Wednesday 14 April 2010

Arsenal wakataa kutaka kumuuza Fabregas Msimu ukiisha
Mwenyekiti wa Arsenal Peter Hill-Wood ametamka kuwa wana makubaliano na Barcelona ya kuitaka Klabu hiyo ya Spain isimrubuni Nahodha Wao Cesc Fabregas ambae amekuwa akivumishwa kwa muda mrefu kuwa yuko njiani kwenda Barcelona Msimu ujao.
Hill-Wood amesema: “Tuna makubaliano na Barca ya kuwataka wasimfuate Fabregas ila baadae wanaweza kuja kwetu moja kwa moja."
Mwenyekiti huyo alitilia mkazo imani yake kuwa makubaliano hayo hayawezi kuvunjwa na akasisitiza kwamba Arsenal na Barca walikutana Aprili 6 kulijadili hilo kwa mara nyingine na kukubaliana tena.
Fabregas ana Mkataba na Arsenal hadi mwaka 2014.
Lakini kila siku kumekuwa na uvumi kuwa Fabregas atarudi Barca Klabu aliyoanza kuichezea tangu akiwa mtoto.
Juve yampa siku 10 Rafa
Rafael Benitez amepewa siku 10 na Juventus aamue kama bado anataka kuhamia Klabu hiyo kwa Msimu ujao ili watayarishe listi yao ya nani wana nia ya kufanya kazi Juve.
Inaaminika listi ya Mameneja wanaotakiwa na Juventus ni pamoja na Kocha wa Brazil, Dunga, lakini Klabu hiyo kigogo ya Italia inamwona Benitez kama chaguo lao la kwanza.
Juventus ilimtimua Kocha wao Ciro Ferrara mwezi Januari na kumweka Kocha wa muda Alberto Zaccherano waliposhindwa kumchota Benitez wakati huo ingawa inadaiwa kulikuwa na makubaliano kati ya pande hizo mbili.
Inasemekana Benitez ameahidiwa donge nono la kununua Wachezaji, kitu ambacho hakipati Liverpool, na pia Juve kuhamia kwenye Uwanja mpya Makao Makuu yao Mjini Turin.
‘Wakombozi Wekundu’ wanakamilisha ofa ya Man United
Habari zimeibuka kuwa lile Kundi la Matajiri wanaotaka kuiondoa Manchester United mikononi mwa Familia ya Kimarekani ya kina Glazer, Kundi linaloitwa “Wakombozi Wekundu’, wanategemewa kukamilisha ofa yao ya kuinunua Klabu hiyo wiki hii.
Ingawa Wamiliki wa Manchester United, Familia ya Glazer, imekuwa ikidai Klabu hiyo haiuzwi, ‘Wakombozi Wekundu’ wana imani ofa yao itawafanya Wamarekani hao waisikilize na kusogea mezani kujadiliana.
Kundi hili pia limepata nguvu baada ya Man United kutolewa nje ya Mashindano ya UEFA CHAMPIONS LIGI na hivyo thamani ya Klabu kushuka chini.

No comments:

Powered By Blogger