA: Nicky Shorey na Nigel Reo-Coker ndio wanaohusishwa na uhamisho.
BIRMINGHAM
WANAHITAJI: Wachezaji zaidi wa viwango vya juu huku Straika akiwa juu ya listi yao.
FEDHA: Mmiliki wao Carson Yeung ameahidi kutoa Pauni Milioni 40 ili kununua Wachezaji.
WALENGWA: Listi yao ya ununuzi wamo Mchezaji wa Sporting Gijon Michel na Mchezaji wa Rangers Kris Boyd.
ZIADA: Huenda Kevin Phillips, Franck Queudrue na Teemu Tainio wakauzwa.
BLACKBURN
WANAHITAJI: Mfungaji magoli kwani wana uhaba mkubwa wa magoli. Vilevile, wameonyesha nia ya kuongeza Mkataba kwa Franco Di Santo ambae wamemkopa kutoka Chelsea.
FEDHA: Meneja Sam Allardyce aliufilisi mfuko wa kununua Wachezaji kabala Msimu kuanza hivyo atalazimika kuuza Wachezaji kabla ya kununua.
WALENGWA: Straika wa Stoke James Beattie na Beki kutoka Portsmouth Nadir Belhadj.
ZIADA: Winga Morten Gamst Pedersen na Mshambuliaji Benni McCarthy huenda wakauzwa.
BOLTON
WANAHITAJI: Kiungo mlinzi na Mshambuliaji.
FEDHA: Meneja Gary Megson ndie alietumia fedha kidogo kupita yeyote kwenye Ligi Kuu katika ununuzi wa Wachezaji.
WALENGWA: Kiungo wa Celtic Scott Brown, Mchezaji wa Blackpool Charlie Adam na Straika wa Stoke James Beattie.
ZIADA: Danny Shittu yumo kwenye listi hii.
BURNLEY
WANAHITAJI: Sentafowadi na labda Mshambuliaji.
FEDHA: Meneja Owen Coyle huenda akalazimika kuomba pesa itakazolipwa Klabu hivi karibuni kama mgao wao wa malipo toka Kampuni za TV, zinazokadiriwa kuwa Pauni Milioni 7, ili kunua Wachezaji kwa sababu hana na hawezi kuuza Mchezaji hata mmoja ili kupata pesa.
WALENGWA: Beki wa Celtic Gary Caldwell au Beki wa Sheffield United Matt Kilgallon.
ZIADA: Hamna.
CHELSEA
WANAHITAJI: Washambuliaji kuziba mapengo ya Didier Drogba na Salomon Kalou watakaokuwa Afrika mwezi Januari kucheza kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika. Huenda wakamrudisha Franco Di Santo ambae yuko Blackburn kwa mkopo.
FEDHA: Meneja Carlo Ancelotti ametamka hanunui mtu mwezi Januari lakini hakuna anaemwamini na kwa Chelsea fedha si tatizo.
WALENGWA: Sergio Aguero, kwa Pauni Milioni30, anategemewa kuhama kutoka Atletico Madrid kwenda Stamford Bridge.
ZIADA: Chelsea hawathubutu kuuza Mchezaji yeyote kwa vile wanakabiliwa na adhabu ya FIFA ya kutosajili Mchezaji yeyote hadi 2011 baada ya kumsajili Mchezaji Gael Kakuta kinyume cha sheria. Adhabu hii imesitishwa na CAS [Mahakama ya Usuluhishi katika Michezo] hadi itakapotoa uamuzi.
EVERTON
WANAHITAJI: Lundo la Wachezaji majeruhi kupona na Louis Saha kusaini Mkataba mpya kabla hajakuwa Mchezaji huru mwishoni mwa msimu.
FEDHA: Kitita walichopata baada ya kumuuza Joleon Lescott Manchester City kimeshatumiwa na Meneja David Moyes hana hata senti moja ya kununua mtu Januari.
WALENGWA: Mchezaji anaecheza Timu moja na David Beckham huko LA Galaxy, Landon Donovan, atatua Januari kucheza kwa mkopo.
ZIADA: Wakati karibu Timu nzima ni majeruhi, hakuna atakaeondoka Goodison Park.
FULHAM
WANAHITAJI: Meneja Roy Hodgson amesuka Timu nzuri yenye Kikosi kidogo lakini kwa vile pia wanacheza Ulaya kwenye EUROPA LIGI, watakabiliwa na mechi nyingi zaidi na wanahitaji kuimarisha Kikosi chao.
FEDHA: Ni lazima wauze kabla ya kununua.
WALENGWA: Wanataka kumfanya Jonathan Greening, waliemchukua kwa mkopo toka West Brom, awe Mchezaji wao wa kudumu.
ZIADA: Seol Ki-Hyeon, Eddie Johnson na Diomansy Kamara hawana namba za kudumu.
HULL CITY
WANAHITAJI: Mchezaji yeyote mfungaji magoli na Kiungo wa kucheza badala ya Jimmy Bullard anaeumia mara kwa mara.
FEDHA: Meneja Phil Brown ameamrishwa na Mwenyekiti Adam Pearson apunguze Kikosi chake chenye Wachezaji 41.
WALENGWA: Hana.
ZIADA: Ni upunguzwaji wa Wachezaji hao 41.
LIVERPOOL
WANAHITAJI: Straika kumpunguzia mzigo Fernando Torres.
FEDHA: Meneja Rafa Benitez amepoteza pesa nyingi kwa kusaini Wachezaji wasio na manufaa. Ni lazima auze ndio anunue.
WALENGWA: Kiungo wa West Ham Scott Parker na Straika wa Bayern Munich Luca Toni ndio wanaowindwa.
MANCHESTER CITY
WANAHITAJI: Meneja aliefukuzwa, Mark Hughes, alitumia zaidi ya Pauni Milioni 50 kuwanunua Walinzi Kolo Toure, Joleon Lescott na Wayne Bridge na wote hawajang’ara. Sasa Meneja mpya Roberto Mancini inabidi aanze upya.
FEDHA: Klabu inamilikiwa na Koo ya Kifalme ya Abu Dhabi ambao ni Matajiri wakubwa! Bila shaka, vijisenti si tatizo!!
WALENGWA: Senta Hafu wa Juventus Giorgio Chiellini na Fulbeki wa Inter Milan Maicon ndio walengwa wakubwa. Lakini, nani anajua kama Man City hawatamzonga tena Nahodha wa Chelsea, John Terry?
