Saturday 26 December 2009

LIGI KUU England: Yafikia Nusu, Uhamisho kufunguliwa Januari, je nini kitegemewe?
Ligi Kuu England wikiendi hii inafikia hatua muhimu ya Timu kufikia kucheza mechi 19 ambazo ni nusu ya mechi zote na vita kileleni iko wazi huku kuna Timu 8 zikigombea Ubingwa na nafasi 4 za kucheza UEFA CHAMPIONS LEAGUE msimu ujao na huko mkiani, ukitoa Timu hizo 8 zilizo fungu la kugombea Ubingwa, Timu zote zilizobaki, kimahesabu, zipo kwenye vita ya kukwepa kushuka Daraja.
Mwezi Januari dirisha la uhamisho litafunguliwa na kufungwa Januari 31 na kila Timu, pengine, itakuwa ikifikiria kuingia sokoni na kuimarisha Vikosi vyao. Lakini, kikawaida, biashara ya Wachezaji mwezi Januari ni ngumu na vile vile Klabu nyingi kwa sasa zinakabiliwa na matatizo ya kifedha.
Ifuatayo ni tathmini ya kila Klabu ie, nini kinahitajika, uwezo kifedha na Wachezaji gani walengwa:
ARSENAL
WANAHITAJI: Sentafowadi mwenye nguvu hasa baada ya kuumia kwa Robin van Persie na Nicklas Bendtner ambao wako nje kwa muda mrefu.
FEDHA: Arsenal wanasisitiza pesa wanazo ila tatizo ni kumlazimisha Arsene Wenger jinsi ya kuzitumia.
WALENGWA: Straika wa Wolfsburg Edin Dzeko ambae thamani yake ni Pauni Milioni 20 na mwingine ni Mchezaji wa Bordeaux Marouane Chamakh ambae Wenger amesita kumsaka kwa ajili ya bei yake.
ZIADA: Beki kutokaUswisi Philippe Senderos huenda akahamia Atletico Madrid.
ASTON VILLA
WANAHITAJI: Meneja Martin O'Neill anafurahishwa na mwenendo wa Klabu yake lakini anataka kusajili Straika mmoja.
FEDHA: Villa haijafuja pesa kama Klabu nyingine, hivyo, bila shaka, mfuko wao wa ununuzi wa Wachezaji bado umetuna.
WALENGWA:Kuna tetesi kuwa endapo Spurs wataamua kumuuza Nahodha wao Robbie Keane, Villa watamdaka.
ZIADA: Nicky Shorey na Nigel Reo-Coker ndio wanaohusishwa na uhamisho.
BIRMINGHAM
WANAHITAJI: Wachezaji zaidi wa viwango vya juu huku Straika akiwa juu ya listi yao.
FEDHA: Mmiliki wao Carson Yeung ameahidi kutoa Pauni Milioni 40 ili kununua Wachezaji.
WALENGWA: Listi yao ya ununuzi wamo Mchezaji wa Sporting Gijon Michel na Mchezaji wa Rangers Kris Boyd.
ZIADA: Huenda Kevin Phillips, Franck Queudrue na Teemu Tainio wakauzwa.
BLACKBURN
WANAHITAJI: Mfungaji magoli kwani wana uhaba mkubwa wa magoli. Vilevile, wameonyesha nia ya kuongeza Mkataba kwa Franco Di Santo ambae wamemkopa kutoka Chelsea.
FEDHA: Meneja Sam Allardyce aliufilisi mfuko wa kununua Wachezaji kabala Msimu kuanza hivyo atalazimika kuuza Wachezaji kabla ya kununua.
WALENGWA: Straika wa Stoke James Beattie na Beki kutoka Portsmouth Nadir Belhadj.
ZIADA: Winga Morten Gamst Pedersen na Mshambuliaji Benni McCarthy huenda wakauzwa.
BOLTON
WANAHITAJI: Kiungo mlinzi na Mshambuliaji.
FEDHA: Meneja Gary Megson ndie alietumia fedha kidogo kupita yeyote kwenye Ligi Kuu katika ununuzi wa Wachezaji.
WALENGWA: Kiungo wa Celtic Scott Brown, Mchezaji wa Blackpool Charlie Adam na Straika wa Stoke James Beattie.
ZIADA: Danny Shittu yumo kwenye listi hii.
BURNLEY
WANAHITAJI: Sentafowadi na labda Mshambuliaji.
