Friday 19 March 2010

EUROPA LIGI: Fulham, Liverpool zaingia Robo Fainali!
• Fulham yaibutua Juve 4-1!
Pengine jana ndio siku kubwa mno katika historia ya Fulham kwani baada ya kupigwa 3-1 katika mechi ya kwanza na Vigogo wa Italia Juventus kila mtu aliwaona wamekufa lakini hapo jana Fulham wakafufuka na kuiwasha Juventus 4-1 Uwanjani Craven Cottage na kutinga Robo Fainali ya EUROPA LIGI.
Fulham waliianza mechi hii vibaya mno pale walipofungwa bao dakika ya pili tu ya mchezo Mfungaji akiwa David Trezeguet lakini wakatulia na Bobby Zamora akasawazisha dakika ya 9.
Jahazi la Juventus likaanza kwenda mrama dakika ya 27 pale Beki wa Italia Fabio Cannavaro alipopewa Kadi Nyekundu baada ya kumchezea rafu Gera aliekuwa akienda langoni.
Gera akaipatia bao Fulham dakika ya 39 na kipindi cha pili akafunga tena kwa penalti na kufanya Fulham iwe mbele kwa bao 3-1 na hivyo kufanya Timu hizo ziwe sare kwa jumla ya bao 3-3 na endapo matokeo yangebaki hivyo basi nusu saa ya nyongeza ingebidi ichezwe.
Lakini Mchezaji alieingia kutoka benchi la akiba Clint Dempsey ndie alieleta furaha Craven Cottage kwa kupachika bao la 4 lililoipeleka Fulham Robo Fainali.
Kwa Juventus siku hiyo ilimalizika vibaya zaidi pale Zebina alipotwangwa Kadi Nyekundu na kuwaacha Juve wamalize mechi wakiwa mtu 9.
Huko Anfield, Liverpool walifuta kipigo cha mechi ya kwanza cha 1-0 mikononi mwa Lille na kuinyuka Timu hiyo bao 3-0 na kutinga Robo Fainali.
Liverpool walifunga bao la kwanza kwa penalti iliyopigwa na Kepteni Steven Gerrard na Supa Straika Fernando Torres akapachika bao 2.
Ushindi huu unawapa matumaini makubwa Liverpool kuwa huenda msimu huu angalau wakaambua Kombe moja kwani wameshatolewa Vikombe vingine vyote na kwenye LigI Kuu wanachopigania sasa ni kumaliza nafasi ya 4.
Matokeo kamili:
Sporting Lisbon 2 v Atletico Madrid 2 [jumla 2-2, Atletico wapita kwa magoli ya ugenini]
Marseille 1 v Benfica 2 [jumla 2-3]
Anderlecht 4 v Hamburg 3 [jumla 5-6]
Fulham 4 v Juventus 1 [jumla 5-4]
Liverpool 3 v Lille 0 [jumla 3-1]
Standard Liege 1 v Panathinaikos 0 [jumla 4-1]
Wolfsburg 2 v Rubin Kazan 1 [jumla 3-2]
Werder Bremen 4 v Valencia 4 [jumla 5-5, Valencia wanasonga kwa mabao ya ugenini]
Timu zilizoingia Robo Fainali:
-Atletico Madrid
-Benfica
-Hamburg
-Fulham
-Liverpool
-Standard Liege
-Wolfsburg
-Valencia
Riera atupwa nje ya Kikosi Liverpool!!
Baada ya kumbatukia Meneja wake Rafa Benitez kuwa ana chuki binafsi, Mchezaji wa Liverpool Albert Riera ameachwa kwenye Kikosi cha Liverpool kilichokuwa kikijitayarisha kucheza na Lille kwenye mechi ya EUROPA LIGI hapo jana.
Riera alitoa tuhuma hizo kwenye Radio Marca ya Spain kwa kudai anapuuzwa na Kocha wake na kutaka uhamisho aende Urusi ili kuweka hai matumaini yake kuichezea Spain Fainali za Kombe la Dunia.
Habari nyingine zimedai kuwa Riera ameambiwa asijihusishe na Timu hiyo hadi Jumatatu na hivyo hatakuwemo Kikosi cha Liverpool kitakachocheza Old Trafford Jumapili na Manchester United kwenye BIGI MECHI ya LIGI KUU.
BIGI MECHI Jumapili: Giggs ataka ushindi na Liverpool!!!
Msimu uliokwisha katika mechi ya marudio ya Ligi Kuu, Liverpool walipata ushindi wa bao 4-1 Uwanjani Old Trafford na kuwatoa nishai Mahasimu wao wakubwa Manchester United lakini hata hivyo walishindwa kunyakua Ubingwa na kuambua nafasi ya pili huku Man United wakiibuka Bingwa.
Safari hii wanakutana tena katika mechi ya marudio Old Trafford siku ya Jumapili lakini Liverpool wanachopigania safari hii ni angalau kuipata japo nafasi ya 4 tu kwa vile wamevurunda vibaya Ligi ya msimu huu.
Kwa Manchester United, waliobakisha mechi 8 kumaliza Ligi huku wakiongoza, ushindi ni muhimu mno ili kutwaa Ubingwa wa England kwa mara ya 3 mfululizo na kuweka historia.
Kiungo Veterani Ryan Giggs, ambae huenda akacheza mechi hii baada ya kuwa nje tangu mwishoni mwa Januari alipovunjika mkono kwenye mechi ya Ligi na Aston Villa, amenena: “Msimu uliokwisha hatukucheza vizuri na wao walistahili kushinda. Lakini hii ni mechi kubwa na muhimu kwetu! Wakati huu tunacheza vizuri na tunafunga magoli! Ushindi ni lazima!”
Giggs ameisaidia Man United kunyakua Ubingwa mara 11 na kuifikia rekodi ya Liverpool ya kuwa Bingwa mara 18 hivyo ushindi juu ya Liverpool ni muhimu kwake na pia kuivunja rekodi na kutwaa Ubingwa mara 19.
Hargreaves acheza mechi yake ya kwanza!!
Mchezaji wa Manchester United Owen Hargreaves ambae hajacheza tangu Septemba 2008 alipocheza mechi na Chelsea huko Stamford Bridge na kisha kusumbuliwa na matatizo ya magoti, Siku ya Alhamisi alicheza mechi yake ya kwanza kwa muda wa dakika 45 kwenye mechi ya Timu za Risevu za Manchester United na Burnley.
Hargreaves alifanyiwa operesheni za magoti yake yote mawili huko Marekani na kurudi kwake uwanjani kumekuwa kunaahirishwa mara kwa mara lakini katika mechi hiyo ya Risevu inadaiwa alicheza vizuri bila matatizo.
Hargreaves alinunuliwa kutoka Bayern Munich kwa Pauni Milioni 17 mwaka 2007 lakini ameichezea Manchester United mechi 37 tu kutokana na matatizo ya magoti.

No comments:

Powered By Blogger