Saturday 9 May 2009

Liverpool watwaa uongozi LIGI KUU: West Ham 0 Liverpool 3

Liverpool wakicheza nyumbani kwa West Ham Uwanja wa Upton Park wameweza kuwafunga wenyeji wao West Ham kwa mabao 3-0 kwa magoli mawili ya Nahodha wao Steven Gerrard na la tatu alilofunga Ryan Babel.
Bao la kwanza alifunga Gerrard, akicheza mechi yake ya kwanza baada ya kukosa mechi kadhaa kwa kuwa majeruhi, baada ya pande zuri la Fernando Torres kwenye dakika ya pili tu. Goli la pili lilifungwa baada ya Gerrard kupiga penalti ambayo Kipa wa West Ham Robert Green aliokoa lakini Gerrard akautokea tena mpira na kuukwamisha wavuni.
Hadi mapumziko West Ham 0 Liverpool 2.
Kipindi cha pili, Ryan Babel, alieingizwa kipindi hicho alifunga bao la 3.
Sasa Liverpool anaongoza LIGI KUU England akiwa na pointi 80 sawa na Manchester United lakini ana tofauti ya magoli bora ingawa amecheza mechi 2 zaidi ya Manchester United. Liverpool amecheza mechi 36 na Man U mechi 34.
Kesho Manchester United atacheza na Mtani wake wa Jadi Manchester City nyumbani kwake Old Trafford.
Jumatano Man U anacheza mechi yake ya kiporo ugenini kwa Wigan na Jumamosi ijayo tarehe 16 Mei Man U anamkaribisha Arsenal Old Trafford.
Liverpool mechi yake inayofuata ni Jumapili tarehe 17 Mei wakati atakapokuwa mgeni wa West Bromwich Timu inayopigana isishushwe Daraja.
Lakini Manchester United akishinda mechi yake ya kesho na Man City, na ile ya Jumatano na Wigan, na, pengine, kushinda au kutoka suluhu mechi ya Jumamosi ijayo na Arsenal, basi atakuwa Bingwa moja kwa moja hata kabla Liverpool hajacheza mechi yake inayokuja dhidi ya West Bromwich.
Vikosi ni:
West Ham: Green, Neill, Tomkins, Upson, Ilunga, Boa Morte, Noble, Kovac, Stanislas, Di Michele, Tristan.
Akiba: Lastuvka, Lopez, Nsereko, Spector, Collison, Sears, Payne.
Liverpool: Reina, Arbeloa, Skrtel, Carragher, Aurelio, Benayoun, Mascherano, Lucas, Gerrard, Kuyt, Torres.
Akiba: Cavalieri, Dossena, Hyypia, Babel, Insua, Ngog, Degen.
Refa: Alan Wiley
LIGI ITALIA SERIE A: KIBANO KWA CLAUDIO RANIERI WA JUVENTUS!!!!
Claudio Ranieri, Meneja wa zamani wa Chelsea ambae sasa yuko Juventus huko kwao Italy, kesho ana kitimtim kikubwa kwani kesho Timu yake Juventus inacheza na AC Milan na wakiwafunga tu AC Milan basi Bingwa Italia ni Inter Milan, inayoongozwa na pia Meneja wa zamani wa Chelsea Jose Mourinho, huku kukiwa na mechi 3 za LIGI YA SERIE A zimebaki.
Ikiwa Ubingwa watachukuwa Inter Milan kwa sababu tu Juventus kawafunga AC Milan Mashabiki wa Juventus watakasirika sana kwa sababu hawaipendi Inter Milan ambao wakichukua tena Ubingwa itakuwa ni mara ya 4 mfululizo.
Lakini kitimtim cha Claudio Ranieri si hicho tu!
Juventus wakifungwa na AC Milan vilevile Mashabiki watakasirika kwani AC Milan pia ni adui mkubwa wa Juventus.
Kwa kifupi, Claudio Ranieri, inategemewa hana kazi msimu ujao.
Juventus walikuwa bado kwenye kinyang'anyiro cha Ubingwa lakini wamepoteza mwelekeo kwa kutokushinda mechi 5 mfululizo hadi sasa.
Mpaka sasa Juventus wako nafasi ya 3 wakiwa na pointi 65 kwa mechi 33, AC Milan pointi 67 mechi 33 na vinara Inter Milan wana pointi 77 kwa mechi 34.
MECHI ZA KESHO JUMAPILI ZA ITALIA SERIE A: [saa za bongo]
AC Milan v Juventus, [saa 1 na nusu usiku]
Chievo v Inter Milan, [saa 10 jioni]
Kindumbwendumbwe cha kuingia LIGI KUU: Burnley 1 Reading 0
Katika mtoano maalum wa kutafuta Timu ya 3 itakayojumuika na Wolverhampton Wanderers na Birmingham kuingia LIGI KUU msimu ujao, leo Timu ya Burnley imeifunga Reading bao 1-0. Reading ilishushwa Daraja kutoka LIGI KUU England msimu uliokwisha.

Timu hizi zitaruadiana Mei 12 na mshindi atachuana na mshindi kati ya Preston na Sheffield United ambazo jana zilitoka suluhu 1-1 na ambazo zinarudiana tarehe 11 Mei.
Mchezaji wa Cameroun, Andre Bikey, anaechezea Reading alipewa Kadi Nyekundu na Refa baada ya kumkanyaga kwa makusudi Robbie Blake wa Burnley.
Bikey alipopewa Kadi hiyo alikasirika sana na kuvua jezi na kuichana.
Bikey atakumbukwa sana kwenye mechi ya Kombe la Mataifa ya Afrika alileta aibu kubwa alipompiga Mhudumu wa Kwanza alieingia uwanjani kumsaidia Mchezaji alieumia katika Nusu Fainali kati ya Cameroun na Ghana ambayo Cameroun walishinda 1-0.

Stoke City wajinusuru, wabaki LIGI KUU!!!!!!!

Stoke City wakicheza ugenini KC Stadium wamewafunga wenyeji wao Hull City mabao 2-1 na kufikisha pointi 42 ambazo zimewahakikishia kubaki LIGI KUU msimu ujao huku wakiwa wamebakisha mechi 2 ligi kufikia tamati. Kwa kipigo hiki, Hull City mpaka sasa hawajui hatima yao huku wakiwa na pointi 34 na wamebakisha mechi 2 tu, moja watacheza na Bolton ugenini na ya mwisho watakuwa nyumbani kupambana na Mabingwa Watetezi wa ligi hiyo Manchester United.
Hull wako nafasi ya 17 wakifuatiwa na Timu zilizo nafasi ya kuporomoka Daraja yaani nafasi ya 18 ni Newcastle pointi 31, nafasi ya 19 ni Middlesbrough pointi 31 na wa mwisho ni West Bromwich pointi 31 na yuko nafasi ya 20.
Newcastle na Middlesbrough, waliocheza mechi moja pungufu ya Hull City, wanacheza pamoja Jumatatu usiku na ikiwa Newcastle atashinda basi atakuwa na pointi 34 sawa na Hull City lakini Hull atashushwa hadi nafasi ya 18 kwa kuwa ana uhafifu wa magoli na hilo ni eneo hatari la kuporomoka Daraja.
Timu iliyo mkiani yashinda!!!! Je yaweza kujinusuru kuteremshwa Daraja?
West Brom 3 Wigan 1
West Bromwich Albion, Timu ambayo iko mkiani mwa LIGI KUU kwa muda mrefu sasa, leo imeweza kuifunga Wigan, Timu iliyo nafasi ya 11, kwa mabao 3-1 na hivyo kufikisha pointi sawa na Timu mbili zilizo juu yake, yaani Middlesbrough na Newcastle, zote zikiwa na pointi 31 lakini wanatenganishwa kwa tofauti ya magoli.
Timu hizi 3, Newcastle, Middlesbrough na West Brom, zote zipo nafasi za mwisho na kimsimamo Timu zinazokuwa nafasi hizo hushushwa Daraja mwishoni mwa ligi.
Juu ya Timu hizi ipo Hull City wenye pointi 34 lakini Newcastle na Middlesbrough, waliocheza mechi moja pungufu ya Hull City, wanacheza pamoja Jumatatu usiku na ikiwa Newcastle atashinda basi atakuwa na pointi 34 sawa na Hull City lakini Hull atashushwa hadi nafasi ya 18 kwa kuwa ana uhafifu wa magoli na hilo ni eneo hatari la kuporomoka Daraja.
West Bromwich wamebakisha mechi mbili moja wanacheza nyumbani na Liverpool na ya mwisho ugenini na Blackburn.
Blackburn 2 Portsmouth 0
Blackburn polepole wanaanza kujinasua toka balaa la kushushwa Daraja baada ya leo kuwapiga Portsmouth 2-0 na hivyo kufikisha pointi 40 na kuwaacha Portsmouth wakiwa na pointi 38.
Ingawa bado kimahesabu Blackburn hajanusurika lakini ushindi huu unawapa afueni kubwa hasa ukizingatia ukweli kuwa Timu tatu za mwisho ni Newcastle, Middlesbrough na West Brom , ambazo ziko hatarini kuporomoshwa Daraja zina pointi sawa, pointi 31, na kizuri zaidi ni kuwa Newcastle na Middlesbrough wanapambana wenyewe Jumatatu usiku.
MATOKEO KAMILI MECHI ZILIZOCHEZWA JUMAMOSI MEI 9 KUANZIA SAA 11 JIONI [Bongo taimu}
Blackburn 2-0 Portsmouth
Bolton 0-0 Sunderland
Everton 0-0 Tottenham
Fulham 3-1 Aston Villa
Hull City 1-2 Stoke City
West Brom 3-1 Wigan

