Wednesday 19 May 2010

Barca wamnasa Villa
David Villa atatangazwa rasmi kama Mchezaji wa Barcelona siku ya Ijumaa baada ya kufanikiwa kumnunua kutoka Valencia kwa dau la Pauni Milioni 34.
Villa, miaka 28, amesaini Mkataba wa Miaka minne na Barcelona na kesho atapimwa afya yake.
Mchezaji huyo ambae ni mmoja wa Mastaa wakubwa wa Spain ameongeza joto kwa Mafowadi wa Barca hasa Thierrry Henry ambae sasa anaonekana kama ziada.
Man United kuchukua Mchezaji mmoja tu!!
Sir Alex Ferguson amepasua kuwa Manchester United inategemea kuongeza Mchezaji mmoja tu kabla Msimu ujao haujaanza na kauli hii imezua mjadala kwa Wadau wanaohisi Wamarekani Wamiliki wa Klabu hiyo, Familia ya Glazer, haitaki kutoa bulungutu kununua Wachezaji.
Hata hivyo, David Gill, Mkurugenzi Mtendaji, amekanusha hayo na kusema fedha zipo wakati wowote ule ila tatizo ni Soko la Wachezaji kupotoshwa kwa kupandishwa bila msingi thamani za Wachezaji.
Tayari Manchester United imeshawachukua kwa ajili ya Msimu ujao Wachezaji Chipukizi kutoka Mexico, Javier Hernandez, na Beki wa Fulham, Chris Smalling.
Ferguson ametamka: “Soko la sasa ni gumu lakini hata hivyo Kikosi chetu kina uwiano mzuri na kuna Vijana wengi tu!”
Kugushia wakati wa penalti marufuku!
Wapigaji penalti kuanzia sasa hawaruhusiwi kukimbia kisha kugushi na kusimama wakifika kwenye mpira na kisha kuupiga na Mchezaji akifanya hivyo atatwangwa Kadi ya Njano na penalti kurudiwa.
Mabadiliko hayo yamefanywa na Bodi ya Chama cha Soka cha Kimataifa [IFAB=The International Football Association Board] ambao ndio wenye mamlaka ya kubadili sheria za Soka na Bodi hiyo hujumuisha FIFA pamoja na Vyama vya Soka vya England, Scotland, Wales na Ireland ya Kaskazini ambao ndio Waanzilishi wa Soka Duniani.
FIFA imesema Mchezaji anaruhusiwa kugushi akiwa anakimbia lakini akifika kwenye mpira haruhusiwi.
Vilevile, IFAB imesema Yule Refa wa 4 [Refa wa Akiba] ambae kawaida husimamia ubadilishaji Wachezaji, nyongeza ya muda na kuzuia benchi la kila Timu kuingilia mchezo, sasa ataruhusiwa kuingia Uwanjani kumsaidia Refa katika maamuzi wakati wa mchezo.
Mabadiliko haya yanategemewa kuonekana kwenye Fainali za Kombe la Dunia zinazoanza Juni 11 huko Afrika Kusini.

No comments:

Powered By Blogger