Sunday 23 May 2010

Kibopa wa Nigeria ataka hisa Ze Gunners!!!
Bilionea mmoja wa huko Nigeria anaesifika kuwa ni tajiri wa kupindukia anataka kuzinunua Hisa za Klabu ya Arsenal za Asilimia 16 ambazo inadaiwa zitauzwa na Mmiliki wake Mama Nina Bracewell-Smith na inasemekana Tajiri huyo, Aliko Dangote, amekazania kuzitwaa.
Mpaka sasa ndani ya Arsenal kuna mvutano mkubwa kati ya Wamiliki wake wakuu wawili wa Hisa zake, Mmarekani Stan Kroenke na Mrusi Alisher Usmanov, ambao wanavuta nikuvute ya kutaka kuzoa Hisa nyingi ili wadhibite Klabu.
Dangote ni Mmiliki wa Kampuni kubwa ya Uzalishaji huko kwao iitwayo Dangote Group na ashawahi kuwa Mkuu wa Soko la Hisa huko Nigeria.
Shea za Mama Nina Bracewell-Smith zinauzwa kwa thamani ya Pauni Milioni 160 na Dangote yumo katika Listi ya mwisho ya Watu wanaofaa kuzinunua.
Rio yu tayari kwa Unahodha!!
Rio Ferdinand amesema yuko tayari kwa kila kitu ili kuiongoza England kama Kepteni kwenye Kombe la Dunia ingawa amekuwa na Msimu mbaya kwenye Klabu yake Manchester United kufuatia kuandamwa na maumivu ya mara kwa mara yaliyomfanya aichezee Klabu yake mechi 21 tu Msimu wote wa 2009/10 ulioisha Mei 9.
Rio amekuwa akisumbuliwa na tatizo la mgongo Msimu wote lakini amesema yuko fiti na anajisikia freshi sana kwa vile alizoea kucheza mechi 40 mpaka 50 kwa Msimu lakini Msimu huu amecheza mechi chache mno.
Rio alikuwemo kwenye Kikosi cha England cha Fainali za Kombe la Dunia Mwaka 1998 huko Ufaransa na England wakatolewa Raundi ya Pili na Argentina lakini yeye hakucheza hata mechi moja.
Rio, aliechukua Unahodha wa England baada ya John Terry kutimuliwa baada ya skandali, alicheza Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2002 na 2006 ambazo zote walitolewa Robo Fainali na Brazil na iliyofuatia na Ureno.
England wataanza kampeni yao ya Kombe la Dunia huko Afrika Kusini Juni 12 kwa kucheza na USA Mjini Rustenburg.
Rio ametamka: “Kuwa Nahodha ni heshima kubwa na ni wajibu ambao nauhusudu! Lakini hili haliwezi kunibadili! Ntabaki vilevile tu! Kabla sijawa Kepteni Wachezaji Chipukizi walikuwa wanajua mie ni mtu rahimu wanaeweza kumfuata wakiwa na tatizo na hilo ni muhimu kuliko kuwa Nahodha!”
Gerrard azua utata kubaki Liverpool!!!!!
Steven Gerrard ameididimiza Liverpool katika utata mkubwa aliposema hatma yake kubaki au kuondoka Klabu hiyo itajulikana baada ya Fainali za Kombe la Dunia.
Gerrard yuko kambini Nchini Austria pamoja na Kikosi cha England kinachojitayarisha na Kombe la Dunia.
Liverpool, baada ya kumaliza Ligi Kuu wakiwa nafasi ya 7, wamekosa nafasi ya kucheza UEFA CHAMPIONS LIGI Msimu ujao na hilo limemvunja moyo Gerrard na kuzua mjadala kuwa Nahodha huyo wa Liverpool atahama.
Gerrard, mwenye miaka 29 ambae Mwaka 2004 nusura asaini Chelsea lakini akabadili mawazo dakika za mwisho, amesema: “Sitafikiria wala kuamua lolote mpaka baada ya Kombe la Dunia. Baada ya hapo huwa tunakuwa na Wiki 3 au 4 za holidei na huo ni wakati mzuri kuamua hatma yako!”

No comments:

Powered By Blogger