Wababe Scotland wapambana leo: Rangers 1 Celtic 0

Huku kukiwa kumebakiwa mechi 3 tu kwa LIGI KUU Scotland kumalizika leo Rangers wamewafunga watani zao wa jadi Celtic bao 1-0 Uwanjani Ibrox, Glasgow na kuchukua uongozi wa ligi hiyo wakiwa na pointi 79 na Celtic wakifuatia wakiwa na pointi 77. Bao lililoinyuka Celtic lilifungwa na Davis dakika ya 37 na Davis huyo huyo akawa tena shujaa wa Rangers pale alipookoa mpira kwa kichwa kwenye mstari wa goli wakati Kipa wake keshapitwa.
Kabla ya mechi yao ya kesho, Wenger aikandya Chelsea!!!
Arsene Wenger, Meneja wa Arsenal, ameiponda Chelsea kwa kuwaambia pesa hazinunui mafanikio na kauli hii imekuja huku Timu hizo zinategemewa kupambana hapo kesho jioni kwenye LIGI KUU England katika mechi inayozikutanisha Chelsea iliyo nafasi ya 3 na Arsenal nafasi ya 4 kwenye msimamo wa ligi.
Pia mechi ya kesho inazikutanisha Timu mbili zilizotolewa wiki hii kwenye Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE wakati Arsenal ilitupwa nje na Manchester United kwa jumla ya magoli 4-1, Chelsea ilibwagwa kwa goli la ugenini baada ya kutoka sare 1-1 na Barcelona.
Wenger ameiponda Chelsea kwa kusema: 'Chelsea wametumia mamilioni ya pesa lakini mpaka sasa hajashinda Kombe la Ulaya!! Si kutumia pesa tu bali ni lazima kuendeleza msimamo wa kukuza vipaji!! Sisi tunaweza kuendelea zaidi kwani tuna Wachezaji chipukizi lakini wao Wachezaji wao wanashuka mlima na sisi ndio kwanza tunapanda kilima!! Tumeingia nne bora huko Ulaya, hatujafungwa mechi yeyote ya LIGI KUU tangu Novemba!! Ndio tumefungwa kwenye Nusu Fainali ya Ulaya na si kitu cha kuona haya kwani tumefungwa na Timu bora!! Manchester United ni Mabingwa wa Ulaya na Dunia!!!'
Ovrebo, Refa wa Chelsea v Barcelona, asema hakujificha!!!

Refa Tom Henning Ovrebo, raia wa Norway, aliechezesha Nusu Fainali ya Chelsea na Barcelona ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE amekanusha taarifa zilizozagaa kuwa amejificha kwa kuwa anawindwa kuuliwa na Mashabiki wa Chelsea.
Refa huyo alizua mzozo mkubwa kuhusu maamuzi yake ya utata na mara baada ya filimbi ya mwisho ya mchezo Wachezaji wa Chelsea walimzonga na kumkashifu kwa madai amewanyima penalti kadhaa.
Katika mechi hiyo Barcelona walisawazisha bao dakika za majeruhi na kuwatupa nje Chelsea kwa bao la ugenini.
Ovrebo amesema: 'Wikiendi ijayo nachezesha mechi huku Norway.'
Chelsea haimwadhibu Drogba!!

Meneja wa Chelsea, Guus Hiddink, ametamka kuwa Klabu yao haina nia ya kumpa adhabu yeyote Didier Drogba kwa utovu wa nidhamu alioufanya mara baada ya mechi ya Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE kati yao na Barcelona iliyomalizika 1-1 lakini Barcelona wakaingia Fainali kwa goli la ugenini.
Hiddink ametamka: 'Ndio ni makosa lakini hatumpi adhabu kwani ameshaomba radhi waziwazi. Tukimpiga faini haiwezi kumponya adhabu ya UEFA.'
Inasemekana Mwakilishi wa UEFA kwenye mechi hiyo, Janis Mezeckis kutoka Nchi ya Latvia ameandika kwenye ripoti yake kuhusu vitendo vyote vya Wachezaji wa Chelsea baada ya mechi hasa Drogba.
UEFA imeahidi kutoa tamko lao wiki ijayo.
ARSENAL NAO MATATANI NA UEFA!!!!

Kuna habari kwamba UEFA huenda ikaipiga faini Arsenal kufuatia vitendo vya baadhi ya Watazamaji uwanjani kwao Emirates kuonekana wakirusha chupa za plastiki za maji wakati Manchester United wakisherehekea bao la pili la Ronaldo katika pambano la Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE Jumanne iliyopita mechi ambayo Man U waliifunga Arsenal 3-1.
Inasemekana Refa wa pambano hilo Roberto Rosetti ameandika kwenye ripoti yake ya mechi hiyo kuhusu tukio hilo na sasa UEFA inategemewa kutoa tamko hapo Julai 23.
HOMA YA MAFUA YA KITIMOTO YAZITOA TIMU ZA MEXICO KWENYE COPA LIBERTADORES!!!

Klabu mbili za Mexico, Chivas Guadalajara na San Luis, zimelazimika kujitoa kwenye Kombe la Klabu Bingwa za Nchi za Marekani ya Kusini maarufu kwa jina la Copa Libertadores baada ya kukosa viwanja vya kuchezea mechi hizo kufuatia mlipuko wa gonjwa la ‘homa ya mafua ya kitimoto’ nchini Mexico ambako mpasa sasa watu 42 wamefariki.
Chivas Guadalajara walikuwa wawakaribishe Sao Paulo ya Brazil na San Luis walikuwa wawe wenyeji wa Nacional ya Uruguay.
Juhudi za mechi hizo kuchezwa nje ya Mexico ziligonga mwamba baada ya Serikali za Colombia na Chile kuvigomea Vyama vya Soka vyao kuwa wenyeji wa mapambano hayo kuogopa kuambukizwa gonjwa hilo.
Hivyo, Chama cha Soka cha Mexico kikawajulisha Shirikisho la Soka za Nchi za Marekani ya Kusini kujitoa kwa Timu zao.

Ferguson, Arshavin ndio BORA Aprili!!!

