Tuesday 13 January 2009

MCHEZAJI BORA WA DUNIA NI---------Ronaldo!!!!!!!!!

Cristiano Ronaldo, Mchezaji kutoka Ureno anaechezea Klabu ya Manchester United ambao ni Mabingwa wa England, Ulaya na Dunia, amekuwa Mchezaji wa kwanza kutoka LIGI KUU England kunyakua Tuzo ya Mchezaji Bora Duniani ya FIFA kwa 2008.
Ronaldo amewashinda Wachezaji wengine mahiri kama Kaka wa AC Milan, Fernando Torres wa Liverpool na Lionel Messi na Xavi wa Barcelona.
'Ni wakati mkubwa sana kwangu na natoa tuzo hii kama zawadi kwa familia yangu, marafiki na Wachezaji wenzangu!' Alitamka Ronaldo.
Katika msimu ulioisha mwaka 2008, Ronaldo alifunga jumla ya mabao 42 na kuiwezesha Manchester United kunyakua Ubingwa wa England, UEFA Champions League na Ubingwa wa Dunia.
Ronaldo vilevile alishinda Tuzo za Mchezaji Bora wa Ulaya na Mchezaji Bora wa Dunia wa FifPro, tuzo inayotolewa na Wachezaji wa Kulipwa wa Dunia.
Ronaldo akipokea Tuzo hiyo ya Mchezaji Bora wa Dunia, alimsifia sana Meneja wake Sir Alex Ferguson kwa kusema: 'Ni kweli Meneja ni muhimu sana na Meneja huyo ndie aliekuwa mtu muhimu sana kwangu na nimejifunza mengi kutoka kwake! Uzoefu wake wa miaka mingi umeisaidia sana Klabu yangu na mimi binafsi! Ni heshima kubwa sana kuwa na Meneja Bora! Nina furaha kubwa sana kuwa sehemu ya historia ya Manchester United!'
Ronaldo ni Mchezaji wa pili kutoka Ureno kunyakua zawadi hii wa kwanza akiwa Luis Figo aliepewa mwaka 2001.
Kwa upande wa kina mama, kama ilivyotarajiwa, Marta wa Brazil alishinda kwa mara ya tatu mfululizo.

No comments:

Powered By Blogger