Thursday 15 October 2009

MZOZO WA KUNG'OA JINO:
FIFA: Fellaini ruksa kuichezea Everton LIGI KUU Jumamosi!!
FIFA imewaruhusu Everton kumchezesha Kiungo wao Marouane Fellaini ambae amekumbwa na mzozo na Nchi yake Ubelgiji baada ya Mchezaji huyo kuondoka kwenye Kambi ya Timu ya Taifa ya Ubelgiji ambayo Jumamosi iliyokwisha ilicheza na Uturuki na jana ilicheza na Estonia na Chama cha Soka cha Ubelgiji [KBVB] kuijulisha Everton kuwa imemfungia Mchezaji huyo siku 5 kuanzia jana kama sheria za FIFA zinavyowapa uwezo.
Fellaini awali, baada ya mechi ya Uturuki Jumamosi iliyopita, aliruhusiwa na Kocha wa Ubelgiji Dick Advocaat kuondoka kambini kwenda kung'oa jino na hivyo kuruhusiwa kutokuwepo kambini kwa ajili ya mechi ya jana lakini inasemekana Kocha huyo alibadili mawazo na kumtaka Mchezaji huyo aendelee kuwepo kambini.
Hata hivyo Fellaini aliondoka kambini na ndipo KBVB ikawatumia faksi Everton kuwajulisha inatumia uwezo wanaopewa na FIFA kumfungia Mchezaji siku 5 kutochezea Klabu yake tangu aondoke kwenye mechi aliyotakiwa kuichezea Nchi yake na hivyo asingeruhusiwa kucheza Ligi Kuu Jumamosi ambapo Everton watacheza na Wolverhampton Wanderers.
Everton ililalamikia hatua hiyo ya KBVB na kusema wao kama Klabu hawahusiki na mzozo binafsi kati ya Mchezaji na Nchi yake.
FIFA leo asubuhi imewaruhusu Everton kumchezesha Fellaini hapo Jumamosi.

No comments:

Powered By Blogger