ZIADA: ni ngumu kujua Meneja mpya Roberto Mancini hamtaki nani kwa vile yupo Klabuni kwa muda mfupi sana [wiki tu].
MANCHESTER UNITED
WANAHITAJI: Madifenda hasa baada ya wimbi la kuumia Madifenda wote na kutokujulikana lini Rio Ferdinand atapona na kurudi uwanjani.
FEDHA: Zipo hasa baada ya kutumia Pauni Milioni 20 tu kati ya Pauni Milioni 80 walizopata kwa kumuuza Cristiano Ronaldo.
WALENGWA: Kiraka wa Ajax Gregory van der Wiel, Beki wa West Ham Matthew Upson na Kiungo wa Everton Jack Rodwell.
ZIADA: Haitegemewi kuondoka mtu.
PORTSMOUTH
WANAHITAJI: Kuondolewa kwa kufungiwa kwao kutosajili Mchezaji hadi watakapolipa madeni yanayowakabili kwa kutokumalizia kulipa ada za uhamisho za Wachezaji waliowanunua.
FEDHA: Hawana. Klabu inatakiwa ilipe Pauni Milioni 8 kama deni la ada za uhamisho wa Wachezaji. Njia yao ya kupata Wachezaji ni kwa njia ya mkopo tu.
WALENGWA: Kuongeza mkataba wa mkopo wa Jamie O’Hara kutoka Tottenham.
ZIADA: Inabidi wauze ili walipe madeni na Wachezaji wanaoweza kutolewa kafara ni Nadir Belhadj, John Utaka na pengine Kipa David James.
STOKE CITY
WANAHITAJI: Mshambuliaji wa bei poa.
FEDHA: Meneja Tony Pulis alizilipua pesa zake zote za kununulia Wachezaji kabla Msimu huu haujanza alipotumia Pauni Milioni 20 kuwanunua Tuncay, Robert Huth, Dean Whitehead na Danny Collins.
WALENGWA: Mshambuliaji wa Leeds Jermaine Beckford
ZIADA: Baada ya kugombana na Meneja Tony Pulis, Mshambuliaji James Beattie atauzwa na pia Mshambuliaji mwingine, Dave Kitson, kiwango kimeporomoka hivyo yumo mbioni kuuzwa.
SUNDERLAND
WANAHITAJI: Bosi wa Sunderland Steve Bruce anakerwa sana na udhaifu wa Difensi yake.
FEDHA: Zipo.
WALENGWA: Beki wa pembeni Maynor Figueroa toka Wigan, Sentahafu wa Middlesbrough David Whetaer.
ZIADA: Anton Ferdinand na David Healy hawampendizi Steve Bruce hivyo huenda wakauzwa.
TOTTENHAM
WANAHITAJI: Meneja Harry Redknapp anaridhika na Kikosi chake lakini yeye daima huwa macho wazi kukiimarisha.
FEDHA: Bodi ya Klabu imesisitiza lazima wauzwe Wachezaji ndio wanunuliwe wengine.
WALENGWA: Wachezaji wa West Ham Scott Parker na Matthew Upson wanatajwa sana.
ZIADA: David Bentley na Roman Pavlyuchenko watauzwa. Uvumi umezagaa Robbie Keane nae yuko
njiani kuuzwa.
WEST HAM
WANAHITAJI: Wafungaji kubeba mzigo wa Dean Ashton [amestaafu baada ya kuumia] na Carlton Cole.
FEDHA: Inabidi wauze ndio wanunue.
WALENGWA: Robbie Keane kutoka Tottenham ambae watabadilishana na Mchezaji wao.
ZIADA: Ili kutatua uhaba wa fedha Klabuni, itabidi Scott Parker na Matthew Upson wauzwe.
WIGAN
WANAHITAJI: Walinzi na pengine Viungo wapiganaji.
FEDHA: Zipo baada ya kuuza Wachezaji kadhaa msimu huu.
WALENGWA: Wachezaji wa Portsmouth Younes Kaboul na Kevin-Prince Boateng. Pia mazungumzo yanaendelea ili kumchukua kutoka Chile Mlinzi Waldo Ponce.
ZIADA: Maynor Figueroa yuko njiani kwenda Sunderland na Paul Scharner amedokeza anahama.
WOLVES
WANAHITAJI: Meneja Mick McCarthy anaridhishwa na Kikosi chake.
FEDHA: Hawana.
WALENGWA: Labda wambebe Dave Kitson kwa mkopo kutoka Stoke.
Ziada: Hamna.
Kitendawili cha Rio kurudi uwanjani!!!
Rio Ferdinand anasumbuliwa na tatizo la mgongo ambalo husababisha hata kuumwa kwa misuli ya miguu yake na ugonjwa huu umemweka nje ya uwanja tangu mwishoni mwa Oktoba na kusababisha kuzikosa mechi za Klabu yake Manchester United 13 na mpaka sasa Klabu yake haijui lini atarudi uwanjani.
Sir Alex Ferguson, Meneja wa Man U, amesema Rio ataonekana muda si mrefu ingawa hakusema lini ila aligusia tu kuwa wiki mbili zilizopita alipigwa sindano na baada ya wiki moja akaanza mazoezi kweye jim na bado wanamwangalia maendeleo yake.
Siku chache zilizopita, mwenyewe Rio alitamka, wakati wa ufunguzi wa Mfuko wake wa Hisani, kuwa nafasi yake kwenye Kikosi cha England kitakachoenda Fainali za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini mwezi Juni haiko mashakani.
Lakini, wakati Ligi Kuu leo inatimiza kufikia hatua ya Nusu yake kwa Timu kucheza mechi 19 kati ya 38 wanazotakiwa kucheza, Wadau wanajiuliza kuhusu Rio na Ferguson akazungumza: “Rio yuko imara. Hajaonyesha athari zozote kisaikolojia kuhusu kuumia kwake. Lakini nina hakika yeye kama Mchezaji ana usongo mkubwa wa kutaka kucheza mechi hasa wakati huu kwenye mvutano mkubwa kuelekea Ubingwa!”

Friday 25 December 2009

Wachezaji kutimkia Afrika: Chelsea bila Drogba na wenzake, Portsmouth kuathirika sana!!
Huku Klabu zikiminyana kutafuta Ubingwa na nyingine zikipigania uhai wao wa kubaki Ligi Kuu England, Wachezaji karibu 27 wanaondoka muda wowote kuanzia sasa kujiunga na Timu zao za Taifa zinazojitayarisha kwa ajili ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazochezwa Nchini Angola kuanzia Januari 10 hadi 31.