Meneja wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, ameshinda Tuzo ya Meneja Bora wa LIGI KUU kwa mwezi Aprili na Mchezaji wa Arsenal, Andrey Arshavin, ametunukiwa Tuzo ya Mchezaji Bora wa Aprili kwa ligi hiyo.
Sir Alex Ferguson ameshashinda Tuzo ya Meneja Bora jumla ya mara 23 na kwa msimu huu hii ni mara yake ya pili baada ya kushinda mwezi Januari. Ferguson amepata Tuzo hii baada ya kuiongoza vizuri Manchester United kushinda mechi 4 za ligi kati ya 4 walizocheza mwezi Aprili na kuwafanya wajizatiti kileleni mwa LIGI KUU. Nazo ni ile waliyoifunga 3-2 Aston Villa, Sunderland wakafungwa 2-1, Portsmouth 2-0 na kile kipigo cha 5-2 walichowashushia Totenham.
Andrey Arshavin amepewa Tuzo ya Mchezaji Bora baada ya kufunga goli 5 katika mechi 4 alizochezea Arsenal mwezi Aprili.
Mrusi Arshavin atakumbukwa aliifungia Arsenal mabao yao yote manne katika sare ya 4-4 na Liverpool katika mwezi huo.
Kindumbwendumbwe cha kuingia LIGI KUU: Preston 1 Sheffield United 1
Katika mtoano maalum wa kutafuta Timu ya 3 itakayojumuika na Wolverhampton Wanderers na Birmingham kuingia LIGI KUU msimu ujao, Timu za Preston na Sheffiled United zimetoka sare ya bao 1-1.
Timu hizi zitaruadiana Mei 11 na mshindi atachuana na mshindi kati ya Burnley na Reading ili kupata Timu moja itakayopanda Daraja.
Jumamosi Mei 9, Burnley watawakaribisha Reading katika mechi ya kwanza na marudiano ni Mei 12 huko nyumbani kwa Reading.
UEFA KUTOA UAMUZI HATMA YA CHELSEA NA WACHEZAJI WAKE WIKI IJAYO!!!
UEFA, Chama cha Soka Ulaya, kimetoa tamko kuwa watatoa uamuzi wa hatua zitakazochukuliwa wa ama kuwaadhibu Chelsea na baadhi ya Wachezaji wake au la wiki ijayo kufuatia vitendo vyao vya kumzonga na kumkashifu Refa kutoka Norway Tom Henning Ovrebo baada ya mechi ya Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE na Barcelona kwa madai kuwa aliwanyima takriban penalti 4 za wazi.
Pambano hilo liliisha bao 1-1 baada ya Andres Iniesta kuisawazishia Barcelona dakika za majeruhi na hivyo kuipa Barcelona ushindi kwa bao la ugenini.
Mara baada ya kipyenga cha mwisho, Wachezaji wa Chelsea hasa John Terry, Michael Ballack na Didier Drogba walimzonga Refa na Drogba akasikika akifoka na kutoa kashfa huku akizuiwa na Walinzi. Pia, Mchezaji mwingine, Jose Bosingwa, alikaririwa na vyombo vya habari akimwita Refa huyo 'mwizi'.
Hata hivyo Klabu ya Chelsea pamoja na Drogba na Bosingwa wameomba radhi kwa vitendo vyao.
Vilevile, UEFA imethibitisha haikupokea Rufaa yeyote kutoka kwa Barcelona ndani ya Masaa 24 kama kanuni zinavyotaka kuhusu Kadi Nyekundu ya Mchezaji wa Barcelona Eric Abidal na hivyo hawezi kucheza Fainali ambayo Barcelona watakutana na Mabingwa Watetezi Manchester United huko Rome Mei 27.
Thierry Henry huenda asicheze Fainali na Manchester United!!!
Klabu ya Barcelona imetangaza kuwa kuna wasiwasi mkubwa wa Mchezaji wao Thierry Henry, miaka 31, kutocheza Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE huko Rome Mei 27 watakapokutana na Mabingwa Watetezi Manchester United baada ya kuumia goti.
Henry hakucheza mechi ya Nusu Fainali huko Stamford Bridge walipotoka sare 1-1 na Chelsea na imethibitika hatocheza mechi ya Fainali ya Kombe la Spain ambayo Barcelona watakutana na Athletic Bilbao Jumatano ijayo. Vilevile atazikosa mechi 3 za La Liga ambazo Barcelona wamebakisha.
Thierry Henry aliumia Jumamosi iliyopita kwenye mechi Barcelona waliyoikung'uta Real Madrid mabao 6-2 huku Henry akipachika bao 2 na alitolewa kwenye dakika ya 60 baada ya kuumia.

Friday 8 May 2009

Nani kuungana na Wolves na Birmingham kupanda Daraja kuingia LIGI KUU England?
Baada ya Wolverhampton Wanderers kushika nafasi ya kwanza na Birmingham nafasi ya pili kwenye Ligi ya Coca Cola Championship na hivyo kuingia moja kwa moja LIGI KUU England msimu ujao, Timu ya 3 itakayounga nao itatokana na mtoano maalum unaozishirikisha Timu 4 zilizoshika nafasi ya 3 hadi ya 6 na nazo ni Reading, Preston, Burnley na Sheffield United.
RATIBA YA MTOANO HUO NI:
-MEI 8, PRESTON V SHEFFIELD UNITED
-MEI 9, BURNLEY V READING
-MEI 11, SHEFFIELD UNITED V PRESTON
-MEI 12, READING V BURNLEY
Mshindi kati ya Preston v Sheffield United na Burnley v Reading watakutana Fainali huko Wembley na ataeibuka mshindi wa Fainali hiyo ndio anapandishwa Daraja.
BOSINGWA NA DROGBA WAOMBA MSAMAHA!! Barcelona wamsifia Nahodha wa Chelsea John Terry!!!
Baada ya kumvamia na kumtukana Refa Tom Henning Ovrebo kutoka Norway aliechezesha mechi ya juzi kati ya Chelsea na Barcelona iliyoisha sare ya 1-1 lakini Barcelona ametinga Fainali kwa goli la ugenini, Wachezaji wa Chelsea Jose Bosingwa na Didier Drogba waomba radhi kwa kauli na vitendo vyao.
UEFA inachunguza vitendo vya Chelsea pamoja na Ripoti ya Refa na imeahidi kutoa uamuzi wa hatua gani zitachukuliwa wiki ijayo.
Wakati huohuo, Meneja wa Barcelona, Pep Guardiola, amemsifia Nahodha wa Chelsea John Terry kuwa ni muungwana na ni mwanamichezo wa kweli kwa kitendo chake cha kwenda kwenye chumba cha kubadili jezi cha Barcelona na kuwapongeza huku akimpa mkono kila mtu ndani ya chumba wakiwemo Makocha na Wachezaji wote.
Kitendo hicho kilishangiliwa sana na Wachezaji wa Barcelona na wakaanza kumuimba wakimpongeza.
Pep Guardiola amesema: 'Natoa shukrani zangu za dhati kwa John Terry! Ni muungwana wa kweli!!'
UEFA CUP: FAINALI NI Werder Bremen v Shakhtar Donetsk!!!
Jana Werder Bremen iliibuka na ushindi wa ugenini wa 3-2 dhidi ya Wajerumani wenzao Hamburg na hivyo kutinga Fainali ya UEFA CUP.
Katika mechi ya kwanza Hamburg walishinda pia ugenini kwa bao 1-0 lakini Werder Bremen wameweza kusonga mbele kwa kufunga magoli mengi ugenini.
Sasa Werder Bremen watapambana Timu ya Ukraine Shakhtar Donetsk waliowabwaga wenzao wa Ukraine Dynamo Kiev kwa mabao 2-1.
Shakhtar Donetsk pia waliifunga Dynamo Kiev bao 1-0 kwenye mechi ya kwanza.
Fainali ya Kombe hili ni 20 Mei 2009.
RATIBA LIGI KUU ENGLAND WIKIENDI HII: [saa ni za bongo]
Jumamosi, 9 Mei 2009
[saa 11 jioni]
Blackburn v Portsmouth
Bolton v Sunderland
Everton v Tottenham
Fulham v Aston Villa
Hull City v Stoke City
West Brom v Wigan
[saa 1 na nusu usiku]
West Ham v Liverpool
Jumapili. 10 Mei 2009
[saa 9 na nusu mchana]
Man U v Man City
[saa 12 jioni]
Arsenal v Chelsea
Jumatatu, 11 Mei 2009
[saa 4 usiku]
Newcastle v Middlesbrough
Jumatano, 13 Mei 2009
[saa 4 usiku]
Wigan v Man U [HII NDIO ILE MECHI YA KIPORO YA MAN U YA MUDA MREFU]

Thursday 7 May 2009

NI VURUGU BAADA YA CHELSEA KUTUPWA NJE!!
WACHEZAJI CHELSEA WALALAMIKIA NJAMA ZA KUZUIA ENGLAND KUWA NA TIMU 2 FAINALI!!