FEDHA: Meneja Owen Coyle huenda akalazimika kuomba pesa itakazolipwa Klabu hivi karibuni kama mgao wao wa malipo toka Kampuni za TV, zinazokadiriwa kuwa Pauni Milioni 7, ili kunua Wachezaji kwa sababu hana na hawezi kuuza Mchezaji hata mmoja ili kupata pesa.
WALENGWA: Beki wa Celtic Gary Caldwell au Beki wa Sheffield United Matt Kilgallon.
ZIADA: Hamna.
CHELSEA
WANAHITAJI: Washambuliaji kuziba mapengo ya Didier Drogba na Salomon Kalou watakaokuwa Afrika mwezi Januari kucheza kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika. Huenda wakamrudisha Franco Di Santo ambae yuko Blackburn kwa mkopo.
FEDHA: Meneja Carlo Ancelotti ametamka hanunui mtu mwezi Januari lakini hakuna anaemwamini na kwa Chelsea fedha si tatizo.
WALENGWA: Sergio Aguero, kwa Pauni Milioni30, anategemewa kuhama kutoka Atletico Madrid kwenda Stamford Bridge.
ZIADA: Chelsea hawathubutu kuuza Mchezaji yeyote kwa vile wanakabiliwa na adhabu ya FIFA ya kutosajili Mchezaji yeyote hadi 2011 baada ya kumsajili Mchezaji Gael Kakuta kinyume cha sheria. Adhabu hii imesitishwa na CAS [Mahakama ya Usuluhishi katika Michezo] hadi itakapotoa uamuzi.
EVERTON
WANAHITAJI: Lundo la Wachezaji majeruhi kupona na Louis Saha kusaini Mkataba mpya kabla hajakuwa Mchezaji huru mwishoni mwa msimu.
FEDHA: Kitita walichopata baada ya kumuuza Joleon Lescott Manchester City kimeshatumiwa na Meneja David Moyes hana hata senti moja ya kununua mtu Januari.
WALENGWA: Mchezaji anaecheza Timu moja na David Beckham huko LA Galaxy, Landon Donovan, atatua Januari kucheza kwa mkopo.
ZIADA: Wakati karibu Timu nzima ni majeruhi, hakuna atakaeondoka Goodison Park.
FULHAM
WANAHITAJI: Meneja Roy Hodgson amesuka Timu nzuri yenye Kikosi kidogo lakini kwa vile pia wanacheza Ulaya kwenye EUROPA LIGI, watakabiliwa na mechi nyingi zaidi na wanahitaji kuimarisha Kikosi chao.
FEDHA: Ni lazima wauze kabla ya kununua.
WALENGWA: Wanataka kumfanya Jonathan Greening, waliemchukua kwa mkopo toka West Brom, awe Mchezaji wao wa kudumu.
ZIADA: Seol Ki-Hyeon, Eddie Johnson na Diomansy Kamara hawana namba za kudumu.
HULL CITY
WANAHITAJI: Mchezaji yeyote mfungaji magoli na Kiungo wa kucheza badala ya Jimmy Bullard anaeumia mara kwa mara.
FEDHA: Meneja Phil Brown ameamrishwa na Mwenyekiti Adam Pearson apunguze Kikosi chake chenye Wachezaji 41.
WALENGWA: Hana.
ZIADA: Ni upunguzwaji wa Wachezaji hao 41.
LIVERPOOL
WANAHITAJI: Straika kumpunguzia mzigo Fernando Torres.
FEDHA: Meneja Rafa Benitez amepoteza pesa nyingi kwa kusaini Wachezaji wasio na manufaa. Ni lazima auze ndio anunue.
WALENGWA: Kiungo wa West Ham Scott Parker na Straika wa Bayern Munich Luca Toni ndio wanaowindwa.
MANCHESTER CITY
WANAHITAJI: Meneja aliefukuzwa, Mark Hughes, alitumia zaidi ya Pauni Milioni 50 kuwanunua Walinzi Kolo Toure, Joleon Lescott na Wayne Bridge na wote hawajang’ara. Sasa Meneja mpya Roberto Mancini inabidi aanze upya.
FEDHA: Klabu inamilikiwa na Koo ya Kifalme ya Abu Dhabi ambao ni Matajiri wakubwa! Bila shaka, vijisenti si tatizo!!
WALENGWA: Senta Hafu wa Juventus Giorgio Chiellini na Fulbeki wa Inter Milan Maicon ndio walengwa wakubwa. Lakini, nani anajua kama Man City hawatamzonga tena Nahodha wa Chelsea, John Terry?
