Monday 6 September 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Hodgson aomba Liverpool iuzwe
Meneja wa Liverpool Roy Hodgson amesema kazi yake ya sasa ni kuhakikisha Kikosi cha Wachezaji wake wa sasa wanabaki pamoja hadi Wamiliki wapya wa Klabu watakapoingia na kumpa mtaji wa kukiimarisha.
Hadi sasa Liverpool imekuwa haiuziki ingawa Wamiliki wa sasa, Wamarekani wawili Tom Hicks na George Gillet, wamekuwa wakihaha kuiuza ili kuyakimbia madeni yanayoikaba Klabu hiyo.
Ingawa Hodgson, alierithi Umeneja kutoka kwa Rafael Benitez aliehamia Inter Milan, amekuwa akijitahidi kuwabakisha Wachezaji hivi karibuni alilazimika kumuacha Kiungo Javier Mascherano aende Barcelona.
Hodgson amesema: “Klabu inauzwa lakini hakuna anaejua mwelekeo wake mpya Wanunuzi wakiingia. Hali ikibadilika huenda tukapata fungu la kununua Wachezaji na kujiimarisha.”
Hata hivyo Hodgson amesisitiza Liverpool iliyopo itapigana kupata ushindi.
Shawcross wa Stoke amponda Wenger
Beki wa Stoke City, Ryan Shawcross, ambae hivi karibuni alishambuliwa na Meneja wa Arsenal Wenger kwa kuitwa Mcheza Raga, amejibu mapigo na kumshambulia Mfaransa huyo.
Stoke City ilipeleka malamiko rasmi kwa FA kuhusu Wenger lakini FA ilisema Meneja huyo hana kesi ya kujibu.
Hasira za Wenger kwa Shawcross zilianza mwanzoni mwa Mwaka huu pale Beki huyo wa Stoke alipomvunja mguu Chipukizi wake Aaron Ramsey.
Hivi karibuni, Wenger alimwita Shawcross Mcheza Raga na kuitaja mechi kati ya Stoke na Tottenham.
Shawcross amehoji: “Kila Mtu ana maoni yake lakini mechi ile haikuhusu Timu yake, kwa nini aizungumzie? Huyu Bwana ana lake kuhusu mimi. Inashangaza kuniingiza mimi. Siku zote ana matatizo na Stoke, Meneja wetu na baadhi ya Wachezaji wetu.”

No comments:

Powered By Blogger