Klabu zitakazopata pigo la kuondokewa Wachezaji ambalo linatofautiana kwa idadi ya Wachezaji ni pamoja na Chelsea, Arsenal, Manchester City na Portsmouth.
Klabu ambazo haziathiriki hata kidogo na wimbi la kuondokewa Wachezaji ni Manchester United, Liverpool na West Ham.
Wachezaji walio njiani kuelekea Angola:
Arsenal: Emmanuel Eboué (Ivory Coast), Alex Song (Cameroon)
Aston Villa: Moustapha Salifou (Togo)
Bolton Wanderers: Danny Shittu (Nigeria)
Burnley: André Bikey (Cameroon)
Chelsea: Didier Drogba (Ivory Coast), Michael Essien (Ghana), Salomon Kalou (Ivory Coast), John Obi Mikel (Nigeria)
Everton: Aiyegbeni Yakubu, Joseph Yobo (both Nigeria)
Fulham: John Pantsil (Ghana), Dickson Etuhu (Nigeria)
Hull: Daniel Cousin (Gabon), Seyi Olofinjana (Nigeria)
Manchester City: Kolo Touré (Ivory Coast), Emmanuel Adebayor (Togo)
Portsmouth: Nadir Belhadj, Hassan Yebda (both Algeria), John Utaka, Nwankwo Kanu (both Nigeria), Aruna Dindane (Ivory Coast)
Stoke City: Mamady Sidibe (Mali)
Sunderland: John Mensah (Ghana)
Tottenham Hotspur: Benoît Assou-Ekotto (roon)
Wigan Athletic: Richard Kingson (Ghana
LIGI KUU England: Tathmini Mechi za Boksingi Dei na za Jumapili
Timu za Ligi Kuu England, baada ya kusheherekea Xmas, hawana nafasi ya kufungua zawadi zao Siku ya Boksingi Dei kwani Klabu 16 zitakuwa kazini siku hiyo na siku inayofuatia Klabu 4 zilizobaki nazo pia zinaingia mtamboni.
RATIBA:
Jumamosi, 26 Desemba 2009
[saa 9 dak 45 mchana]
Birmingham v Chelsea
[saa 10 jioni]
Fulham v Tottenham
West Ham v Portsmouth
[saa 11 jioni]
Burnley v Bolton
[saa 12 jioni]
Man City v Stoke
Sunderland v Everton
Wigan v Blackburn
[saa 2 na nusu usiku]
Liverpool v Wolves
Jumapili, 27 Desemba 2009
[saa 10 na nusu jioni]
Arsenal v Aston Villa
[saa 1 usiku]
Hull v Man U
Baada ya malamiko na kukerwa kwa kutimuliwa kwa Mark Hughes huko Manchester City, Meneja mpya wa Klabu hiyo Mtaliana Roberto Mancini ataanza kibarua chake kwa kuikaribisha Stoke City Uwanja wa City of Manchester hapo kesho.
Mechi nyingine ya kesho ambayo italeta ushindani wa nguvu ni ile itakayozikutanisha Timu za mkiani West Ham ambayo itaikaribisha Portsmouth Uwanjani Upton Park. Katika mechi zao za mwisho Timu hizi zilizo mashakani zilijitutumua na kupata mafanikio mazuri pale Portsmouth walipoitandika Liverpool 2-0 na West Ham kwenda sare na vinara wa Ligi Chelsea kwa bao 1-1.
Birmingham City, walio nafasi ya 7 kwenye Ligi baada ya kutofungwa katika mechi 9 za mwisho, wanawakaribisha Chelsea ambao siku hizi za hivi karibuni wameonyesha kupwaya mno baada ya kushinda mechi moja tu katika 6 walizocheza mwisho. Chelsea huenda wakalazimika kumchezesha Chipukizi Daniel Sturridge baada ya Anelka kuumia na pia kumpa uzoefu kwani hii ni mechi ya mwisho kwa Didier Drogba kucheza kabla hajaenda kwao kujiunga na Timu ya Taifa ya Ivory Coast inayojitayarisha kucheza Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
Liverpool ambao wako kwenye wakati mgumu kufuatia matokeo mabaya wanawakaribisha Wolves Uwanjani Anfield huku Benitez akisakamwa na kutetewa na Wachezaji wake asifukuzwe. Benitez mwenyewe ameshatangaza ni lazima washinde mechi hii.
Kimbembe kipo kwenye Dabi ya Timu za London huko Craven Cottage wakati Fulham watakapowakaribisha Tottenham, Timu iliyo nafasi ya 5. Kwa sasa Fulham wana matumaini makubwa hasa baada ya kuwaangushia Mabingwa Watetezi Manchester United kipigo cha 3-0 kwenye mechi yao ya mwisho.
Mechi ya Sunderland v Everton ni mechi muhimu mno kwa Klabu hizo kwa vile zote zinasuasua huku Sunderland wakiwa wameshinda mechi 2 tu-dhidi ya Arsenal na Liverpool- katika mechi zao 11 za mwisho na Everton hawajashinda mechi yeyote katika 6 walizocheza mwisho na sasa wako pointi 2 tu juu ya Timu zilizo eneo la kuporomoka Daraja.
Bolton watafanya safari fupi kuelekea East Lancashire Uwanjani Turf Moor kukumbana na Timu ambayo ni ngumu Uwanjani hapo, Burnley, waliofungwa mechi moja tu kati ya 9 za Ligi Kuu Uwanjani hapo. Hata hivyo, bila shaka, Bolton watakuwa wanajiamini hasa baada ya kuifunga West Ham kwenye mechi yao ya mwisho na pia kupata mapumziko ya siku 11 baada ya mechi yao ya Jumatatu iliyokwisha waliyokuwa wacheze na Wigan kuahirishwa kwa sababu ya hali ya hewa ya baridi kali na barafu.
Wigan v Blackburn ni mechi nyingine ngumu inayozikutanisha Timu zenye tofauti ya pointi moja tu kati yao.
Jumapili itaanza kwa mechi kubwa kati ya Arsenal v Aston Villa.
Kimsimamo Arsenal wako nafasi ya 3 na Villa wako nafasi ya 4. Villa hawajawahi kufungwa Uwanja wa Emirates na katika mechi kama hii msimu uliokwisha, Villa waliifunga Arsenal.
