Thursday 15 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Anelka atoboa mpasuko ndani ya France
Nicolas Anelka, ambae alitimuliwa toka Kikosi cha Ufaransa kwenye Kombe la Dunia huko Afrika Kusini baada kugombana na Kocha Raymond Domenech, ametoboa kuwa Wachezaji wote walikubaliana kugomea mazoezi baada ya yeye kufukuzwa.
Anelka amepasua hali ndani ya kambi ya France ilikuwa tete na kama isingekuwa yeye basi ni lazima Mchezaji mwingine angelipuka kwa hasira.
Pia, alisema ni Wachezaji wote kwa pamoja walikubaliana kugoma na hakuwepo kiongozi wa mgomo kwani kila mtu aliunga mkono.
Kauli hiyo ya Anelka iliungwa mkono na Mchezaji mwingine, Jeremy Toulalan, ambae alisema kuwa hakukuwa na kiongozi wa mgomo kwa vile hatua hiyo ilikuwa ya pamoja.
Msimamo huo wa Toulalan umepata pongezi toka kwa Anelka alietamka: “Ni ushujaa kwake kusimama na kusema ukweli! Ninasikia fahari kubwa kucheza nae Ufaransa!”
Hata hivyo, Anelka aligeuka mbogo kwa Bixente Lizarazu, Mchezaji wa zamani wa Ufaransa aliekuwemo France iliyochukua Kombe la Dunia 2008, ambae alikaririwa akimponda Anelka kwa kuwa mbinafsi na asiejituma huko Afrika Kusini wakati wa mechi.
Anelka alihoji: “Lizarazu- ni nani? Yeye ni Mchezaji wa zamani tu , aliekosa sifa na kutambuliwa, kwa vile alikuwa kivuli tu mbele ya kina Zinedine Zidane na Christophe Dugarry. Amesahau alikuwa Kombe la Dunia 2002? Sikuchukuliwa na sikusema lolote! Asizungumze kuhusu heshima, haijui huyo!”
Henry….huyooo aaga Ufaransa!!!
Thierry Henry ametangaza kujiuzulu kucheza Ufaransa.
Henry, ambae juzi tu ametangaza kuihama FC Barcelona kujiunga na MLS huko Marekani na Klabu ya New York Red Bulls, ameamua kung’atuka baada ya Miaka 13 ya kuwa na Timu ya Taifa ya Ufaransa.
Mchezaji huyo mwenye Miaka 32 alianza kucheza Ufaransa Mwaka 1997 na alikuwemo kile Kikosi kilichotwaa Kombe la Dunia Mwaka 1998 na EURO 2000 lakini alikumbwa na kashfa ya kushika mpira na mkono kwenye mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia 2010 dhidi ya Ireland iliyozua bao la kusawazisha kwa Ufaransa na kuifikisha Fainali huko Afrika Kusini.
Na huko Afrika Kusini, hakuwa na wakati mzuri na hakuanza hata mechi moja ya Kikosi cha Ufaransa kilichokumbwa na mzozo mkubwa wa kufukuzwa Anelka, Wachezaji kugoma na kisha kutupwa nje ya Kombe la Dunia wakiwa mkiani chini ya New Zealand kwenye hatua ya kwanza tu ya Makundi.
Henry ameichezea Ufaransa mara 123 na kufunga bao 51 na ndie Mfungaji Bora katika historia ya Timu ya Ufaransa.
Katika taarifa fupi, Henry ametamka: “Huu ndio mwisho wangu kwa Timu ya Taifa.”

No comments:

Powered By Blogger