Thursday 28 January 2010

KOMBE LA AFRIKA: Leo Watani wa Jadi wakumbana Nusu Fainali !!!
  • Ni Algeria v Misri na Ghana v Nigeria
Kihistoria, mechi za leo zinakutanisha Nchi ambazo zina ushindani wa jadi ambao mara nyingine huzua balaa hata nje ya Uwanja wa Mpira hasa kwa mechi za Misri v Algeria na mfano ni hivi karibuni Nchi hizo zilipokutana kwenye Mtoano wa Kombe la Dunia na ukazuka mtafuruku mkubwa na hata Basi la Wachezaji wa Algeria kupigwa mawe huko Cairo mwezi Novemba mwaka jana.
Vurugu hizo zilitapakaa hadi Nchini Algeria ambako Wamisri walishambuliwa na wengi kuikimbia Nchi hiyo.
Pia kulikuwa na ripoti kuwa Jamii za Raia wa Nchi hizo waishio Ufaransa walipambana baada ya mechi hiyo ya Cairo.
Lakini Wadau wanategemea mechi za leo zitaisha salama huko Angola ingawa kila Nchi imethibitisha kuwapeleka mamia ya raia zao kwa ndege maalum.
Ghana na Nigeria watacheza Uwanja wa Novemba 11 huko Luanda, Angola na mechi yao itaanza saa 1 usiku saa za bongo.
Nigeria watamkosa Mlinzi Onyekachi Apam ambae alipewa Kadi Nyekundu kwenye mechi ya Robo Fainali waliyowatoa Zambia kwa penalti.
Ghana wao wanategemea kuwa na Kikosi chao kamili.
Algeria na Misri zipo Uwanja wa Ombaka huko Benguela na mechi yao itaanza saa 4 na nusu saa za bongo.
Beki wa Misri Wail Gomaa ameeleza kuwa wao hawataki kisasi na Algeria kwa kuwabwaga nje ya Kombe la Dunia ila wanachotaka tu ni ushindi.
Washindi wa mechi za leo watakutana Fainali Jumapili.
MECHI ZA LIGI KUU JANA: Ushindi kwa Chelsea, Everton na Blackburn Rovers, Villa na Arsenal ngoma ngumu!!!
Chelsea wameukwaa tena uongozi wa Ligi Kuu kwa kuwapiga Birmingham City mabao 3-0 huku Aston Villa na Arsenal wakitoka suluhu ya 0-0.
Everton, wakiwa kwao Goodison Park, waliwabutua Sunderland 2-0 na kuendeleza kwao wimbi la matokeo mazuri.
Nao Blackburn wamezidi kujikongoja kujinasua toka eneo la hatari la mkiani kwenye msimamo wa Ligi kwa kuifunga Wigan 2-1.
Ushindi wa Chelsea uliowapa uongozi wa Ligi Kuu uliletwa na mabao ya Malouda na Lampard aliefunga mawili.
Arsenal walibanwa na Aston Villa na hivyo kushindwa kuipiku Manchester United toka nafasi ya pili na sasa wamebaki wakiwa wa 3 wakiwa pointi moja nyuma Man U kwa mechi sawa zilizochezwa.
Pia, Arsenal wamepata pigo kubwa kwenye mechi hiyo baada ya kuumia kwa Beki wao alionyesha umahiri mkubwa Msimu huu, Thomas Vermaelen, ambae inahofiwa amevunjika mfupa mguuni.

No comments:

Powered By Blogger