Thursday 4 February 2010

FA Cup: Leeds 1 Tottenham 3
Kwenye mechi ya marudianoya Kombe la FA huko Elland Road hapo jana, Leeds ilishindwa kuutumia vyema Uwanja wa nyumbani na kujikuta ikipigwa bao 3-1 na bao zote 3 za Tottenham zilifungwa na Starika Jermaine Defoe.
Timu hizi zilitoka sare 1-1 huko White Hart Lane mwishoni mwa Januari.
Tottenham imesonga mbele Raundi ya 5 ya Kombe hili na itasafiri kwenda kucheza na Bolton wiki inayokuja.
LIGI KUU: Fulham 1 Portsmouth 0
Bao pekee la Jonathan Greening limeipa ushindi Fulham na kuendeleza balaa kwa Timu ya mkiani Portsmouth ambayo pia ipo kwenye hali ngumu kifedha huku Wachezaji wake jana kwa mara ya 4 wakiingia Uwanjani Craven Cottage, nyumbani kwa Fulham, wakiwa hawana mishahara baada ya kuchelewa kuipata kwa mara ya 4 sasa.
Portsmouth walishindana kume pambano hilo na kukosa nafasi kadhaa za kufunga lakini walizamishwa kwa bao la dakika ya 74 kufuatia krosi ya Damien Duff kumkuta Greening aliepachika wavuni.
Jana Straika wa Italia Stefano Okaka aliichezea Fulham kwa mara ya kwanza tangu ahamie hapo kwa mkopo akitokea AS Roma hivi juzi.
Skandali la Terry: Hautemi Unahodha hadi abonge na Capello
Kuna taarifa kuwa John Terry, alieandamwa na kashfa kubwa ya kutembea na gelfrendi wa Mchezaji mwenzake Wayne Bridge aliekuwa nae Chelsea kabla hajahamia Manchester City, hatajiuzulu Unahodha wa Timu ya Taifa ya England kabla hajakutana na Meneja wa England Fabio Capello.
Terry na Capello wanategemewa kukutana siku ya Ijumaa ili kuzungumzia mkasa huo wa Terry na hatima yake kama Nahodha wa England ukizingatia skandali hilo.
Kashfa ya Terry ilifumuka baada ya Mahakama kuiondoa amri ya kutomtaja Terry iliyowekwa awali ili kuyazuia Magazeti yasiandike habari hizo.
FA imesema kuwa uamuzi wa Terry kubaki Nahodha au la anao Capello ambae kwa sasa yuko Uswisi akiuguza goti lake alilofanyiwa operesheni na anategemewa kutua London Alhamisi.
Huku Wadau wakimngoja kwa hamu Capello kusema yake, skandali hili la Terry linaweza kuchukua hatua mpya baada ya kuibuka tetesi kuwa huyo gelfrendi wa Wayne Bridge ambae ni Mfaransa aitwae Vanessa Perroncel ameshapokea bulungutu la Pauni Laki 250 kutoka Gazeti maarufu ili aelezee upande wake wa sakata hilo na hivyo kumfedhehesha zaidi John Terry.
LIGI KUU England: RATIBA WIKI NZIMA IJAYO
[saa za kibongo]
Jumamosi, Februari 6
[saa 9 dak 45 mchana]
Liverpool v Everton
[saa 12 jioni]
Bolton v Fulham
Burnley v West Ham
Hull v Man City
Man Utd v Portsmouth
Stoke v Blackburn
Sunderland v Wigan
[saa 2 na nusu usiku]
Tottenham v Aston Villa
Jumapili, Februari 7
[saa 10 na nusu jioni]
Birmingham v Wolverhampton
[saa 1 usiku]
Chelsea v Arsenal
Jumanne, Februari 9
[saa 4 dak 45 usiku]
Fulham v Burnley
Man City v Bolton
Portsmouth v Sunderland
Wigan v Stoke
Jumatano, Februari 10
[saa 4 dak 45 usiku]
Arsenal v Liverpool
Aston Villa v Man Utd
Blackburn v Hull
West Ham v Birmingham
Wolverhampton v Tottenham
[saa 5 usiku]
Everton v Chelsea
Beckham: ‘Man United ni kipenzi changu!’
Supastaa David Beckham amekiri kuwa Manchester United ni kipenzi chake cha kwanza na ana hamu kubwa sana ya kurudi kucheza Old Trafford wakati Timu anayochezea sasa hivi kwa mkopo AC Milan itakapoenda huko kuikwaa Man United baadae mwezi huu kwa pambano la Mtoano la UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Beckham alianza kucheza soka tangu akiwa mtoto kwenye Chuo cha Watoto hapo Manchester United na aliinukia na kuchezea Timu ya kwanza mechi 265 katika kipindi cha miaka 12 na kutwaa Mataji mengi hadi alipohama na kwenda Spain kuchezea Real Madrid mwaka 2003.
Beckham sasa anacheza soka lake huko Marekani akiwa na Timu ya LA Galaxy.
Beckham amesema: “Nilipoondoka Man United miaka ya mwanzoni ilikuwa migumu sana kwani niliimisi sana Timu hiyo! Ni Klabu pekee niliyotaka niichezee daima! Siku zote natamani bado ningebakia Man United! Mie ni shabiki mkubwa wao na hutazama mechi zao zote nikiwa na nafasi!”

No comments:

Powered By Blogger