Wachezaji wa Chelsea wakiongozwa na Nahodha John Terry, Michael Ballack na Didier Drogba walimwandama Refa Tom Henning Ovrebo kutoka Norway wakilalamika uamuzi wake wa 'kuwanyima' penalti kadhaa baada ya Wachezaji wa Barcelona kuonekana wakiushika mpira ndani ya boksi.
Ballack alionekana akimshika Refa huyo huku Drogba akionekana mwenye ghadhabu akizuiwa na walinzi kumvamia na alibaki kuonyesha kidole na kufoka.
Nahodha wa Chelsea John Terry alilamika sana: 'Ni uamuzi mbovu! Nashangaa UEFA wanaweka Waamuzi dhaifu kwenye mechi kubwa! Tumekosa kuingia fainali kwa uamuzi mbovu!! Tizama mechi ya jana Darren Fletcher anaikosa Fainali kwa uamuzi mbovu!! Drogba hakufanya kosa ni haki kabisa kulalamika!!'
UEFA imesema inachunguza matukio hayo.
Lakini Meneja wa Chelsea, Guus Hiddink, ametetea vitendo hivyo kwa kusema ni kawaida damu kuchemka baada ya mechi na hakuna Mchezaji wake yeyote aliemvaa Refa Ovrebo ingawa yeye binafsi anashangaa kunyimwa penalti 3 au 4. Alipoulizwa kuhusu baadhi ya malalamiko ya Wachezaji wake waliosikika wakimpigia kelele Refa kwamba hizo ni njama za UEFA kuzuia Fainali ya Timu za England pekee, Hiddink alikataa kuamini kama kuna njama.
Manchester United waliingia Fainali juzi baada ya kuwatoa Arsenal.
MAN U WAWASILISHA RUFAA UEFA KUTENGUA KADI NYEKUNDU YA FLETCHER!!
Manchester United wamepeleka malalamiko yao rasmi kwa UEFA kuomba kuitengua Kadi Nyekundu aliyopewa Kiungo Darren Fletcher alietuhumiwa na Refa Roberto Rosetti kumchezea faulo Cesc Fabregas ndani ya boksi na Arsenal kupewa penalti iliyofungwa na Robin van Persie kwenye mechi ya juzi huko Emirates Stadium ambayo Man U waliwafunga Arsenal 3-1 na kuingia Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Kanuni za UEFA zinazuia rufaa za aina hiyo lakini Man U wameipeleka isikilizwe kwa 'misingi ya kibinadamu.'

Wednesday 6 May 2009

Chelsea nje!!
Ni Wanaume Manchester United v Barcelona huko Rome Mei 27!!!!

Chelsea, wakiwa kwao Stamford Bridge, wamekatwa maini dakika ya mwisho baada ya Andres Iniesta wa Barcelona kusawazisha bao dakika ya 90 na kufanya mechi iwe 1-1 na hivyo Barcelona kuingia Fainali kwa goli la ugenini. Mechi ya kwanza kati yao huko Nou Camp, Barcelona ilimalizika 0-0.

Chelsea walipata bao la kuongoza kipindi cha kwanza dakika ya 8 tu baada ya mpira uliopigwa na Frank Lampard kuelekea ndani ya boksi kumbabatiza Yaya Toure na kupaa juu na kumkuta Michael Essien alieachia kigongo kilichogonga besera juu na kushuka ndani ya wavu.

Eric Abidal wa Barcelona alipewa Kadi Nyekundu na Refa kutoka Norway Tom Henning Ovrebo kwa kumchezea rafu Anelka na hivyo atakosa kucheza Fainali.
Katika mechi hii, mara kadhaa Refa alionekana akiwaminya Chelsea penalti kadhaa.

Kwa matokeo haya, Fainali Rome, Italy ndani ya Olympic Stadium tarehe 27 Mei 2009 ni kati ya Mabingwa Watetezi Manchester United na Barcelona.
Baada ya Mechi=Kauli za Ferguson na Wenger!!

Baada ya kindumbwendumbwe cha jana cha Emirates Stadium ambapo Mabingwa Watetezi wa UEFA CHAMPIONS LEAGUE, Manchester United, waliwatoa nishai wenyeji wao Arsenal kwa kuwapiga bao 3-1 ukiwa ni ushindi wao wa pili baada ya kushinda 1-0 kwenye mechi ya kwanza huko Old Trafford na hivyo kutinga Fainali huko Rome hapo Mei 27 kupambana na mshindi wa leo kati ya Chelsea v Barcelona, Mameneja wa Timu zote mbili walizungumzia pambano.
FERGUSON:

-Walishindwa kumdhibiti Ronaldo-yeye ndio tofauti ya mechi hii!!!!
-Magoli mawili ya haraka yaliwatoa upepo!!
-Wenger anastahili sifa kwani anafanya kazi kwa bidii na uadilifu. Tatizo kwa Wenger na mimi ni kuwa kadri unavyozidi kudumu kwenye soka unapachikwa lebo nyingi tu! Ushinde au ufungwe. Ukifungwa, we ni bure tu hufai, ukishinda, we ndo kidume tu!!!
WENGER:

-Ni usiku mbaya sana kwenye maisha yangu ya soka!!
-Mashabiki walitegemea usiku mkubwa kwao. Tumewaangusha, inauma sana!!!
-Kitu kigumu ni kuwa hatujisikii kama tulicheza Nusu Fainali ya Ulaya!! Tulitolewa baada ya dakika 10 tu!!
-Hatumlaumu mtu binafsi!! Ndani ya dakika 3 tumepigwa bao 2 na hilo ni balaa kubwa!!
-Nahitaji kukaa mbali na msimu huu!! Tulicheza mechi 21 bila kufungwa lakini katika mechi kubwa na Chelsea na Man U hatukushinda na hilo linahitaji kulifikiri!!
-Lakini, tumefungwa na Man U timu inayofanya kuua ni kama sanaa na ukifanya kosa tu wanakumaliza!! Na Ronaldo alitupa wakati mgumu sana!!!

Mchezaji Mikosi: Joey Barton!!!!!!

Jumapili iliyopita, Joey Barton, Kiungo wa Newcastle alichapwa Kadi Nyekundu baada ya kumrukia miguu miwili Xabi Alonso wa Liverpool katika mechi Liverpool waliyoshinda mabao 3-0 na kuzidi kuitosa Newcastle kwenye hatari ya kushushwa Daraja.
Kwa kosa la kupewa Kadi Nyekundu, Joey Barton atakosa mechi 3 lakini kwa vile Newcastle imabakiza mechi 3 kumaliza ligi msimu huu ina maana msimu wa Joey Barton umeshakwisha mapema.
Sakata la Joey Barton halikuisha hapo kwani baada ya mechi hiyo kwisha yeye na Meneja wake Alan Shearer nusura wapigane ngumi ndani ya vyumba vya kubadilishia jezi na sasa Klabu yake ya Newcastle imeamua kumsimamisha kwa muda usiojulikana.
Kwa Joey Barton hili si tukio la kwanza kwani Joey Barton ana mlolongo wa mikasa ambayo inaweza kutungiwa muvi na ikashinda kila tuzo.
Joey Barton, ambae ameichezea Timu ya Taifa ya England mara moja, alinunuliwa na Newcastle kutoka Manchester City ambao walilazimika kumuuza baada ya yeye kumpiga na kumuumiza vibaya Mchezaji mwenzake Ousmane Dabo mazoezini.
Wakati kesi ya Ousmane Dabo iko Mhakamani, Joey Barton akakamatwa uraiani kwa kumpiga na kumjeruhi mtu na kuhukumiwa kwenda jela miezi 6.
Akiwa kifungoni, hukumu ya kesi yake ya kumjeruhi Ousmane Dabo ikatoka na akabahatika kupata kifungo cha nje cha miezi minne.
Lakini kwa tukio la Ousmane Dabo, Joey Barton akapewa adhabu na FA, Chama cha Soka England, ya kufungiwa mechi 12 [alipunguziwa ikawa mechi 6 na 6 zikawekwa kiporo kuangaliwa mwenendo wake] na kupigwa faini Pauni Elfu 25.
Huko nyuma Joey Barton ashapatwa na mikasa kibao na baadhi ni:
-Msimu wa 2004/5 kwenye Pati ya Chrismas ya Klabu ya Manchester City, Joey Barton alimchoma jichoni na moto wa sigara Mchezaji wa Vijana wa Timu hiyo. Alinusurika kufukuzwa.
-2005, kwenye ziara ya kabla ya msimu kuanza ya Manchester City huko Thailand, Joey Barton alimkung'uta shabiki wa Everton kwenye baa ya hoteli waliyofikia. Joey Barton akapandishwa ndege kurudishwa England na Klabu ikampa adhabu nyingine.
Tangu ajiunge na Newcastle kutokea Manchester City mwaka 2007, Joey Barton amecheza mechi 26 tu na amekosa mechi nyingi ama kwa kuwa jela au kufungiwa na FA au kuwa majeruhi.
Msimu huu ameichezea Newcastle mechi 9 tu na hiyo mechi ya Jumapili waliyocheza na Liverpool na kupewa Kadi Nyekundu ilikuwa ni mechi yake ya kwanza tangu auumie Januari 28 mwaka huu.
Wadau wengi wanadhani huu ndio mwisho wake Joey kuichezea Newcastle na wengi wanahisi hakuna Klabu huko England inayoweza kumpokea. Gordon Taylor, Bosi wa PFA [Professional Footballers Association] yaani Chama Cha Wachezaji Soka wa Kulipwa, amewasiliana na Mchezaji huyo na amesema Joey Barton anatambua madhara ya sakata lake hili la mwisho. Gordon Taylor amesema: 'Joey anajua ile ilikuwa rafu mbaya na ameomba radhi kwa Alonso, Refa na Meneja wake. Muda unazidi kuyoyoma kwa Joey lakini watu hawana budi kumvumilia na kumsaidia. Maisha yetu yamejaa watu ambao siku zote unajiuliza kama watajifunza. Na hii ni kwa Joey pia lakini tunachoomba asaidiwe hadi maisha yake kimpira yatakapoisha.'