Mechi hii itaikutanisha Fowadi ya Arsenal inayofunga Magoli kemkem, Magoli 44 katika mechi 17, na Difensi ngumu ya Aston Villa, iliyofungwa Goli 14 tu katika mechi 18.
Mechi ya pili na ya mwisho siku ya Jumapili ni kati ya Hull City na Manchester United Uwanjani KC. Mabingwa Watetezi, Man U wanaokabiliwa na matatizo ya Difensi kufuatia kujeruhiwa Madifenda wao wote [isipokuwa Evra], wanatoka kwenye kipigo cha 3-0 walichopewa ugenini na Fulham. Hull City nao wana hali mbaya huku wakiwa nafasi ya 17 kwenye msimamo wa Ligi.
Mvuto kwenye mechi hii ni Refa Alan Wiley [pichani] kupangiwa kuichezesha ikiwa ni mechi yake ya kwanza kwa Man U tangu Meneja wa Man U, Sir Alex Ferguson, kumbatukia hayuko fiti kuchezesha, kauli aliyoitoa mara baada ya sare ya 2-2 kati ya Man U na Sunderland mwezi Oktoba.
Kauli hiyo ilimfanya Ferguson afungiwe mechi 2 na FA licha ya kumwomba msamaha Refa Alan Wiley.
Fergie ashutumu kufukuzwa Hughes Man City!!
Sir Alex Ferguson amefoka na kulaumu jinsi Manchester City walivyomfukuza aliekuwa Meneja wao Mark Hughes na kumteua Roberto Mancini kuchukua nafasi yake na kukiita kitendo hicho kuwa ‘hakikubaliki”.
Ingawa Mark Hughes ameiongoza vizuri Manchester City msimu huu ikiwa imefungwa mechi 2 tu kwenye Ligi Kuu, ikiwa ni idadi ndogo kupita Timu yeyote kwenye Ligi Kuu, na pia kuipeleka Timu hiyo kwenye Nusu Fainali ya Kombe la Carling ambako watakutana mwezi Januari na Mahasimu wao Manchester United, hayo yote hayakutosha kumnusuru kwenye kibarua chake.
Mameneja wengi, akiwemo Mchezaji mwenzake wa zamani Steve Bruce ambae alicheza pamoja na Hughes Manchester United chini ya Sir Alex Ferguson, wamejitokeza kumtetea Mark Hughes na kuponda kwa sauti kali jinsi alivyofukuzwa.
Manchester City, ikiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wao Garry Cook, wametetea uamuzi wao wa kumtimua Hughes lakini Ferguson amesema: “Ni vitendo visivyokubalika! Hatujali kama umepoteza mechi 2 au 20, kuna njia ya kuwathamini na kuwatendea binadamu! Nashangaa, Naona Xmas huwafanya Wamiliki wa Klabu kuonyesha tabia zao mbovu! Sijui kwa nini! Asubuhi yote ya Jumamosi, mashine za uvumi zilizagaa kufukuzwa kwa Mark Hughes na bila shaka Mark alisikia hilo! Ni hali mbaya mno kuwa kwenye mazingara hayo huku ukijua mechi ya Jumamosi ni ya mwisho kwako!”
Meneja wa Hull Brown aponda mashitaka ya FA na kusema ni kashfa!!!
Meneja wa Hull City Phil Brown amelaumu Klabu yake kushitakiwa, ikijumuishwa na Arsenal, kwa kushindwa kudhibiti Wachezaji wake kufuatia zogo lililotokea kwenye mechi ya Ligi Kuu wiki iliyopita huko Emirates Stadium ambayo Arsenal walishinda 3-0.
Zogo hilo lilizuka baada ya Samir Nasri wa Arsenal kumkanyaga Richard Garcia wa Hull na ndipo Wachezaji wa pande zote kuzongana na Refa Steve Bennett akawapa Kadi za Njano Nasri na Stephen Hunt wa Hull kwa tukio hilo.
Lakini baadae, wakati Timu zikienda Vyumba vya Kubadilisha jezi, Wachezaji wakavaana tena na kuleta kitimtim.
FA imezipa hadi Januari 13 Klabu hizo kuwasilisha utetezi wao wa mashitaka yao.
Phil Brown amedai Klabu yake isingehusishwa kwenye mashitaka hayo na ni Nasri ndie chanzo cha fujo hizo ambazo alizianzisha alipoona Refa Steve Bennett haoni.
Brown amedai Klabu yake itapinga tuhuma za kuleta fujo.
Keane haondoki Spurs!!!
Harry Redknapp amesema hataki kumuuza Nahodha wake Robbie Keane licha ya kukumbwa na mzozo wa kuongoza Wachezaji wa Tottenham kwenda Dublin, Ireland wiki iliyopita kwenye Pati ya Xmas bila ya ridhaa ya Klabu.
Uvumi ulikuwa umezagaa kuwa Harry Redknapp atamuuza Keane na kumnunua Craig Bellamy kutoka Manchester City lakini Meneja huyo wa Tottenham amekanusha habari hizo.
Uvumi huo uliota mizizi kwa Wadau wengi wakizingatia kuwa katika mechi nyingi za hivi karibuni Redknapp amekuwa akiwachezesha kwa pamoja Jermain Defoe na Peter Crouch na kumtupa benchi Keane lakini Redknapp amesema: “Sitaki kumuuza Keane. Hamna Keane wengi kwenye Soka!”
Hata hivyo Redknapp alidokeza huenda akaingia sokoni dirisha la uhamisho litakapofunguliwa mwezi Januari kwani Wachezaji wake Roman Pavlyuchenko na David Bentley wanang’ang’ania kuhama kwa sababu hawapati namba za kudumu hapo Spurs na hivyo huenda akalazimika kuwauza na pesa zao zikasaidia kununua Wachezaji wengine.
Vilevile, Redknapp alizungumzia kuhusu Mchezaji wao Jamie O’Hara ambae yuko Portsmouth kwa mkopo na kusema kuwa ataongea na Mwenyekiti wake ili waamue kama aendelee kubaki Portsmouth au wamrudishe Tottenham.

Thursday 24 December 2009

Liverpool yadidimia, Nahodha Gerrard kiwango chini!!
Wakati kuna dhana kubwa Meneja wa Liverpool Rafa Benitez atatimuliwa wakati wowote, pia kuna imani kubwa Nahodha wao Steven Gerrard kiwango chake kimeporomoka mno.
