Wednesday 25 February 2009

Wenger astushwa Timu yake kuanza kipindi cha pili ikiwa na Wachezaji 9 tu uwanjani!!!
Mourinho amkacha Ferguson baada ya mechi!!!

Leo, Liverpool ugenini, Chelsea nyumbani!!!

Vioja kwenye mechi za jana vilivyoacha gumzo kubwa kwa Wadau wa Soka ni pale Arsenal waliokuwa nyumbani Emirates wakicheza na AS Roma kukianza kipindi cha pili cha mchezo wakiwa na Wachezaji 9 tu ndani ya uwanja baada ya Mabeki Kolo Toure na William Gallas kuchelewa kuingia uwanjani wakati mechi inaanza kipindi cha pili.
Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, alihojiwa juu ya tukio hilo la ajabu alilielezea hivi: 'Ni kosa letu. Kengele inapolia lazima muwe tayari kutoka nje ya vyumba vya kubadilishia nguo. Tatizo lilikuja pale ile desturi na imani ya Kolo Toure ya kila siku kuwa wa mwisho kutoka chumbani na wa mwisho kuingia uwanjani! Kolo Toure ilibidi amsubiri Gallas aliekuwa anapatiwa matibabu na hilo lilimchelewesha Gallas kuvaa buti zake na kufunga vizuri gadi za ugoko. Toure ilibidi amsubiri Gallas atangulie ili yeye awe wa mwisho! Hawakujua kama mechi ilishaanza!'
Walipoibuka uwanjani wakakuta mechi ishaanza na Kolo Toure kwa pupa akaingia ndani bila ruhusa ya Refa na ikabidi Refa amtwange Kadi ya Njano.

Na huko San Siro, mara baada ya mechi kati Inter Milan na Manchester United kumalizika, Meneja wa Inter Milan hakuonekana kwenda kupeana mkono na mwenzake Sir Alex Ferguson kama ilivyo desturi mechi ikiisha.
Alipohojiwa, Mourinho alijitetea: 'Benchi letu la akiba lilipo tuna mlango maalum ambao hunipeleka moja kwa moja vyumba vya kubadilishia nguo! Sikumkimbia Ferguson na sisi ni marafiki! Mbona nimempelekea hotelini kwake chupa ya mvinyo wa Dola 300?'

Leo usiku ni zamu ya Liverpool na Chelsea kuingia vitani kupambana kwenye UEFA CHAMPIONS LEAGUE huku Liverpool wakiwa wageni wa Real Madrid ndani ya Uwanja wa Santiago Bernabeu na Chelsea akimkaribisha aliekuwa Meneja wa zamani wa Chelsea Claudio Ranieri akiongoza Timu yake Juventus ya Italy.

Mechi zingine za leo ni kati ya Sporting Lisbon ya Ureno na Bayern Munich ya Ujerumani na Villareal ya Spain na Panathinaikos ya Ugiriki.
FA CUP: Matokeo mechi za jana
Coventry 1 Blackburn o
Fulham 2 Swansea 1
Timu ya daraja la chini Coventry jana iliibwaga Blackburn iliyopo LIGI KUU na sasa watapambana na Chelsea kwenye Raundi inayofuata ya Kombe la FA mechi itakayochezwa tarehe 7 Machi.
Nao Fulham waliwabwaga Swansea na sasa watakutana na Manchester United hapo tarehe 7 Machi.

No comments:

Powered By Blogger