Wednesday 21 April 2010

Mourinho achekelea na kuiponda Barca!!!
Jose Mourinho amewaponda Barcelona kwa kuwa wasahaulifu na kuanza kulaumu kunyimwa penalti katika kipigo cha 3-1 jana Uwanjani San Siro mikononi mwa Timu yake Inter Milan katika Nusu Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI.
Mourinho alisema: “Inasikitisha. Mwaka jana Chelsea walikuwa wanalia na Barca wakawa wanacheka na Refa. Walikuwa wanacheka kwa sababu Refa aliwanyima Vijana wangu wa Chelsea haki yao.”
Mourinho, ambae alikuwa Bosi wa Chelsea na kuondoka Septemba 2007, alikuwa akikumbushia Nusu Fainali ya Msimu uliopita ya UEFA CHAMPIONS LIGI kati ya Chelsea na Barcelona ambayo Barcelona walishinda kwa goli la ugenini baada ya Andres Iniesta kusawazisha dakika za majeruhi katika mechi ambayo Refa Tom Ovrebo aliwanyima Chelsea penalti kibao.
Katika mechi ya jana, Mchezaji wa Barca Daniel Alves alitwangwa Kadi ya Njano baada ya kujidondosha kwenye boksi huku Barca wakidai ilikuwa ni penalti.
Mourinho alikisifia Kikosi chake kwa kucheza kwa ustadi na kuifunga ‘Timu Bora Duniani.’
Nae Kocha wa Barcelona, Pep Guardiola, alikataa kutoa kisingizio cha uchovu kwa kusafiri kutoka Spain hadi Italia kwa Mabasi kufuatia kusimama kwa safari za anga huko Ulaya baada ya kukumbwa na balaa la majivu kutoka Volcano ya Iceland.
Guardiola amesema: “Hii hutokea kwenye Nusu Fainali ukicheza na Timu ngumu kama Inter. Najua Wachezaji wamechoka lakini hio sio sababu. Huko Barcelona, tutashambulia! Tutamwagia maji kiwanja ili mpira uwe unateleza haraka kwenye nyasi jambo ambalo hapa hawakufanya!”
Liverpool watua Madrid kwa ‘Daladala!”
Liverpool wamewasili Mjini Madrid huko Spain kwa ajili ya pambano lao la Nusu Fainali ya EUROPA LIGi la kesho watakapocheza na Atletico Madrid baada ya safari ya zaidi ya Maili 1200 kwa kutumia Treni, Basi na Ndege.
Usafiri huo mgumu umesababishwa na athari ya Majivu ya Volcano kutoka Iceland iliyolipuka na kutapakaza Majivu yaliyosimamisha safari za Ndege eneo kubwa la Ulaya.
Liverpool walianza safari yao Siku ya Jumanne.
Na wenzao Fulham ambao pia wanacheza Nusu Fainali ya EUROPA LIGI hapo kesho huko Ujerumani watakapokutana na Hamburg wamelazimika pia kusafiri kwa usafiri wa ardhini .

No comments:

Powered By Blogger