Thursday 23 September 2010

Chelsea, Liverpool, Man City nje Carling!!!
• Hodgson aomba radhi!
Meneja wa Liverpool Roy Hodgson amelazimika kuomba radhi kufuatia Timu yake kuadhiriwa Uwanjani kwao Anfield na Timu ya Daraja la chini Northampton kwa kutolewa nje ya Carling Cup ilipopigwa na 4-2 kwa mikwaju ya penati baada ya kwenda sare 2-2 katika muda wa kawaida.
Northampton wapo Daraja la Ligi 2 ambayo ni Madaraja matatu chini ya Ligi Kuu.
Hodgson amesema: “Tumecheza na Timu ya chini na usiposhinda hilo ni jambo baya.”
Hodgson, ambae ametokea Fulham kumbadili Rafa Benitez alietimkia Inter Milan, amekiri kazi yake hapo Anfield ni ngumu na ameanza kwa mguu mbaya.
Mpaka sasa Liverpool wapo chini kwenye msimamo wa Ligi Kuu na wana pointi 5 tu kwa mechi 5 na walifungwa mechi yao ya mwisho ya Ligi na Manchester United kwa bao 3-2.
Wikiendi ijayo watakumbana na Sunderland kwenye Ligi Uwanjani Anfield.
Si Liverpool pekee waliokiona cha mtema kuni kwenye mechi za Raundi ya 3 ya Carling hapo jana kwani Chelsea na Manchester City nao wamebwagwa nje.
Chelsea wamefungwa 4-3 na Newcastle Uwanjani kwao Stamford Bridge na Manchester City walichapwa 2-1 na West Bromwich.
Mabingwa Watetezi wa Kombe hilo la Carling, Manchester United, waliangusha kichapo kwa Scunthorpe cha mabao 5-2.

No comments:

Powered By Blogger