Gerrard, miaka29, ndie alikuwa injini ya mafanikio waliyopata Liverpool miaka ya hivi karibuni ikiwemo kutwaa Ubingwa wa Klabu za Ulaya mwaka 2005 huko Instanbul na kuichachafya Manchester United katika kinyang’anyiro cha Ligi Kuu msimu uliopita.
Lakini msimu huu huku Liverpool ikisuasua na kupoteza mechi nyingi Ligi Kuu na pia kubwagwa nje ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE, kiwango cha Gerrard kimeonekana kushuka wazi wazi na kumfanya hata Benitez kumtaka Nahodha wake abadilike na asijipe presha bali acheze mpira wake wa kawaida.
Angalia nini Steven Gerrard alichovuna katika historia yake ya Soka ukulinganisha na Ryan Giggs:
Steven Gerrard [Ameshinda jumla ya Mataji/Tuzo 12:
FA Cup [2], Kombe la Ligi [2], UEFA CHAMPIONS LEAGUE [1], UEFA Cup [1], UEFA Super Cup [2], Tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka, toka kwa Waandishi, [1], Mchezaji Bora wa PFA [Chama cha Wachezaji wa Kulipwa [1], Mchezaji Bora Chipukizi wa PFA [1], Mchezaji Bora wa UEFA [1]
Ryan Giggs [Ameshinda Mtaji/Tuzo 27]:
LIGI KUU [11], FA Cup [4], Kombe la Ligi [3], UEFA CHAMPIONS LEAGUE [2], UEFA Super Cup [1], Klabu Bingwa Duniani [2], Mchezaji Bora wa BBC [1], Mchezaji Bora wa PFA [1], Mchezaji Bora Chipukizi wa PFA [2]]
Wenger: “Giggs ni chaguo langu la Mchezaji Bora katika miaka 10!!”
Hivi karibuni Ryan Giggs alipewa Tuzo ya BBC [Shirika la Utangazaji Uingereza] ya kuwa Mwanamichezo Bora wa Mwaka 2009 na Klabu yake Manchester United ikamwongezea Mkataba ambao utamweka Old Trafford hadi 2011.
Akiwa na umri wa miaka 36, Giggs ndie Mchezaji pekee wa LIGI KUU England aliepata mafanikio makubwa. Giggs ameshashinda Mataji 11 ya Ubingwa wa Ligi Kuu, ametwaa Vikombe vitatu vya Kombe la FA, Vikombe vitatu vya Kombe la Ligi, ameshinda Klabu Bingwa Ulaya mara 2, UEFA Super Cup mara moja na Klabu Bingwa ya Dunia mara 2.
Mafanikio yote ameyapata akiwa na Klabu yake Manchester United ambayo alianza kuichezea tangu akiwa na miaka 14.
Mafanikio yake ni listi ndefu inayozidi kuongezeka.
Giggs ni Mchezaji pekee wa Manchester United kucheza Misimu yote 11 ambayo Man U alitwaa Ubingwa wa Ligi Kuu. Ni Mchezaji pekee wa Man U aliefunga magoli katika Misimu 11 ya kucheza katika Mashindano ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Ni Mchezaji pekee kwenye Ligi Kuu kucheza kila Msimu na kufunga katika kila Msimu tangu Ligi Kuu ilipoanza.
Ni Mchezaji wa Pili wa Kiungo katika Ligi Kuu aliefunga zaidi ya Magoli 100 wa kwanza akiwa ni Matt Le Tissier aliekuwa akichezea Southampton.
Arsene Wenger amebaini: “Ryan Giggs ni Mchezaji Bora Ligi Kuu katika kipindi cha Miaka 10 iliyopita! Yeye ana staili na ni Mshindi! Lakini lile goli alilotufunga kwenye Nusu Fainali ya Kombe la FA mwaka 1999 bado linaniumiza roho!!”
LIVERPOOL: Hofu ya kutimuliwa Benitez, Wachezaji waaanza kumtetea!!
Rafa Benitez amekalia kuti kavu hasa baada ya Liverpool kubwagwa nje ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE na pia kufanya vibaya kwenye LIGI KUU England wakiwa wameshinda mechi 3 tu kati ya 12 walizocheza mwisho na hivyo kuwa nafasi ya 8 kwenye msimamo wa ligi.
Ingawa inaaminika kibarua chake kiko salama kwa sababu tu Liverpool hawana uwezo kifedha kumfukuza na kuteua Meneja mpya kwa kuwa wanakabiliwa na lundo la madeni, hali ni mbaya Klabuni kiasi cha kufanya Wachezaji kujitokeza na kuanza kunadi utetezi wake.
Nyota wa Liverpool, Fernando Torres, amesema: “Kumfukuza Meneja si jawabu! Meneja hachezi, ni sisi inabidi tucheze vizuri pamoja!”
Nae Nahodha wa Liverpool, Steven Gerrard, akiunga mkono hoja hiyo, amesema: “Sisi ni timu! Ni sisi wa kulaumiwa kwa hali tuliyonayo!”
Liverpool, inayomilikiwa na Matajiri wa Kimarekani George Gillet na Tom Hicks, inadaiwa Pauni Milioni 240 na endapo watashindwa kufuzu kucheza UEFA CHAMPIONS LEAGUE msimu ujao watakosa mapato ya zaidi ya Pauni Milioni 20.
Hali ya Rafa Benitez imezidishwa ugumu kwa vile hana pesa za kununua Wachezaji ili kuimarisha Kikosi na ili afanye hivyo ni lazima auze baadhi ya Wachezaji ingawa Fernando Torres na Steven Gerrard hawauzwi.
Wachezaji ambao wanadhaniwa watapelekwa sokoni ni Ryan Babel, Andrea Dossena, Andry Voronin na Philipp Degen.
Na endapo watafaulu kuuza Wachezaji, inasemekana Liverpool wanawawinda Luca Toni kutoka Bayern Munich na Ruud van Nistelrooy toka Real Madrid.
Wakati huo huo, Mlinzi wa Liverpool, Glen Johnson, huenda akahojiwa na Polisi baada ya Mwanafunzi mmoja kudai alishambuliwa nje ya Naitiklabu moja Jijini London.
Arsenal na Hull City kitanzini FA!!!
Klabu za Arsenal na Hull City zimeshitakiwa na FA, Chama cha Soka England, kwa kushindwa kuwadhibiti Wachezaji wao kufuatia mechi ya Ligi Kuu iliyochezwa Uwanja wa Emirates wikiendi iliyopita ambayo Arsenal walishinda 3-0.
