Wednesday 8 July 2009

Arsenal itajenga Timu, si kununua Timu!!
Mkurugenzi Mtendaji wa Arsenal Ivan Gazidis amesisitiza wao watajenga Timu na si kununua Timu wakati wakijitahidi kupata mafanikio ambayo wameyakosa tangu mwaka 2005 walipochukua Kikombe kwa mara ya mwisho walipolinyakua Kombe la FA.
Wakati Manchester United, Chelsea, Liverpool na Manchester City zinategemewa kutumia Mamilioni kununua Wachezaji, Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, hana bajeti kubwa ya kuingia Soko la Wachezaji na alichokifanya ni kuimarisha Mikataba ya Wachezaji wake Chipukizi waliokuwa nao kama vile Lukasz Fabianski, Kieran Gibbs, Aaron Ramsey, Theo Walcott, Jack Wilshere na Robin van Persie ambao wote Mikataba yao imeboreshwa na wote wamesisitiza kubaki Arsenal kwa muda mrefu.
Hata Nahodha Cesc Fabregas, anaevumishwa sana kwenda Barcelona, amesisitiza atabaki Arsenal.
Gazidis ametamka: ‘Sisi tunafuata njia nyingine. Sisi tunajenga Timu na hatununui Timu! Ndio maana Wachezaji wetu wanafuatwa fuatwa na Klabu nyingine!’
Inaelekea Real wasalimu amri kwa Ribery!!
Real Madrid, baada ya kumwaga ‘vijisenti’ kwa kuwachukua Ronaldo na Kaka, sasa inaelekea wameanza kuosha mikono kwa kukubali kushindwa kumbabadua Franck Ribery kutoka Klabu ya Ujerumani Bayern Munich.
Mkurugenzi Mtendaji wa Real, Jorge Valdano, akionyesha kukata tamaa, amesema: ‘Tunahisi Ribery haondoki Bayern msimu huu. Bayern wametumia njia nyingi kusema hawataki ahame! Wakati mwingine wanakataa moja kwa moja, wakati mwingine wanatamka dau kubwa sana, kama Euro Milioni 80, ambayo ni njia nyingine ya kusema hapana! Basi, tutasubiri kwani amebakisha miaka miwili na Bayern!’
Hata hivyo kunu fununu kuwa, baada ya Real Madrid kunyosha mikono, huenda Chelsea wakaingia mtamboni kumwania Ribery ingawa inaweza kuwa ngumu kumchukua kwani Ribery mwenyewe, kufuatia urubuni wa Balozi wa Real, Zinedine Zidane, ameweka bayana yeye anataka kwenda Real tu.

No comments:

Powered By Blogger