Thursday 9 July 2009

Mdau adai Arsenal haina pesa kununua Wachezaji!!!
Mrusi Alisher Usmanov, anaemiliki hisa Arsenal ambazo kiidadi zinamfanya yeye kuwa wa pili kwa kumiliki hisa nyingi, amedai kuwa Arsenal haina mtaji wa kuiwezesha kununua Wachezaji wapya.
Usmanov, aliejaribu kuishawishi Bodi ya Klabu hiyo kumpa pesa Arsene Wenger kununua Wachezaji, ametoa kauli inayosema: ‘Bodi imesema ina uwezo wa kununua Wachezaji lakini sisi wadau tunajua pesa hizo hamna!’
Mpaka sasa Arsenal imemununua Mchezaji mmoja tu Mlinzi wa Ajax, Thomas Vermaelen, waliemchukua kwa Pauni Milioni 10.
Hata hivyo alichokifanya Meneja Arsene Wenger ni kuimarisha Mikataba ya Wachezaji wake Chipukizi waliokuwa nao kama vile Lukasz Fabianski, Kieran Gibbs, Aaron Ramsey, Theo Walcott, Jack Wilshere na Robin van Persie ambao wote Mikataba yao imeboreshwa na kurefushwa na wote wamesisitiza kubaki Arsenal kwa muda mrefu.
FIFA yarekebisha sheria za Soka!
Katibu Mkuu wa FIFA Jerome Valcke ametangaza marekebisho kadhaa ya baadhi ya Sheria za Kandanda na marekebisho hayo yameanza kutumika Julai 1.
Kitu kikubwa katika marekebisho hayo ni ile Sheria Namba 11 inayohusu Ofsaidi na hasa hili limekuja baada ya kuibuka utata mkubwa kwenye EURO 2008 katika mechi ya Holland na Italy baada ya Ruud van Nistelrooy wa Holland kufunga goli huku akionekana ofsaidi lakini wakati alipopewa pasi Beki wa Italy alitoka uwanjani kwa kujiangusha nje ya uwanja ili kufanya van Nistelrooy aonekane ofsaidi lakini Refa akamhesabu kama vile alikuwa uwanjani na kulikubali goli.
Wakati huo, Sheria ilimtaka Refa amwonye Mchezaji huyo aliyejitoa Uwanjani na haikutamka lolote kuhusu kumhesabu kama bado yuko uwanjani na hivyo Mfungaji anahesabiwa sio ofsaidi.
Sasa FIFA imefuta utata huo na sheria hiyo ya ofsaidi inasema kuwa endapo Mchezaji atajitoa uwanjani ili kumfanya Mpinzani aonekane kazidi basi atahesabiwa yuko uwanjani na baada ya mpira kusimama Mchezaji aliejitoa uwanjani atapewa onyo kali.

No comments:

Powered By Blogger