Friday 7 May 2010

Ancelotti aomba Wachezaji wake kuwa Kul!!
Bosi wa Chelsea Carlo Ancelotti amewataka Wachezaji wake kuwa watulivu watakapocheza Jumapili na Wigan Uwanjani Stamford Bridge katika mechi ya mwisho ya Msimu wa Ligi Kuu England ambayo Chelsea wakishinda tu wao ni Mabingwa wa 2009/10 na wakipata matokeo mengine zaidi ya hayo na Manchester United, watakaocheza nyumbani kwao Old Trafford na Stoke City kushinda, basi Man United watatwaa tena Ubingwa kwa mara ya 4 mfululizo.
Ancelotti amekiri Timu yake iko nafasi nzuri ya kuuchukua Ubingwa lakini ujumbe kwa Wachezaji wake umekuwa ni kuwataka waondoe hofu na kutulia.
Ancelotti amesema: “Kuwa Bingwa, lazima tucheze kama tulivyocheza na Stoke na Liverpool. Lazima tuwe na utulivu, tuwe na ukakamavu na nia ile ile!”
Safari hii, Ancelotti ataomba Chelsea iwe na bahati tofauti na ile iliyowapa kipigo cha 3-1 na Wigan walipokutana huko Uwanja wa DW mwezi Septemba katika mechi ya kwanza ya Ligi.
Fergie: ‘Wiki moja mbaya ilitugharimu!’
Sir Alex Ferguson ameungama kuwa wiki moja mbaya ndio imewaweka njia panda ya kuutetea Ubingwa wao wa Ligi Kuu kwa mara ya 4 mfululizo na pia kutoendelea kuwemo kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Wiki hiyo, mwezi Aprili, walifungwa na Chelsea 2-1 na wakatolewa na Bayern Munich kwenye UEFA CHAMPIONS LIGI kwa magoli ya ugenini.
Ferguson amesema: “Ilikuwa wiki mbaya na imetupotezea kila kitu!”
Baada ya kufungwa 2-1 huko Ujerumani na Bayern Munich, wakatoka sare 0-0 na Blackburn kwenye Ligi Kuu na kuwapa mwanya Chelsea kuongoza Ligi na hatimaye Chelsea kuishinda Man United kiutata bao 2-1 wiki hiyo hiyo.
Nae Kiungo wa Man United, Darren Fletcher, yeye anaamini uhakika wa wao kutwaa Ubingwa ulipata dosari pale walipokumbwa na majeruhi wengi na hata kubakiwa na Difenda mmoja tu alie fiti na kuwalazimu yeye mwenyewe, Michael Carrick na Chipukizi Ritchie De Laet kucheza Difensi na kufungwa 3-0 na Fulham.
Fletcher amesema: “Bila ya dosari ile mambo yangekuwa mengine! Tulicheza gemu 3 au 4 tukiwa na Difensi ya kuungaunga!”
LA LIGA: Pellegrini adai Ubingwa ni Wikiendi hii!
Kocha wa Real Madrid, Manuel Pellegrini, amedai Ubingwa wa Spain utaamuliwa wikiendi hii kutokana na mechi za Real Madrid v Athletic Bilbao na Sevilla v Barcelona ambazo zitafanya kila Timu ibakiwe na mechi moja tu Ligi kwisha.
Mpaka sasa Mabingwa Watetezi Barcelona wanaongoza Ligi hiyo kwa pointi moja mbele ya Mahasimu wao wakubwa Real Madrid.

No comments:

Powered By Blogger