Thursday 31 December 2009

MECHI YA LIGI KUU ENGLAND JANA YAWEKA HISTORIA: Hakuna hata Mchezaji mmoja wa England aliecheza!!!
  • Waingereza waja juu!!!!
Meneja wa Blackburn Rovers Sam Allardyce ameitabiria Timu ya Taifa ya England kuwa katika hali ngumu hapo baadae baada ya mechi ya Ligi Kuu hapo jana kati ya Portsmouth na Arsenal kuweka historia ya kuwa mechi ya kwanza kabisa katika Ligi hiyo kuchezwa huku hamna hata Mchezaji mmoja Raia wa England aliecheza.
Allardyce alisema: “Kwa Timu ya Taifa, hilo linasikitisha sana! Ligi Kuu na FA lazima walitazame hilo!”
Rais wa FIFA Sepp Blatter amekuwa akipiga kampeni ya kuanzisha Sheria inayoitwa “6 jumlisha 5”, ikimaanisha Timu lazima ziwe na Wachezaji watano Raia wa Nchi yenye Ligi yake au waliolelewa na Klabu za Nchi hiyo katika mechi moja lakini hilo limekuwa likipingana na Sheria za Haki na Uhuru wa Binadamu zilizowekwa na Jumuia ya Nchi za Ulaya.
Katika mechi hiyo iliyochezwa jana Jumatano Desemba 30 ambayo Arsenal iliifunga Portsmouth 4-1, Wachezaji 22 walioanza mechi hiyo walikuwa wanatoka Nchi 15 [hamna hata mmoja toka England] huku Ufaransa ikitoa Wachezaji 7.
Kulikuwa na Wachezaji wawili kutoka Algeria, na mmoja mmoja kutoka Bosnia, Ireland, Israel, Iceland, Afrika Kusini, Scotland, Ujerumani, Spain, Belgium, Wales, Cameroun, Croatia na Urusi.
Katika Wachezaji wa Akiba kulikuwa na wanne kutoka England na wawili kati yao, Craig Esmond wa Arsenal aliingizwa badala ya Mfaransa Samir Nasri, na, Portsmouth wakamuingiza Michael Brown badala ya Richard Hughes kutoka Scotland.
Historia hiyo iliwekwa hapo jana ikiwa ni miaka 10 baada ya Chelsea kuweka historia ya kuichezesha Timu bila Mchezaji hata mmoja toka England katika mechi yao na Southampton iliyochezwa Desemba 26, 1999.
Meneja wa Sunderland Steve Bruce aliunga mkono katika kuponda hali hiyo lakini alisema: “Hatutoi Wachezaji wazuri Chipukizi na ndio maana tunahaha dunia nzima kusaka Wachezaji wenye vipaji! Kila Meneja wa Klabu za England angependa kuwa na Wachezaji wa England lakini hamna vipaji!”
Nae Nahodha wa zamani wa Manchester United, Roy Keane, ambae ni Raia wa Ireland na kwa sasa ni Meneja wa Ipswich Town, alisema: “Hilo, pengine, litamuumiza kichwa Fabio Capello, Meneja wa England lakini kwangu halinikoseshi usingizi!!!”

No comments:

Powered By Blogger