Wednesday 30 December 2009

Meneja Bolton apigwa Shoka!!
Bolton Wanderers imethibitisha kuwa Meneja wao Gary Megson amefukuzwa kazi.
Megson alichukua Umeneja hapo Bolton Oktoba 2007 na katika msimu wake wa kwanza aliinusuru Klabu hiyo kushushwa Daraja na msimu uliokwisha aliinyanyua Timu na kumaliza nafasi ya 13 kwenye Ligi.
Lakini msimu huu, Timu hiyo imekuwa ikiyumba na katika mechi ya jana, wakiwa nyumbani, waliupoteza uongozi wa bao 2-0 na kuwaruhusu Hull City kupata sare ya 2-2.
Kimsimamo, Bolton wako nafasi ya 18 na wana pointi 18 kwenye Ligi ikiwa ni nafasi ya kushushwa Daraja ingawa wamecheza mechi chache (mechi 18) ukilinganisha na Timu nyingi zilizocheza mechi 20.
Wadau wengi wa Bolton wamekuwa hawampendi Megson na hata jana mara baada ya mechi na Hull kumalizika mwenyewe Megson alikiri Mashabiki wa Bolton hawamtaki.
Bolton imetangaza kuwa Timu itasimamiwa na Meneja Msaidizi Chris Evans ambae atasaidiwa na Kocha wa Timu ya Kwanza Steve Wegley.
Fergie: Ubingwa ni mbio za mtu 2!!!
Bosi wa Manchester United Sir Alex Ferguson anategemea kinyang’anyiro cha Ubingwa wa Ligi Kuu ni kupiganiwa na Timu mbili tu ambazo ni Man U na Chelsea huku Timu nyingine zinazoweka ngumu wakati huu kupukutika kadri Ligi inavyosonga mbele.
Ferguson amesema: “Kwa sasa haionekani hivyo lakini historia inatuambia ni Timu mbili tu ndizo zitakuwa wababe wa kugombea taji!! Chelsea ni hatari kubwa kwa sababu wana uzoefu mkubwa!”
Ferguson alitamka mwanzoni mwa msimu kuwa Chelsea ndie atakuwa mshindani wao mkubwa, na, licha ya upinzani mkubwa unaoonyeshwa na Timu mbalimbali kwa sasa, Ferguson bado anaamini Chelsea ndio tishio.
Ferguson amesisitiza: “Mwanzoni mwa msimu niliwaona Chelsea ndio tishio kubwa na bado sijabadili mawazo!”
Ukichukulia majeruhi yaliyowakumba Manchester United, na sasa Kipa Edwin van der Sar kwenda likizo ya muda usiojulikana kumuuguza mkewe ambae ni mgojwa sana, Man U kuwa nyuma ya vinara Chelsea kwa pointi chache kwenye Ligi ni kitu kinachowatia imani kubwa Wadau wa Mabingwa hao Watetezi.
Vilevile, kuweza kufunga mabao 40 katika mechi 19 za Ligi ni kitu cha mvuto hasa ukizingatia pengo la Mfungaji wao bora msimu uliopita, Cristiano Ronaldo, alietimkia Real Madrid.
Ferguson ametamka: “Watu wamechukulia kumpoteza Ronaldo kama pigo kubwa! Wamehisi hatuwezi kuwa wazuri kama alivyokuwepo! Ronaldo ni Mchezaji Bora sana! Lakini sisi tumebadilika na ukweli ni kuwa msimu uliokwisha baada ya mechi 19 tulikuwa na pointi 41, msimu huu kwa mechi 19 tuna pointi 40!!”

No comments:

Powered By Blogger