Shitaka hilo linafuatia mzozo uliotokea baada ya Mchezaji wa Arsenal Samir Nasri kumkanyaga Kiungo wa Hull Richard Garcia na kundi la Wachezaji wa pande zote mbili kuvaana baada ya tukio hilo.
Refa Steve Bennett aliwapa Kadi za Njano Nasri na Stephen Hunt wa Hull kufuatia mzozo huo lakini vurugu ziliendelea wakati Wachezaji walipokuwa wakitoka Uwanjani kuelekea Vyumba vya kubadilishia jezi.
Msimu uliokwisha Timu hizi pia ziligubikwa na mzozo baada ya Hull City kudai Nahodha wa Arsenal, Cesc Fabregas, ambae hakucheza siku hiyo ya tukio kwenye mechi ya Kombe la FA, alimtemea mate Meneja Msaidizi wa Hull lakini uchunguzi wa FA ulishindwa kuthibitisha tukio hilo na hivyo Fabregas hakuchukuliwa hatua yeyote.
Arsena na Hull City zimepewa hadi Januari 13 kujibu mashitaka hayo.

Wednesday 23 December 2009

Anelka kuzikosa mechi za Ligi Kuu Xmas!!
Mshambuliaji wa Chelsea Nicolas Anelka atazikosa mechi za Chelsea za Ligi Kuu za Desemba 26 watakapocheza ugenini na Birmingham na ile ya Desemba 28 watakapoivaa Fulham katika dabi ya Timu za Magharibi ya London kwa sababu ni majeruhi.
Anelka hakucheza mechi ya Jumapili iliyopita ya Ligi Kuu Chelsea walipotoka sare na West Ham kwa vile ameumia mguu na sasa tatizo hilohilo limemfanya aendelee kuwa nje.
Sasa Chelsea wamesema wanategemea Anelka kuanza kucheza kwenye mechi ya Kombe la FA hapo Januari 3 watakapocheza na Watford.
Chelsea pia watamkosa Mshambuliaji wao mkubwa Didier Drogba ambae anatakiwa ajiunge na Timu ya Taifa ya Ivory Coast kabla ya mwisho wa Desemba kwa ajili ya matayarisho ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazochezwa huko Angola kuanzia Januari 10.
Ivory Coast inategemewa kupiga Kambi yake ya mazoezi Nchini Tanzania mwanzoni mwa Januari ambako itakutana na Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, katika mechi mbili za kujipima nguvu.
Diouf apata kibali kuchezea Man U!!!
Mchezaji kutoka Senegal, Mame Biram Diouf, miaka 22, amepewa kibali cha kazi na hivyo kuruhusiwa kuichezea Manchester United kuanzia Januari.
Diouf alisajiliwa na Manchester United kabla msimu huu kuanza kutoka Klabu ya Molde ya Norway lakini ikabidi aendelee kuichezea Molde kwa mkopo kwa sababu ya kukosa kibali cha kazi.
Tangu wakati huo, ameshaichezea Molde mechi 12 na kufunga mabao manne na kufanya idadi yake ya magoli kwa Klabu ya Molde kuwa ni 33 katika mechi 75 alizoichezea.
Bosi wa Man U, Sir Alex Ferguson, amemsifia Diouf ambae ameshaichezea Senegal mara moja, kwa kutamka: “Anafanya mazoezi na sisi na anafurahisha na kuvutia! Klabu yetu ni bora kwa kuvumbua vipaji na kuvikuza! Yeye ana miaka 22 tu na anaonekana ni bora!”
KOMBE LA MATAIFA YA AFRIKA lamtia kinyaa Grant!!!
Meneja wa Portsmouth, Avram Grant, anashangazwa mno na FIFA kuruhusu Kombe la Mataifa ya Afrika kuchezwa Januari na kulazimisha Wachezaji Mastaa wanaocheza Ligi kubwa Ulaya kuziacha Klabu zao zinazowalipa pesa nyingi na kwenda Afrika kwa mwezi mzima.
Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitachezwa huko Angola kuanzia Januari 10 hadi 31 na Klabu kadhaa za Ligi Kuu England zitawakosa Mastaa wao wanaotoka Afrika.
Portsmouth, Klabu iliyomo mashakani kwani ipo mkiani kwenye Ligi Kuu na pia hairuhusiwi kusajili Mchezaji yeyote kwa vile inakabiliwa na madeni yanayotokana na kushindwa kumalizia kulipia ada za uhamisho za Wachezaji kadhaa iliyowanunua, itawakosa Wachezaji wake kina Aruna Dindane toka Ivory Coast, Kanu toka Nigeria, Nadir Belhadj na Hassan Yebda toka Algeria.
Grant ametamka: “Sijui kwa nini FIFA wanaruhusu hili! Sisi tunawalipa Wachezaji hao pesa nyingi, wao wanakaa nao miezi miwili bure! Wachezaji hao wanatakiwa kujiunga na Timu zao za Taifa wiki 2 kabla! “
Grant amesema ataongea na Timu za Taifa za Wachezaji wake ili kuwaombea wachelewe kujiunga ili angalau wawepo kwenye mechi ya Desemba 30 watakapocheza na Arsenal.
Wenger akata tamaa kuhusu Van Persie!!
Bosi wa Arsenal, Arsene Wenger, amekiri kuwa itakuwa ni bahati kubwa kama Staa wake Robin van Persie atapona enka aliyoumia na kurudi uwanjani kabla msimu haujaisha hapo Mei mwakani.
Wenger amesema: “Ikiwa wewe ni mtu wa matumaini, unaweza ukasema atacheza Aprili lakini ukweli ni kuwa ni pengine ni Mei ndio atarudi! Sitaki kujipa matumaini ya uongo! Bora nisubiri tu na ikitokea akirudi mapema hilo litakuwa kama zawadi!”
Van Persie aliumizwa na Difenda wa Italia Giorgio Chiellini Novemba 14 katika mechi ya kirafiki kati ya Uholanzi na Italia na ikabidi afanyiwe upasuaji kwenye enka yake ili kuunga kamba za musuli zilizokatika.
Arsenal imekitaka Chama cha Soka cha Uholanzi kuwalipa fidia kwa kuumizwa Mchezaji huyo lakini inawezekana malipo hayo yasitolewe kwani kuna makubaliano kati ya FIFA na UEFA kulipa fidia tu kwa Wachezaji wanaoumia kwenye Fainali za Kombe la Dunia na Fainali za EURO Cup na si mechi nyingine zozote.