Arsenal wapata faraja kidogo-yanyakua Kombe la FA la Wanawake!!!!!!
Wakati msimu huu unaisha kwa mara nyingine tena Arsenal kutokuchukua Kombe lolote na mara ya mwisho kuchukua Kikombe ilikuwa 2005 walipotwaa FA CUP kwa kuitoa Manchester United kwa matuta, Klabu hiyo imepata faraja kubwa baada ya Timu yao ya Wanawake kuifunga Sunderland 2-1 na kutwaa Kombe la FA la Wanawake.

Hii ni mara ya 4 mfululizo kwa Timu hiyo ya Wanawake ya Arsenal kuchukua Kombe hilo.

Hao Arsenal Wanawake wanaweza pia kutwaa Kombe la LIGI KUU England kwa Wanawake wakiifunga Everton wiki ijayo.
UEFA: 'KADI YA FLETCHER HAIFUTWI!!!'
UEFA, Chama cha Soka Ulaya, kimethibitisha Kiungo wa Manchester United, Darren Fletcher, ataikosa Fainali ya Klabu Bingwa Ulaya itakayochezwa huko Rome, Italy Mei 27 kati ya Klabu yake Manchester United na mshindi wa leo kati ya Chelsea v Barcelona, kwa sababu ya kupewa Kadi Nyekundu katika mechi ya jana Man U walipoiua Arsenal 3-1.
Fletcher alipewa Kadi Nyekundu dakika ya 75 baada ya Refa Roberto Rosetti kumdhania amemchezea rafu Cesc Fabregas wa Arsenal ndani ya boksi. Kwa kosa hilo, Refa huyo pia aliwapa Arsenal penalti waliyofunga bao lao moja.
Marudio ya video ya tukio hilo yalionyesha dhahiri Fletcher alicheza mpira na hivyo kupewa Kadi Nyekundu ni kosa. Hata Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, alikubali Refa alichemsha kwa uamuzi ule.
Baada ya mechi kulikuwa na dhana kuwa endapo Refa Roberto Rosetti ataandika kwenye ripoti yake ya mechi kuwa, baada ya kuliona tena tukio hilo, amegundua alifanya kosa na asingetoa Kadi Nyekundu, basi Fletcher atasamehewa na UEFA na hivyo kucheza Fainali.
Leo, UEFA imetangaza hairuhusiwi kukata rufaa yeyote kuhusu Kadi Nyekundu hata kama Refa anakubali kosa.
Taarifa ya UEFA ilifafanua: 'Manchester United wana haki ya kuleta malalamiko yao ndani ya saa 24 baada ya mechi. Lakini malalamiko hayo yanakubalika pale tu Refa akikubali kuwa alitoa Kadi, iwe Njano au Nyekundu, kwa Mchezaji mwingine kimakosa badala ya yule ambae kweli katenda kosa. Hamna Rufaa yeyote inayosikilizwa kuhusu maamuzi yeyote ya Refa. Kuhusu Fletcher hamna ushahidi wowote unaoonyesha Refa alimpa Kadi Nyekundu kwa makosa wakati aliecheza Rafu ni Mchezaji mwingine.'
Akieleza masikitiko yake, Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, amesema: 'Namheshimu Refa yule lakini ni juu yake kusema alikosea. Fletcher ni Mchezaji mkweli kabisa na kukosa Fainali ni mkosi mkubwa sana kwake!!'
Chelsea v Barcelona

Leo tena London inawaka moto na dunia nzima 'itakuwa huko jijini London' kushuhudia mechi ya marudiano ya Nusu Fainali Kombe la Klabu Bingwa Ulaya, UEFA CHAMPIONS LEAGUE, kati ya Chelsea na Barcelona huko Stamford Bridge nyumbani kwa Chelsea. Mechi hii itaanza saa 3 dakika 45 bongo taimu.
Mechi ya kwanza kati ya timu hizi iliyochezwa huko Nou Camp nyumbani kwa Barcelona iliisha 0-0 na leo lazima Chelsea ashinde ili kuingia Fainali kupambana na Mabingwa Watetezi wa Kombe hili, Manchester United, ambao jana waliwakung'uta Arsenal 3-1 huko Emirates Stadium, nyumbani kwa Arsenal.
Suluhu ya magoli ya aina yeyote ile itawapa mwanya Barcelona kuingia Fainali kwa vile wanacheza ugenini na mabao ya ugenini huhesabika mawili endapo timu zipo suluhu.
Chelsea leo watamkaribisha tena Beki wao wa pembeni kushoto Ashley Cole ambae aliikosa mechi ya kwanza kwa kuwa alikuwa na Kadi.
Lakini Barcelona ndio wenye pengo kubwa kwenye defense yao kwa kuwakosa Mabeki wao wawili wa kati, yaani sentahafu, kina Carles Puyol, mwenye Kadi, na Rafael Marques alie majeruhi. Inategemewa Gerrard Pique, Mchezaji Chipukizi wa zamani wa Manchester United, na Martin Caceres, toka Uruguay, wanaweza kuziba pengo hilo.
Hata hivyo, Barcelona wana wasiwasi mkubwa kuhusu kucheza kwa Mshambuliaji wao nyota Thierry Henry ambae aliumia goti siku ya Jumamosi Barcelona walipoibamiza Real Madrid 6-2. Henry jana alishindwa kufanya mazoezi na Barcelona wamesema leo atachekiwa ili kutoa uamuzi achezeshwe au la.
Meneja wa Chelsea, Guus Hiddink, akielezea kuhusu pambano la leo, alisema: 'Ushindi wao wa 6-2 kwa Real Madrid ni ubora wao. Sisi hatutishiki kwani kila mechi ni tofauti. Sisi tutacheza mpira wetu wa kawaida tu.'
Nae Meneja wa Barcelona, Pep Guardiola, amesema: 'Hatuwezi kushindana na Chelsea kwa mibavu kwani hio ndio staili yao. Itabidi tucheze staili yetu na staili yetu ni kumiliki mpira na kufunga magoli tu.'
Hii ni mechi ngumu isiyotabirika na iitakayokuwa na soka tofauti kwa kila Timu.
Kwa Chelsea, ni mechi muhimu sana hasa ukitilia maanani hawajawahi kuchukua Kombe hili na katika misimu 6 iliyopita wamefika Nusu Fainali mara 5 na msimu uliopita waliingia Fainali na kubwagwa na Manchester United waliotwaa Ubingwa.
Vikosi vitatokana:
Chelsea: Cech, Hilario, Belletti, Bosingwa, A Cole, Terry, Alex, Ivanovic, Lampard, Obi, Ballack, Essien, Kalou, Malouda, Drogba, Anelka, Stoch, Di Santo, Mancienne.
Barcelona: Victor Valdes, Pinto, Jorquera, Victor Sanchez, Caceres, Pique, Daniel Alves, Abidal, Sylvinho, Busquets, Iniesta, Hleb, Keita, Toure, Xavi, Eto'o, Messi, Henry, Gudjohnsen, Krkic, Pedro.

Mabingwa Man U waifumua Arsenal 3-1 nyumbani kwake, watinga Fainali Rome!!!


Wenger alia: 'Ni usiku mbaya maishani mwangu!!'

Mabingwa Watetezi wa Klabu Bingwa Ulaya, Manchester United, jana wamefanikiwa kuingia Fainali ya Kombe hilo kwa msimu huu baada ya kuwashindilia Arsenal mabao 3-1 uwanjani kwao Emirates katika mechi ya marudiano ya Nusu Fainali.
Katika mechi ya kwanza iliyochezwa Old Trafford, Manchester United walishinda kwa bao 1-0.

