Sunday 5 September 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

FIFA yawafungia Wacongo
FIFA imewafungia Wachezaji wawili wa TP Mazembe ya Congo DR kwa kuleta fujo kwenye mechi ya Kombe la Kagame huko Rwanda Mwezi Mei na kusababisha pambano kati ya APR ya Rwanda na TP Mazembe livunjike.
FIFA inalitambua rasmi Kombe la Kagame ambalo ndio hutoa Klabu Bingwa ya Nchi za Afrika Mashariki na Kati.
Wachezaji hao wawili wa TP Mazembe ni Nahodha wao Tresor Mputu Mabi, aliefungiwa Miezi 12, na Guy Lusadisu aliefungiwa Miezi 11.
CECAFA ililipeleka suala Wachezaji hao kwa CAF ambayo iliamua kuwafungia na sasa FIFA imepitisha rasmi Kifungo hicho ambacho kinahusu mechi za ndani na za Kimataifa.
Mputu na Lisadisu pia huichezea Timu ya Taifa ya Congo.
Polisi walimbamba Supa Mario na Bulungutu!
Wiki kadhaa baada ya kusajiliwa na ‘Timu Tajiri’ Manchester City kwa dau la Pauni Milioni 22, Mchezaji kutoka Italia, Mario Balotelli, maarufu kama Supa Mario, wakati akienda mazoezini asubuhi, Gari alilokuwa akiliendesha aina ya Audi R8 liligongana na Gari jingine.
Mara tu baada ya ajali hiyo iliyotokea Siku 8 zilizopita, Polisi wakatinga kwenye tukio na kama desturi ya huko Ulaya wakampima papo hapo ili kujua kama alikuwa njwii lakini akaonekana safi na ndipo walipompekua wakakuta kwenye mfuko wake wa nyuma wa suruali ana Pauni 5,000.
Polisi wakastuka kumwona Kijana wa Miaka 20, anaeongea Kiingereza kibovu, akiwa na pesa nyingi kama hizo na walipomhoji amepata wapi pesa nyingi kama hizo, Supa Mario, bila kusita wala kutetereka, akajibu: “Ni kwa sababu ni tajiri!”
Kitu kingine cha kushangaza katika tukio hilo la ajali ni pale ilipodhihirika Dereva wa Gari iliyogongana na la Supa Mario alikuwa ni Shabiki la kutupwa la Manchester City ambae alikuwa ana Tiketi ya Msimu kuingia mpirani kwenye mechi za Man City kwa Miaka 25 sasa.

No comments:

Powered By Blogger