LIGI KUU England yaingia patamu!!! Mechi za Xmas, Boksingi Dei na Nyuu Iya kutoa fununu nani mbivu, nani mbichi!!!!
Wakati Chelsea bado kinara, Mabingwa Watetezi Manchester United wakisuasua na Difensi ya kuunga baada ya wote [isipokuwa Evra] kuumia, Arsenal akijikongoja licha ya Majeruhi ya Mastaa wao na Liverpool akipigwa nje ndani huku Timu 'zisizotegemewa' kama Villa, Spurs na Man City, kwa mnyato, zikileta upinzani usiotarajiwa, Ligi Kuu sasa inaingia kipindi cha Sikukuu za Xmas na Nyuu Iya ambacho kihistoria ndio hutoa fununu nani mwenye nafasi kubwa ya kuwa Bingwa na nani yumo hatarini kushushwa Daraja.
Miongoni mwa mechi kali zinazotarajiwa kuchezwa kipindi hiki ni zile kati ya Arsenal v Aston Villa [Desemba 27] na ile ya Aston Villa v Liverpool [Desemba 29].
MSIMAMO LIGI KUU England: [Timu zimecheza mechi 18 isipokuwa inapotajwa]
1 Chelsea pointi 41
2 Man Utd pointi 37
3 Arsenal pointi 35 [mechi 17]
4 Aston Villa pointi 35
5 Tottenham pointi 33
6 Man City pointi 29 [mechi 17]
7 Birmingham pointi 28
8 Liverpool pointi 27
9 Fulham pointi 26 [mechi 17]
10 Sunderland pointi 21
11 Stoke pointi 21 [mechi 17]
12 Wolves pointi 19
13 Blackburn pointi 19
14 Burnley pointi 19
15 Everton pointi 18 [mechi 17]
16 Wigan pointi 18 [mechi 17]
17 Hull pointi 17
18 Bolton pointi 16 [mechi 16]
19 West Ham pointi 15
20 Portsmouth pointi 14
RATIBA: [saa za bongo]
Jumamosi, 26 Desemba 2009
[saa 9 dak 45 mchana]
Birmingham v Chelsea
[saa 10 jioni]
Fulham v Tottenham
West Ham v Portsmouth
[saa 11 jioni]
Burnley v Bolton
[saa 12 jioni]
Man City v Stoke
Sunderland v Everton
Wigan v Blackburn
[saa 2 na nusu usiku]
Liverpool v Wolves
Jumapili, 27 Desemba 2009
[saa 10 na nusu jioni]
Arsenal v Aston Villa
[saa 1 usiku]
Hull v Man U
Jumatatu, 28 Desemba 2009
[saa 9 dak 45 mchana]
Tottenham v West Ham
[saa 12 jioni]
Blackburn v Sunderland
Chelsea v Fulham
Everton v Burnley
Stoke v Birmingham
[saa 4 dak 45 usiku]
Wolves v Man City
Jumanne, 29 Desemba 2009
[saa 4 dak 45 usiku]
Aston Villa v Liverpool
[saa 5 usiku]
Bolton v Hull
Jumatano, 30 Desemba 2009
[saa 4 dak 45 usiku]
Portsmouth v Arsenal
[saa 5 usiku]
Man U v Wigan
Jumanne, 5 Januari 2010
[saa 4 dak 45 usiku]
Stoke v Fulham
Jumatano, 6 Januari 2010
[saa 4 dak 45 usiku]
Arsenal v Bolton
Jumamosi, 9 Januari 2010
[saa 9 dak 45 mchana]
Hull v Chelsea
[saa 12 jioni]
Arsenal v Everton
Burnley v Stoke
Fulham v Portsmouth
Sunderland v Bolton
Wigan v Aston Villa
[saa 2 na nusu usiku]
Birmingham v Man U

Tuesday 22 December 2009

Meneja Mpya Man City atangaza Ubingwa ndani ya Miezi 18!!!
Baada ya kutambulishwa hapo jana, Mtaliana Roberto Mancini aliechukua nafasi ya Umeneja Manchester City iliyokuwa ya Mark Hughes aliefukuzwa Jumamosi iliyopita, amejigamba kuwa atachukua Ubingwa wa England ndani ya kipindi cha Miezi 18.
Mancini, aliewahi kuwa Meneja wa Inter Milan huko Italia, atasaidiwa na Meneja Msaidizi Brian Kidd aliewahi kuwa Msaidizi wa Sir Alex Ferguson huko Manchester United.
Mara baada ya utambulisho, Mancini akajigamba: “Kwa sasa tunalenga kumaliza Ligi Kuu tukiwa ndani ya Timu Bora Nne. Msimu ujao, tunataka tuchukue Ubingwa!”
Wakati huohuo, Mark Hughes, aliemwaga unga Man Cuty, amelalamika kuwa hakupewa taarifa mapema kuwa ataondolewa lakini mrithi wake alikuwa tayari ameshatayarishwa na hivyo kuthibitisha kulikuwa na mipango ya muda mrefu kumwondoa.
Hughes amelalamika kuwa malengo waliyokubaliana na Wamiliki wa Man City ambao ni Koo ya Kitajiri ya Kifalme toka Abu Dhabi yalikuwa ni kuumaliza msimu huu wa Ligi Kuu England wakiwa katika Timu 6 Bora kitu ambacho kilikuwa kinawezekana kwani Timu imepoteza mechi 2 tu ikiwa ni idadi ndogo kupita Timu zote Ligi Kuu.
Hata hivyo Man City imetoka sare mechi 8 zikiwa ni nyingi mno na wameshinda mechi 7 na wako nafasi ya 6 kwenye Ligi Kuu.
Messi Mchezaji Bora Duniani 2009!!
Ronaldo Mfungaji wa Goli la Mwaka!!!
Marta ni Bora kwa Mabibi!!!
Nyota wa Barcelona na Argentina, Lionel Messi, miaka 22, ametunukiwa Tuzo ya FIFA ya Mchezaji Bora kwa Mwaka 2009.
Messi pia hivi karibuni alishinda Tuzo maarufu ya Ballon d’Or ikiashiria ni Mchezaji Bora Ulaya.
Mshindi wa Mwaka jana, Cristiano Ronaldo, amekuwa Mshindi wa Pili.
Kwa upande wa Wanawake, Marta wa Brazil, ndie Mchezaji Bora 2009 ikiwa ni mara yake ya nne mfululizo kutwaa Tuzo hiyo.
