Wednesday 21 April 2010

Nasri: ‘Inakera hatuna Kombe Msimu huu!!!’
Samir Nasri anaamini si haki kabisa kwa Timu yake Arsenal kukosa Kikombe kwa mara nyingine tena Msimu huu wakibaki wakiuendeleza ukame wa Vikombe tangu mwaka 2005 ingawa anaamini tatizo lao kubwa lilikuwa kukabiliwa na majeruhi wengi.
Wengi wanahisi nafasi ya Arsenal ya mwisho kupata Kombe ilipotezwa pale walipoumwaga uongozi wa bao 2-0 huku dakika zimebaki 10 tu na kujikuta wakichapwa 3-2 na Wigan kwenye mechi ya Ligi Kuu wikiendi iliyopita na kuwafanya wawe nyuma ya vinara Chelsea kwa pointi 6 huku mechi zimebaki 3.
Staa wa zamani wa Arsenal Ian Wright ametamka kuwa Klabu hiyo inahitaji mabadiliko makubwa ikiwa wanataka kurudia mafanikio ya enzi zao.
Lakini Samir Nasri anadai, chini ya Wenger, Timu ina mwelekeo mzuri na alisisitiza: “Inakera! Tunafanya kazi kubwa lakini hatupati mafanikio, hatushindi Vikombe! Si haki kwani sisi tunastahili sana kupita wale wanaojenga Timu kwa kutumia pesa nyingi!”
Nasri anaamini kama wasingekuwa na majeruhi wengi Msimu wote lazima wangepata mafanikio.
Kwa nyakati tofauti, Arsenal walikumbwa na kuumia kwa Mastaa kama vile Robin van Persie, Nahodha Cesc Fábregas, Andrey Arshavin na Theo Walcott.
Hata mwenyewe Nasri alikumbwa na balaa la kuvunjika mguu kabla Msimu huu haujaanza.
Wadau wengi wanahisi ni wajibu wa Wenger kukiimarisha Kikosi chake, hasa Defensi, kwa vile Wakongwe kina Sol Campbell, William Gallas na Mikaël Silvestre watakuwa wamemaliza Mikataba yao mwishoni mwa Msimu huu.
Lakini mpaka sasa hakuna anaejua kinachoendelea labda ule ‘uhakika’ wa Straika toka Morocco anaechezea Bordeaux ya Ufaransa, Marouane Chamakh, kutua Arsenal.

No comments:

Powered By Blogger