Thursday 11 June 2009

Brazil 2 Paraguay 1
· Brazil ni Vinara Kundi lao!!
Mabao yaliyofungwa na Robinho na Nilmar katika mechi Brazil waliyoishinda 2-1 Paraguay, Nchi ambayo ilikuwa ikiongoza Kundi la Nchi hizo kwa muda mrefu, yameifanya Brazil wachukue uongozi wa Kundi la Nchi za Marekani ya Kusini katika kinyang’anyiro cha kwenda Fainali Kombe la Dunia Afrika Kusini 2010.
Paraguay walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Salfador Cabanas kwenye dakika ya 26 baada ya kupiga frikiki iliyombabatiza Elano anaechezea Manchester City na kumchanganya Kipa Julio Cesar. Robinho aksawazisha dakika ya 40 na Nilmar akafunga bao la ushindi dakika ya 50.
Brazil, baada ya kila Nchi kucheza mechi 14, inaongoza ikiwa na pointi 27, Chile wako nafasi ya 2 pointi 26, Paraguay ni wa 3 pointi 24, Argentina ni wa 4 pointi 22 na Ecuador wa 5 pointi 20.
Timu 4 za kwanza zitaingia moja kwa moja Fainali Kombe la Dunia na ya 5 itacheza mtoano na Timu moja kutoka Kundi la Nchi za Marekani ya Kati, Kaskazini na Carribean kupata mshindi atakaenda Fainali.
Ecuador 2 Argentina 0
· Maradona: ‘Tutafika Bondeni!!!’
Licha ya kufungwa katika mechi zao 2 katika 3 za mwisho za mchujo wa kwenda Fainali Kombe la Dunia, Kocha wa Argentina, Diego Maradona, ana uhakika Nchi yake itakwenda Fainali za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini mwakani 2010. Maradona amesema: ‘Nina imani na Timu hii!’
Ingawa Jumamosi Argentina ilishinda 1-0 dhidi ya Colombia, katika mechi yao ya mwisho iliyochezwa mwezi Aprili huko La Paz, Bolivia, mji ambao uko juu futi 12000 toka usawa wa bahari na hivyo kufanya kupumua kuwa shida, Argentina ilichapwa 6-1 na wenyeji Bolivia.
Jana, wakicheza mjini Quito, Ecuador, mji ulio juu Futi 9300 toka usawa wa bahari, Argentina wamechapwa 2-0 na wenyeji Ecuador.
Mchezaji wa Manchester United, Carlos Tevez, aliecheza kama Mshambuliaji pacha na Lionel Messi wa Barcelona, aliikosesha Argentina bao kwenye dakika ya 29 alipokosa penalti iliyochezwa na Kipa wa Ecuador Marcelo Elizaga ambae alizaliwa Argentina.
Mabao ya Ecuador, yakifungwa mwishoni na kudhihirisha uchovu wa Argentina kwenye uwanja ulio juu sana, yalifungwa na Marlon Avovi, dakika ya 72 na Pablo Palacios dakika ya 83.
Mechi inayofuata ya Argentina ni kuwa wenyeji wa Wapinzani wao wa Jadi Brazil hapo Septemba 5.
Mpaka sasa Argentina wako nafasi ya 4 nyuma ya Brazil, Chile na Paraguay katika Kundi la Nchi za Marekani ya Kusini. Timu 4 za kwanza zitaingia moja kwa moja Fainali Kombe la Dunia na ya 5 itacheza mtoano na Timu moja kutoka Kundi la Nchi za Marekani ya Kati, Kaskazini na Carribean kupata mshindi atakaenda Fainali.
MATOKEO MECHI NYINGINE MAREKANI YA KUSINI:
Colombia 1 v Peru 0

Venezuela 2 v Uruguay 2
Chile 4 v Bolivia 0

No comments:

Powered By Blogger