Katika sherehe zilizofanyika Zurich, Uswisi hapo jana, Messi alitamka: “Tafadhali, mie si Mfalme wa Dunia wala si nambari wani duniani! Siamini vitu hivyo!!! Nimebahatika tu kuchezea Timu nzuri Barca!!!”
Cristiano Ronaldo alipewa Tuzo ya FIFA iliyokuwa ikitolewa kwa mara ya kwanza iitwayo Puskas [Hili ni jina la Mchezaji Nyota wa zamani toka Hungary] kwa kufunga Goli Bora la Mwaka. Goli lililompa Tuzo hiyo ni lile alilofunga akiwa na Manchester United mwezi Aprili 2009 kwenye mechi ya Robo Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE alipopiga mkwaju toka Mita 40 na kuwafungA FC Porto.
FIFA pia ilitangaza Majina ya Wachezaji Bora 11 wanaounda Kikosi Bora nao ni: Kipa: Casillas, Mabeki: Dani Alves, Evra, Vidic, Terry, Viungo: Xavi, Iniesta, Gerrard Mastraika: Ronaldo, Messi na Torres.

Monday 21 December 2009

Baridi na Barafu yasababisha mechi ya leo LIGI KUU kuahirishwa!!
Mechi ya Ligi Kuu England iliyokuwa ichezwe leo Jumatatu Desemba 21 kati ya Wigan na Bolton imeahirishwa kufuatia baridi kali na barafu iliyosababisha baadhi ya barabara na Uwanja wa Wigan uitwao DW kuganda kwa barafu.
Ingawa Wamiliki wa Uwanja huo wa DW, Klabu ya Wigan, wamesisitiza Uwanja wao uko salama na unachezeka, Mamlaka za Polisi na Wasimamizi wa Usalama wa Raia wamesema ni hatari kwa mechi hiyo kuchezwa hasa ikizingatiwa baridi hiyo kali, barafu na hali mbaya za barabara na hivyo kuhatarisha maisha ya Washabiki waliopanga kuhudhuria mechi hiyo.
SKANDALI YA TERRY: Nahodha huyo wa Chelsea adaiwa kupokea hongo!!!
Nahodha wa Chelsea, John Terry, amegubikwa na skandali iliyoibuliwa na Gazeti moja huko England lilotoa mkanda wa video na kudai Nahodha huyo alipokea hongo ili kusuka mpango uliofanikiwa wa Waandishi wa Habari wa Gazeti hilo kutembelea kwa siri Kambi ya Mazoezi ya Chelsea iliyopo eneo la Cobham huko London.
Inadaiwa Terry alipokea Pauni Elfu 10.
Hata hivyo Klabu ya Chelsea, ikiongozwa na Meneja Carlo Ancelotti, imekanusha tuhuma hizo na kusisitiza wana imani kubwa na Kepteni wao.
Mchezaji kukosa Fainali Kombe la Dunia kwa kuogopa Wadudu Mabuibui!!!
Straika Supastaa wa Sunderland na Timu ya Taifa England, Darren Bent, miaka 25, ana tatizo kubwa la kuogopa Mabuibui lakini yuko tayari kupatiwa tiba ya kuondoa woga huo ili tu awepo kwenye Kikosi cha England kitakachokuwa Fainali za Kombe la Dunia mwakani huko Afrika Kusini ambako kunasifiwa sana kwa kuwa na Mabuibui wengi na wa kila aina wakiwemo wenye sumu kali.
Mwenyewe Bent amesema hachukii Wanyama au Wadudu kwani alishawahi kufuga Nyoka alipokuwa mdogo lakini amekiri Mabuibui ndio humtisha sana na huwaogopa sana.
LIGI KUU ENGLAND: Jana Chelsea chupuchupu!!!
Chelsea imeendelea kuwa kinara wa Ligi Kuu na sasa wanaongoza kwa pointi 4 mbele ya Manchester United baada ya jana kutoka suluhu 1-1 ugenini huko Upton Park walipokutana na West Ham.
West Ham walitangulia kupata bao kipindi cha kwanza kupitia kwa Diamanti aliefunga kwa penalti kufuatia rafu ya Beki wa Chelsea Ashley Cole lakini Chelsea wakasawazisha kwa penalti tata iliyofungwa na Frank Lampard.
Refa Mike Dean aliamuru mara 3 penalti hiyo ya Lampard irudiwe kufuatia Wachezaji kuingia ndani ya boksi kabla penalti hiyo haijapigwa lakini mara zote hizo 3 Lampard alifanikiwa kufunga.
MATOKEO MECHI NYINGINE ZA JANA:
Everton 1 Birmingham 1
Wolves 2 Burnley 0

Sunday 20 December 2009

BAADA YA VIPIGO: Fergie abaki akiombea Madifenda wake wapone, Benitez abaki kulaumu Refa!!!
Kufuatia vipigo kwenye mechi za LIGI KUU England ambako Klabu kongwe Manchester United ilinyukwa na Fulham 3-0 na Liverpool kubamizwa 2-0 na goigoi Portsmouth hapo jana, Mameneja wa Timu hizo wamesimama na kutoa maoni yao tofauti na yenye hisia tofauti.
Sir Alex Ferguson wa Manchester United, ambayo Difensi yake yote, isipokuwa Ptrice Evra, ni majeruhi na hivyo kulazimika kuwachezesha Viungo Darren Fletcher na Michael Carrick kama Masentahafu, amesema Viungo hawawezi kusimama kwenye ulinzi na anaomba kipigo hicho cha Fulham kisije kikawaathiri kutetea Ubingwa wao.
Pia amesisitiza Timu ya Madaktari wa Manchester United inafanya kila hila ili kuwaponya haraka kina Gary Neville, Edwin van der Sar, Wes Brown, Rio Ferdinand, Jonny Evans, Nemanja Vidic, Rafael na Ryan Giggs kabla jahazi halijaenda mrama.
Nae Rafa Benitez, Meneja wa Liverpool, amebaki kumlaumu Refa aliechezesha mechi waliyopigwa 2-0 na Portsmouth kwa kumpa Kadi Nyekundu Kiungo wake Mascherano huku akisahau Kiungo huyo alikula Kadi hiyo huku Liverpool tayari wako nyuma kwa bao 1-0.
Pia alimlaumu Refa huyo kutokumlinda Staa wake Fernando Torres ambae alidai alikuwa akichezewa vibaya kila mara.
Powered By Blogger