Saturday 29 May 2010

Fergie ni Mhusika Mkuu kuteua Mrithi wake
Bosi wa Manchester United Sir Alex Ferguson ndie Mhusika Mkuu wa kumchagua nani amrithi endapo ataamua kustaafu na hilo limetamkwa na Mkurugenzi Mkuu David Gill.
Ferguson amekalia wadhifa wake kwa Miaka 23 na kuisaidia Man United kunyakua Vikombe 34 vikiwemo 11 vya Ubingwa wa Ligi Kuu England na viwili vya Klabu Bingwa Ulaya.
David Gill amesistiza ushauri wa Ferguson ni muhimu katika uteuzi wa Mrithi wake lakini mpaka sasa hawajui ni lini Ferguson atang’atuka.
Gill pia ameongeza kuwa wakati Ferguson akiamua kustaafu wataunda jopo litalowashirikisha yeye, Sir Bobby Charlton, Sir Alex Ferguson na Wamiliki wa Klabu hiyo, Familia ya Glazer, ili kumtafuta Mtu atakaefaa kuwa Meneja.
Kuhusu habari zinazodai kuwa Jose Mourinho akitua Real Madrid anataka kumchukua Wayne Rooney huko, Gill amepuuza habari hizo kwa kusema: “Hawezi kwenda huko. Hatakubali kwenda huko. Hizi ni kelele tu. Sizijali!”
MECHI YA KIRAFIKI: Kesho England v Japan
Kesho England inacheza mechi yake ya mwisho ya majaribio kabla Kikosi chake hakijapunguzwa na kubakisha Wachezaji 23 watakaowasilishwa FIFA hapo Jumanne, Juni 1.
England, ambao wako kambini huko Austria, watacheza na Japan Jumapili, Mei 30 Uwanja wa UPC Arena Mjini Graz, Austria katika mechi itakayoanza saa 9 na robo mchana, saa za bongo.
Kocha wa England, Fabio Capello, inasemekana atafanya mabadiliko katika Kikosi chake kwa kuwaanzisha Tom Huddlestone wa Tottenham na Darren Bent wa Sunderland.
Vilevile, Wachezaji wa Chelsea John Terry, Ashley Cole na Frank Lampard watacheza mechi hiyo baada ya kuikosa mechi ya Jumatatu iliyopita England walipocheza na Mexico huko Wembley na kushinda 3-1.
Vikosi vinategemewa kuwa:
England:
David James, Glen Johnson, John Terry, Rio Ferdinand, Ashley Cole, Theo Walcott, Tom Huddlestone, Frank Lampard, Aaron Lennon, Wayne Rooney, Darren Bent.
Japan:
Narazaki, Uchida, Nakazawa, Tanaka, Nagatomo, Tamada, Endo, Hasebe, Nakamura, Okazaki, Honda.

No comments:

Powered By Blogger