Mechi hii ya marudiano ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu sana hasa baada ya Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, kuwapa matumaini makubwa wapenzi wao kwamba watashinda mechi hii. Lakini, baada ya dakika 11 za kwanza tu za mechi, matumaini hayo yalizikwa pale Man U walipobandika bao mbili za haraka haraka ndani ya kipindi cha dakika tatu.

Bao la kwanza lilifungwa na Ji-Sung Park dakika ya 7 baada ya krosi ya Ronaldo kumfikia huku kila mtu akitegemea Beki Chipukizi wa Arsenal, Kieran Gibbs, angeunasa mpira huo lakini akateleza na mpira kumfikia Park aliemhadaa vizuri Kipa Almunia kwa shuti lake.

Bao la pili lilifungwa dakika ya 11 na Ronaldo alipofumua frikiki ya umbali wa mita kama 30 na kumbabaisha Kipa Almunia. Hadi mapumziko Man U walikuwa mbele kwa bao 2-0.
Kipindi cha pili, kwenye dakika ya 60, Arsenal walipata kona na ilipopigwa Vidic akaokoa kwa kichwa na mpira kumkuta Ronaldo aliempasia Park kwa kisigo na haraka Park akampa Rooney ambae alimwona vizuri Ronaldo ameshachomoka kwa kasi kubwa kuelekea golini kwa Arsenal, na Rooney hakuchelewasha, akatoa pasi murua kwa Ronaldo aliepachika bao la 3. Hilo lilikuwa shambulio la haraka na kustukiza ambalo Wataalam huliita 'counter attack!!'.
Dakika ya 75, Manchester United wakapata mkosi pale Darren Fletcher alipotwangwa Kadi Nyekundu baada ya Refa toka Italia Roberto Rosetti kuuamua amemchezea madhambi Cesc Fabregas ndani ya boksi na pia kutoa penalti iliyofungwa na Robin van Persie. Lakini marudio ya tukio hilo yameonyesha dhahiri Fletcher aliucheza mpira. Kwa Kadi hiyo Fletcher haruhusiwi kucheza Fainali.
Baada ya mechi, Arsene Wenger, aliekuwa na majonzi makubwa alikiri walizidiwa na hasa mabao mawili ya mapema yaliwatia kiwewe. Wenger vilevile alikiri usiku wa jana ulikuwa mbaya sana katika historia yake ya Soka ya zaidi ya miaka 25.
Kwa kufungwa jana Arsenal wanaendeleza wimbi la kutokushinda Kikombe chochote tangu mwaka 2005 walipotwaa Kombe la FA baada ya kuifunga Man U kwa matuta.
Vikosi vilikuwa:
Arsenal: Almunia, Sagna, Toure, Djourou, Gibbs (Eboue 45), Walcott (Bendtner 63), Fabregas, Song Billong, Nasri, Van Persie (Vela 79), Adebayor. Akiba hawakucheza: Fabianski, Silvestre, Diaby, Denilson.
Kadi: Nasri, Adebayor, Eboue.
Goals: Van Persie 76 pen.
Man Utd: Van der Sar, O'Shea, Ferdinand, Vidic, Evra (Rafael Da Silva 65), Fletcher, Carrick, Anderson (Giggs 63), Park, Ronaldo, Rooney (Berbatov 66). Akiba hawakucheza: Kuszczak, Evans, Scholes, Tevez.
Kadi Nyekundu: Fletcher (75).
Watazamaji: 59,867
Refa: Roberto Rosetti (Italy).

Tuesday 5 May 2009

NUSU FAINALI UEFA CHAMPIONS LEAGUE: Arsenal v Manchester United EMIRATES STADIUM, London Saa 3 dakika 45 Bongo Taimu


Baada ya kutunguliwa bao 1-0 wiki iliyokwisha Old Trafford kwa bao lililopachikwa na Beki John O'Shea, leo Arsenal wana nafasi nzuri ya kulipiza kisasi watakaporudiana na Mabingwa Watetezi wa Kombe hili la Klabu Bingwa Ulaya, Manchester United. Arsenal wako nyumbani Emirates Stadium na ili kuingia Fainali Arsenal lazima ashinde 2-0 na endapo Manchester United watapata bao moja kwenye mechi ya leo basi itabidi Arsenal afunge bao 3. Ni mechi ngumu isiyotabirika lakini ukimuuliza Arsene Wenger yeye anang'ang'ania lazima Arsenal isonge mbele!! Meneja huyo hayumbishwi na ana imani kubwa na timu yake. Arsene Wenger anasema: 'Ni kucheza kitimu si kibanafsi!!' Tulikosa umakini mechi ya kwanza lakini leo timu itabadilika!!'
Arsenal itaongezewa nguvu baada ya Mshambuliaji wao bora msimu huu Robin van Persie kupona majeraha yake lakini Mchezaji wao wa Kirusi Andrey Arshavin haruhusiwi kucheza kwa vile alichezea Kombe hili msimu huu alipokuwa na Klabu yake ya zamani Zenit St Petersburg.
Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, yeye anasema: 'Inabidi twende huko huku tukijaribu kufunga. Tukipata goli la ugenini itabidi Arsenal atufunge 3. Hilo litatufanya tuwe kwenye nafasi imara sana!!'
Mara ya mwisho Manchester United kucheza hapo nyumbani kwa Arsenal, Emirates Stadium, ilikuwa ni Novemba 8 mwaka jana kwenye mechi ya LIGI KUU England ambayo Arsenal walishinda 2-1 mabao yao mawili yakifungwa na Samir Nasri na lile la Man U liliwekwa na chipukizi Rafael.
Mechi ya leo itachezeshwa na Refa kutoka Italia, Roberto Rosetti, na ingawa ni mechi muhimu sana lakini kwa baadhi ya Wachezaji wa kila timu wataicheza kwa woga wa kutopata Kadi ya Njano kwani wakiikwaa hiyo tu basi wataikosa Fainali endapo Timu yao itafuzu kwenda Fainali.
Kwa Man U, Wachezaji wenye balaa la Kadi ni Wayne Rooney, Patrice Evra na Carlos Tevez. Wachezaji wa Arsenal walio hatarini ni Robin van Persie, Alexandre Song, Abou Diaby na Samir Nasri.
Vikosi vinategewa kutoka:
Arsenal: Almunia, Sagna, Toure, Djourou, Gibbs, Nasri, Song, Fabregas, Walcott, van Persie, Adebayor, Fabianski, Denilson, Silvestre, Diaby, Eboue, Bendtner, Ramsey.
Man Utd: Van der Sar, Foster, Kuszczak, O'Shea, Rafael, Neville, Ferdinand, Vidic, Evans, Evra, Fabio, Ronaldo, Anderson, Fletcher, Carrick, Scholes, Nani, Park, Giggs, Rooney, Tevez, Berbatov.

LEO NA KESHO MACHO YA DUNIA YAKO LONDON: MARUDIO NUSU FAINALI KUCHEZWA HUKO!!!!!!
Leo na kesho mji wa London utawaka moto kwani zile mechi za marudio za UEFA CHAMPIONS LEAGUE zitachezwa na leo ikiwa Uwanja wa Emirates, ambako Timu za England pekee zinakutana, wakati wenyeji Arsenal wataikaribisha Manchester United ambao ndio Mabingwa Watetezi wa Kombe hili.

Kwenye mechi ya kwanza iliyochezwa nyumbani kwa Man U Old Trafford, Man U walishinda bao 1-0 na hivyo Arsenal lazima ashinde 2-0 ili aingie Fainali. Endapo Arsenal wataruhusu Man U wapate bao moja basi itabidi wafunge bao 3 ili washinde.

Kesho ni zamu ya Stamford Bridge wakati wenyeji Chelsea wanarudiana na Barcelona baada ya kutoka dro mechi ya kwanza kwa bao 0-0 na hivyo Chelsea lazima ashinde ili asonge mbele kwani suluhu ya magoli ya aina yeyote ile itawapa ushindi Barcelona kwa vile wako ugenini na magoli ya ugenini huhesabika mawili endapo timu zinatoka suluhu.

Hata hivyo inabidi Chelsea waingie kwa tahadhari kubwa kwani Barcelona wakicheza ugenini tena nyumbani kwa Watani zao wa jadi, Real Madrid siku ya Jumamosi, waliifumua Real mabao 6-2!!

LIGI KUU ENGLAND: Hull City wazidi kudidimizwa!!!!