ZIADA: ni ngumu kujua Meneja mpya Roberto Mancini hamtaki nani kwa vile yupo Klabuni kwa muda mfupi sana [wiki tu].
MANCHESTER UNITED
WANAHITAJI: Madifenda hasa baada ya wimbi la kuumia Madifenda wote na kutokujulikana lini Rio Ferdinand atapona na kurudi uwanjani.
FEDHA: Zipo hasa baada ya kutumia Pauni Milioni 20 tu kati ya Pauni Milioni 80 walizopata kwa kumuuza Cristiano Ronaldo.
WALENGWA: Kiraka wa Ajax Gregory van der Wiel, Beki wa West Ham Matthew Upson na Kiungo wa Everton Jack Rodwell.
ZIADA: Haitegemewi kuondoka mtu.
PORTSMOUTH
WANAHITAJI: Kuondolewa kwa kufungiwa kwao kutosajili Mchezaji hadi watakapolipa madeni yanayowakabili kwa kutokumalizia kulipa ada za uhamisho za Wachezaji waliowanunua.
FEDHA: Hawana. Klabu inatakiwa ilipe Pauni Milioni 8 kama deni la ada za uhamisho wa Wachezaji. Njia yao ya kupata Wachezaji ni kwa njia ya mkopo tu.
WALENGWA: Kuongeza mkataba wa mkopo wa Jamie O’Hara kutoka Tottenham.
ZIADA: Inabidi wauze ili walipe madeni na Wachezaji wanaoweza kutolewa kafara ni Nadir Belhadj, John Utaka na pengine Kipa David James.
STOKE CITY
WANAHITAJI: Mshambuliaji wa bei poa.
FEDHA: Meneja Tony Pulis alizilipua pesa zake zote za kununulia Wachezaji kabla Msimu huu haujanza alipotumia Pauni Milioni 20 kuwanunua Tuncay, Robert Huth, Dean Whitehead na Danny Collins.
WALENGWA: Mshambuliaji wa Leeds Jermaine Beckford
ZIADA: Baada ya kugombana na Meneja Tony Pulis, Mshambuliaji James Beattie atauzwa na pia Mshambuliaji mwingine, Dave Kitson, kiwango kimeporomoka hivyo yumo mbioni kuuzwa.
SUNDERLAND
WANAHITAJI: Bosi wa Sunderland Steve Bruce anakerwa sana na udhaifu wa Difensi yake.
FEDHA: Zipo.
WALENGWA: Beki wa pembeni Maynor Figueroa toka Wigan, Sentahafu wa Middlesbrough David Whetaer.
ZIADA: Anton Ferdinand na David Healy hawampendizi Steve Bruce hivyo huenda wakauzwa.
TOTTENHAM
WANAHITAJI: Meneja Harry Redknapp anaridhika na Kikosi chake lakini yeye daima huwa macho wazi kukiimarisha.
FEDHA: Bodi ya Klabu imesisitiza lazima wauzwe Wachezaji ndio wanunuliwe wengine.
WALENGWA: Wachezaji wa West Ham Scott Parker na Matthew Upson wanatajwa sana.
ZIADA: David Bentley na Roman Pavlyuchenko watauzwa. Uvumi umezagaa Robbie Keane nae yuko
njiani kuuzwa.
WEST HAM
WANAHITAJI: Wafungaji kubeba mzigo wa Dean Ashton [amestaafu baada ya kuumia] na Carlton Cole.
FEDHA: Inabidi wauze ndio wanunue.
WALENGWA: Robbie Keane kutoka Tottenham ambae watabadilishana na Mchezaji wao.
ZIADA: Ili kutatua uhaba wa fedha Klabuni, itabidi Scott Parker na Matthew Upson wauzwe.
WIGAN
WANAHITAJI: Walinzi na pengine Viungo wapiganaji.
FEDHA: Zipo baada ya kuuza Wachezaji kadhaa msimu huu.
WALENGWA: Wachezaji wa Portsmouth Younes Kaboul na Kevin-Prince Boateng. Pia mazungumzo yanaendelea ili kumchukua kutoka Chile Mlinzi Waldo Ponce.
ZIADA: Maynor Figueroa yuko njiani kwenda Sunderland na Paul Scharner amedokeza anahama.
WOLVES
WANAHITAJI: Meneja Mick McCarthy anaridhishwa na Kikosi chake.
FEDHA: Hawana.
WALENGWA: Labda wambebe Dave Kitson kwa mkopo kutoka Stoke.
Ziada: Hamna.

No comments:

Powered By Blogger