Tuesday 5 May 2009

NUSU FAINALI UEFA CHAMPIONS LEAGUE: Arsenal v Manchester United EMIRATES STADIUM, London Saa 3 dakika 45 Bongo Taimu


Baada ya kutunguliwa bao 1-0 wiki iliyokwisha Old Trafford kwa bao lililopachikwa na Beki John O'Shea, leo Arsenal wana nafasi nzuri ya kulipiza kisasi watakaporudiana na Mabingwa Watetezi wa Kombe hili la Klabu Bingwa Ulaya, Manchester United. Arsenal wako nyumbani Emirates Stadium na ili kuingia Fainali Arsenal lazima ashinde 2-0 na endapo Manchester United watapata bao moja kwenye mechi ya leo basi itabidi Arsenal afunge bao 3. Ni mechi ngumu isiyotabirika lakini ukimuuliza Arsene Wenger yeye anang'ang'ania lazima Arsenal isonge mbele!! Meneja huyo hayumbishwi na ana imani kubwa na timu yake. Arsene Wenger anasema: 'Ni kucheza kitimu si kibanafsi!!' Tulikosa umakini mechi ya kwanza lakini leo timu itabadilika!!'
Arsenal itaongezewa nguvu baada ya Mshambuliaji wao bora msimu huu Robin van Persie kupona majeraha yake lakini Mchezaji wao wa Kirusi Andrey Arshavin haruhusiwi kucheza kwa vile alichezea Kombe hili msimu huu alipokuwa na Klabu yake ya zamani Zenit St Petersburg.
Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, yeye anasema: 'Inabidi twende huko huku tukijaribu kufunga. Tukipata goli la ugenini itabidi Arsenal atufunge 3. Hilo litatufanya tuwe kwenye nafasi imara sana!!'
Mara ya mwisho Manchester United kucheza hapo nyumbani kwa Arsenal, Emirates Stadium, ilikuwa ni Novemba 8 mwaka jana kwenye mechi ya LIGI KUU England ambayo Arsenal walishinda 2-1 mabao yao mawili yakifungwa na Samir Nasri na lile la Man U liliwekwa na chipukizi Rafael.
Mechi ya leo itachezeshwa na Refa kutoka Italia, Roberto Rosetti, na ingawa ni mechi muhimu sana lakini kwa baadhi ya Wachezaji wa kila timu wataicheza kwa woga wa kutopata Kadi ya Njano kwani wakiikwaa hiyo tu basi wataikosa Fainali endapo Timu yao itafuzu kwenda Fainali.
Kwa Man U, Wachezaji wenye balaa la Kadi ni Wayne Rooney, Patrice Evra na Carlos Tevez. Wachezaji wa Arsenal walio hatarini ni Robin van Persie, Alexandre Song, Abou Diaby na Samir Nasri.
Vikosi vinategewa kutoka:
Arsenal: Almunia, Sagna, Toure, Djourou, Gibbs, Nasri, Song, Fabregas, Walcott, van Persie, Adebayor, Fabianski, Denilson, Silvestre, Diaby, Eboue, Bendtner, Ramsey.
Man Utd: Van der Sar, Foster, Kuszczak, O'Shea, Rafael, Neville, Ferdinand, Vidic, Evans, Evra, Fabio, Ronaldo, Anderson, Fletcher, Carrick, Scholes, Nani, Park, Giggs, Rooney, Tevez, Berbatov.

No comments:

Powered By Blogger