Jana usiku, Aston Villa wameifunga Hull City bao 1-0 kwa bao la John Carew uwanjani Villa Park na kuzidi kuwapa wasiwasi Hull wa kukumbwa na balaa la kushushwa Daraja kwani wako nafasi ya 17 na wako juu tu ya Timu 3 za chini za mwisho ambazo huteremshwa Daraja kwa pointi 3 tu.
Timu 3 za mwisho ni ile ya nafasi ya 18 inayoshikiliwa na Newcastle wakiwa na pointi 31 sawa na Timu ya 18 Middlesbrough.
Mkiani wapo West Brom wenye pointi 28.
Mechi zilizobaki Ligi kwisha ni 3.

Monday 4 May 2009

Benitez ni kama 'Fisi' anaenyemelea mkono wa mtu udondoke!!!!
Baada hapo jana ya kuipiga 3-0 Timu 'dhaifu' iliyo kwenye hatari kubwa ya kushushwa Daraja, Newcastle, Rafa Benitez wa Liverpool bado anajipa matumaini makubwa ya kutwaa Ubingwa!!
Liverpool wamebakisha mechi 3 kumaliza Ligi na wana pointi 77 wakati Mabingwa Watetezi, Manchester United, wana pointi 80 huku wakiwa wamebakiwa na mechi 4.
Baada ya ushindi wa jana Benitez alikaririwa akisema: 'Jana tungefunga mabao mengi! ila nimewaambia Wachezaji waongeze bidii kwani Manchester akifanya makosa tuchukue Ubingwa. Manchester ni timu nzuri lakini naamini watafanya makosa na tutawapita!'
Ili Liverpool achukue Ubingwa, kwanza, lazima ashinde mechi zake zote 3 zilizobaki na, pili, aombe Manchester United wapoteze mechi 2 kati ya zao 4 zilizobaki!!!
Lakini Manchester United anaweza kutwaa tena Ubingwa, bila kujali Liverpool kafanya nini, akishinda mechi 2 na kupata sare 1 katika mechi zake 4 zilizobaki.
MECHI ZILIZOBAKI [Timu inayotajwa kwanza iko nyumbani]:
LIVERPOOL:
-Mei 9, West Ham v Liverpool
-Mei 17, West Brom v Liverpool
-Mei 24, Liverpool v Tottenham
MANCHESTER UNITED:
-Mei 10,Man U v Man City
-Mei 13,Wigan v Man U
-Mei 16, Man U v Arsenal
-Mei 24, Hull City v Man U
Birmingham warudi tena LIGI KUU England!!!

Baada ya kuporomoshwa toka LIGI KUU England msimu wa 2007/8 na kukaa COCA COLA CHAMPIONSHIP kwa msimu mmoja tu, jana Birmingham wakicheza ugenini Madejski Stadium waliwafunga wenyeji wao Reading mabao 2-1 na kumudu kumaliza nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi, hivyo kupandishwa kwenda LIGI KUU, wakiwa nyuma ya Mabingwa wa Ligi hiyo Woverhampton Wanderers, maarufu kama Wolves, ambao nao wamepanda Daraja kwenda LIGI KUU. Timu nyingine iliyokuwa inawania kuipuka Birmingham ili kupanda Daraja hapo jana ilikuwa Sheffield United lakini ikakwaa kisiki pale ilipotoka sare 0-0 na Crystal Palace. Hata hivyo, ingawa Reading na Sheffield United zimekosa nafasi ya kupanda Daraja moja kwa moja, kwa kumaliza Ligi nafasi za 3 na ya 4, zitaingia kwenye kapu pamoja na Burnley iliyomaliza ya 5 na Preston ya 6, katika mtoano maalum wa kutafuta Timu moja kuungana na Wolves na Birmigham kupanda Daraja. Timu 3 za mwisho toka LIGI KUU England zitashushwa Daraja kwenda COCA COLA CHAMPIONSHIP kuchukua nafasi ya hizo 3 zilizopanda.

Newcastle na Sunderland zafungwa, hali ni ya hatari kwao!!!! Liverpool ashinda na kujipa matumaini ya Ubingwa endapo Man U atateleza!!

Jana, Timu ya Liverpool, ikiwa Anfield, iliibamiza bila huruma Newcastle mabao 3-0 na kujiongeza matumaini ya kutwaa Ubingwa endapo Man U atateleza lakini ushindi huo umezidi kuididimiza Newcastle katika balaa la kushushwa Daraja.
Wakati Liverpool ikijichimbia nafasi ya 2 wakiwa na pointi 77 kwa mechi 35 huku Man U akiendelea kuongoza kwa pointi 80 mechi 34, Newcastle wamechimbiwa nafasi ya 18 wakiwa na pointi 31 sawa na Middlesbrough walio nafasi ya 19. West Brom wako nafasi ya 20 na ya mwisho wakiwa na pointi 28.
Timu hizi tatu, Newcastle, Middlebrough na West Brom, ndizo zimekalia kuti kavu kwani zipo kwenye nafasi za timu zitakazoporomoka Daraja.
Juu yao kwenye nafasi ya 17 yuko Hull City mwenye pointi 34 lakini amecheza mechi moja pungufu mechi ambayo anaicheza leo usiku na Aston Villa.
Liverpool, wakicheza bila ya shujaa wao Fernando Torres lakini wakimkaribisha shujaa mwingine, Nahodha Steven Gerrard aliekosa mechi kadhaa kwa kuwa majeruhi, walipata ushindi huo wa mabao 3-0 kupitia kwa Yossi Benayoun, dakika ya 22, Kuyt [28] na Lucas[87].
Sunderland, wakicheza nyumbani, walipigwa mabao 2-0 na Everton na hivyo kubakizwa nafasi ya 16 kwenye msimamo wa ligi wakiwa na pointi 35 kwa mechi 35 [pointi moja tu juu ya Hull City waliocheza mechi moja pungufu] na wako pointi 4 tu juu ya Timu zilizo eneo la kushushwa Daraja huku kukiwa kumesaliwa mechi 3 Ligi kumalizika.
RATIBA LIGI KUU England:[saa za bongo]
Jumatatu, 4 Mei 2009
[saa 4 usiku] Aston Villa v Hull City
Jumamosi, 9 Mei 2009
[saa 11 jioni]
Blackburn v Portsmouth
Bolton v Sunderland
Everton v Tottenham
Fulham v Aston Villa
Hull City v Stoke City
West Brom v Wigan
[saa 1 na nusu usiku]
West Ham v Liverpool
Jumapili. 10 Mei 2009
[saa 9 na nusu mchana]
Man U v Man City
[saa 12 jioni]
Arsenal v Chelsea
Jumatatu, 11 Mei 2009 [saa 4 usiku]

Newcastle v Middlesbrough
Jumatano, 13 Mei 2009
[saa 4 usiku]
Wigan v Man U [HII NDIO ILE MECHI YA KIPORO YA MAN U YA MUDA MREFU]

Sunday 3 May 2009

RATIBA YA LIGI KUU ENGLAND:

Jumapili, 3 Mei 2009
[saa 9 na nusu mchana]
Liverpool v Newcastle
[saa 12 jioni]
Sunderland v Everton
Jumatatu, 4 Mei 2009
[saa 4 usiku]
Aston Villa v Hull
NANI KUPANDA DARAJA KUINGIA LIGI KUU ENGLAND MSIMU UJAO?
LEO NDIO MWAMUZI!!!!!!
Ligi iitwayo COCA COLA CHAMPIONSHIP ikiwa ni Daraja la chini tu ya LIGU KUU England leo inafikia tamati na mbali ya Timu ya Wolverhampton Wanderers, maarufu kama Wolves, ambayo tayari imenyakua Ubingwa na hivyo kupanda daraja kuingia LIGI KUU, Timu za Birmingham, Sheffield United na Reading bado zina matumaini ya kuungana na Wolves kwani mojawapo ikipata matokeo mazuri leo pia itapandishwa.
Kawaida ni Timu 3 hupanda Daraja na 3 hushuka toka LIGI KUU. Timu mbili zinazopanda Daraja moja kwa moja ni ile Bingwa na ya pili ni ile inayomaliza nafasi ya pili. Timu zinazoshika nafasi ya 3 hadi ya 6 hucheza mtoano maalum kuamua ipi moja itakayopanda Daraja.
Mechi muhimu za leo zitakazoamua Timu moja ipi itashika nafasi ya pili na hivyo kuungana na Wolves kupanda Daraja moja kwa moja na kuingia LIGI KUU msimu ujao ni:
-Crystal Palace v Sheffield United
-Reading v Birmingham
Birmingham wakiwafunga Reading watapanda Daraja.
Birmingham wakitoka suluhu wanaweza kupanda Daraja endapo tu Sheffield United hawashindi. Birmingham wakifungwa watakosa nafasi ya kupandishwa na wataingia kwenye mtoano maalum kuamua Timu ipi itashika nafasi ya 3 kupandishwa Daraja.
Sheffield United lazima washinde kwanza ili wawe na matumaini ya kushika nafasi ya pili na hivyo kupandishwa Daraja lakini hata hivyo hii itategemea matokeo ya mechi ya Reading v Birmingham.Ikiwa Sheffield United na Reading watashinda au Sheffield United watashinda na mechi ya Reading na Birmingham kuwa suluhu basi Sheffield United watapanda Daraja.
Reading pia lazima washinde na kuomba Sheffield United isishinde ili wapandishwe. Endapo Reading atashinda na Crystal Palace watatoka suluhu na Sheffield United Timu zote 3 yaani Reading, Birmingham na Sheffield United zitakuwa na pointi sawa, pointi 80, lakini Reading atapandishwa kwa kuwa na tofauti ya magoli bora.
Timu mbili kati ya Birmingham, Sheffield United na Reading ambazo zitakwama kupanda Daraja zitaingia moja kwa moja kwenye mtoano maalum wa Timu 4 kuamua ipi moja itaungana na Bingwa Wolves na Timu itakayoshika nafasi ya pili kupanda Daraja.
Timu nyingine 2 zitakazoingia kwenye mtoano huo maalum zitatokana na Timu za Cardiff, Burnley na Preston.
Hivyo, kwa kifupi, Wolverhamton Wanderers ashapanda Daraja na Timu mbili nyingine zitakazoungana nae kuingia LIGI KUU msimu ujao zitatoka kati ya Birmingham, Sheffield United, Reading, Cardiff, Burnley na Preston.

Middlesbrough 0-2 Man Utd

Manchester United polepole wananyemelea kutetea Ubingwa wao wa LIGI KUU England baada ya jana kushinda ugenini Riverside Stadium walipoifunga Middlesbrough, timu iliyo hatarini kuteremshwa daraja, mabao 2-0. Huku wakichezesha Kikosi kilichobadilika na kile kilichoifunga Arsenal ba0 1-0 siku ya Jumatano kwenye mechi ya kwanza ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE, Man U wakiongozwa na wakongwe wao Ryan Giggs na Paul Scholes waliandika bao la kwanza mfungaji Giggs dakika ya 25.
Kipindi cha pili mnamo dakika ya 52 Ji-Sung Park akafunga bao la pili kufuatia pasi murua ya Wayne Rooney.
Kwa ushindi huo, Man U sasa wana pointi 80 kwa mechi 34 wakiwa mbele ya Liverpool kwa pointi 6 ambao wana pointi 74 kwa mechi 34.
Leo jioni Liverpool wanaivaa Newcastle kwake Anfiled.
Lakini balaa kubwa lipo kwa Middlesbrough kwani wamebakisha mechi tatu tu na wako nafasi ya 19 huku wakiwa na pointi 31 sawa na Newcastle walio nafasi ya 18 huku West Bromwich iko nafasi ya 20 ambayo ni ya mwisho na wana pointi 28.
Timu zilizo nafasi ya 18, 19 na 20 hushushwa Daraja.
Middlesbrough: Jones, McMahon (Digard 55), Wheater, Huth, Hoyte, O'Neil (Emnes 70), Sanli, Bates, Downing, King (Alves 55), Aliadiere.
Akiba hawakucheza: Turnbull, Arca, Adam Johnson, Grounds.
Kadi: Huth.
Man Utd: Foster, O'Shea, Vidic, Evans, Evra (Rafael Da Silva 78), Park (Nani 74), Scholes, Giggs, Rooney, Berbatov, Macheda (Tevez 55).
Akiba hawakucheza: Kuszczak, Ronaldo, Anderson, Gibson.
Kadi: Macheda.
Watazamaji: 33,767
Refa: Mark Halsey
Chelsea 3-1 Fulham
Chelsea walianza mechi hii wakiwa kwao Stamford Bridge kwa moto mkubwa sana na iliwachukua sekunde 51 tu kuchomeka bao la kwanza lililoingizwa na Nikolas Anelka na Fulham wasawazisha dakikatu baadae mfungaji akiwa Erik Nevland.
Lakini kwenye dakika ya 10, Malouda akawapeleka mbele kwa kufunga bao la pili na Didier Drogba akaweka la 3 kipindi cha pili.
Sasa Chelsea wamebakisha mechi 3 na wako nafasi ya 3 nyuma ya Liverpool.
Chelsea: Cech, Bosingwa, Alex (Ivanovic 46), Terry, Ashley Cole, Lampard, Essien (Ballack 46), Mikel, Malouda, Anelka, Drogba (Di Santo 84).
Akiba hawakucheza: Hilario, Kalou, Belletti, Mancienne.
Fulham: Schwarzer, Pantsil, Hughes, Hangeland, Konchesky, Dempsey, Etuhu, Murphy, Gera, Zamora (Dacourt 76), Nevland (Kamara 35).
Akiba hawakucheza: Zuberbuhler, Gray, Stoor, Baird, Smalling.
Kadi: Murphy.
Watazamaji: 41,801.
Refa: Alan Wiley , Arsenal
Portsmouth 0-3 Arsenal
Kwa ushind huu, Arsenal wamejihakikishia angalau nafasi ya 4 kwenye ligi na hivyo kuwa na uhakika wa kucheza UEFA CHAMPIONS LEAGUE msimu ujao kwani timu inayowafukuza Aston Villa walio nafasi ya 5 sasa wamepitwa pointi 13 na wamebakisha mechi 4 tu.
Arsenal walifanya mabadiliko ya Kikosi huku wakipumzisha Wachezaji wa nane waliocheza Jumatano iliyopita na Man U lakini hilo halikuwazuia kutawala mechi hii ya ugenini na ushindi huo wa jana umewafanya sasa wawe wamecheza mechi 21 za ligi bila kufungwa.
Mabao ya Arsenal yalifungwa na Bendtner dakika ya 13 na 41 [kwa penalt]na Vela dakika ya 56. Portsmouth: James, Pamarot, Campbell, Distin, Hreidarsson (Kanu 46), Pennant (Utaka 46), Davis, Hughes, Mullins, Belhadj, Crouch.
Akiba hawakucheza: Begovic, Primus, Nugent, Basinas, Cranie.
Kadi Nyekundi: Pamarot (dakika ya 78).
Kadi: Campbell, Kanu, Davis.
Arsenal: Fabianski, Sagna, Song Billong, Djourou, Eboue, Walcott (Bischoff 64), Denilson, Ramsey (Randall 82), Arshavin, Bendtner (Merida 77), Vela.
Akiba hawakucheza: Mannone, Coquelin, Emmanuel-Thomas, Frimpong.
Kadi: Arshavin.
Watazamaji: 20,418
Refa: Lee Mason
MATOKEO MECHI NYINGINE ZA LIGI KUU:
Tottenham 1 West Brom 0
Man City 3 Blackburn 1
Stoke 0 West Ham 1
Wigan 0 Bolton 0
'EL CLASICO': Barcelona waibomoa Real Madrid nyumbani kwake!!!!!
Hizo ni salaam maalum kwa Chelsea!!!!
Barcelona, wakicheza ugenini Santiago Berbabeu uwanjani kwa Real Madrid, jana usiku waliwafumua watani zao wa jadi kwa mabao 6-2 na sasa kuongoza ligi wakiwa mbele kwa pointi 7.
Pengine hizi ni salaam maalum kwa Chelsea kwani baada ya kutoka suluhu 0-0 huko Nou Camp kwenye mechi ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE, sasa Barcelona watatua Stamford Bridge Jumatano kurudiana na Chelsea.
Real ndio walianza kufunga bao la kwanza kupitia kwa Gonzalo Higuain na Barcelona wakasawazisha kupitia kwa Thierry Henry na Puyol na Lionel Messi wakaongeza kuwafanya Barcelona wawe mbele 3-1.
Sergio Ramos akaifungia Real bao la pili lakini mvua ya Magoli iliendelea kuporomoshwa kupitia Thierry Henry, bao la 4, Lionel Messi la 5 na Mchezaji wa zamani wa Man U, Gerrard Pique, akafunga kitabu kwa bao la 6.

Powered By Blogger