Saturday 27 February 2010

LIGI KUU England: Mechi za wikiendi
Jumamosi
Chelsea v Man City
Birmingham v Wigan
Bolton v Wolves
Burnley v Portsmouth
Stoke v Arsenal
Jumapili
Tottenham v Everton
Liverpool v Blackburn
Sunderland v Fulham
Mabingwa Watetezi Manchester United hawachezi Ligi Kuu wikiendi hii na badala yake watakuwepo Uwanjani Wembley Jumapili kucheza Fainali ya Kombe la Carling na Aston Villa.
Mechi za Ligi Kuu Jumamosi zitaanza kwa mechi ya mapema huko Stamford Bridge kati ya wenyeji na vinara wa Ligi Chelsea na Manchester City.
Mechi hii ya Chelsea v Man City licha ya kuzikutanisha Timu iliyo kileleni na inayotaka kubakia huko Chelsea na Man City inayogombea nafasi ya 4, mvuto mkubwa ni yule alietimuliwa Unahodha wa England ambae ni Nahodha wa Chelsea, John Terry, kukutana uso kwa uso na ‘mbaya wake’ Wayne Bridge wa Man City, mtu ambae gelfrendi wake ndie anaesemekana alitembea na Terry na skandali hilo likamfukuzisha Terry Unahodha wa England.
Kashfa hiyo ya Terry pia imemfanya Bridge ajiuzulu kuichezea England ili asikutane na Terry.
Na sasa watakutana Stamford Bridge wakiwa Timu pinzani na swali lililo kinywani mwa kila mtu ni: je watapeana mikono kabla ya mechi?
Wapinzani wengine kwenye mechi hii ni Mameneja wa Timu hizo, Chelsea na Man City, ambao wote ni Wataliana, Carlo Ancelotti wa Chelsea na Roberto Mancini wa Man City.
Wataliana hao walikuwa Timu pinzani huko Italia, Ancelotti akiwa AC Milan na Mancini akiwa Inter Milan.
Chelsea watamkosa Kipa wao nambari wani Petr Cech alieumia kwenye kipigo cha huko San Siro toka kwa Inter Milan cha 2-1.
Man City watamkosa Adebayor aliefungiwa mechi 4 kwa kumpiga Mchezaji wa Stoke kwenye mechi ya marudiano ya FA Cup hapo juzi lakini Carlos Tevez amesharudi toka kwao Argentina alikoenda kwa matatizo ya kifamilia.
Arsenal wataenda Britannia Stadium ambako mara nyingi huumbuka ili kukutana na Stoke City na msimu uliokwisha Arsenal alipigwa 2-1.
Msimu huu, Stoke na Arsenal zilikutana kwenye FA Cup na Arsenal akachapwa 3-1.
Msimi huu, Stoke haijafungwa.
Burnley v Portsmouth ni mechi ya Timu za mkiani huku Portsmouth wakiwa pengine washajilaani kushushwa daraja baada ya kukabidhiwa mikononi mwa Msimamizi maalum ili kuwanusuru wasifilisiwe na hilo huadhibiwa kwa kukatwa pointi 9 kitu ambacho wasimamizi wa Ligi Kuu wanangojewa kukithibitisha.
Huko Reebok, Bolton wanaikaribisha Wolves na mpaka sasa ni mechi 5 tangu Bolton wafunge goli. Bolton na Wolves ziko mwishoni mwa msimamo wa Ligi na Wolves wako pointi moja tu mbele ya Bolton.
Birmingham wako nafasi ya 10 na wako pointi 12 mbele ya Wigan watakaocheza nao Uwanja wa Mtakatifu Andrew.
Siku ya Jumapili, Uwanjani White Hart Lane, wenyeji Tottenham Hotspur watacheza na Everton wanaotoka kwenye kipigo cha 3-0 mikononi mwa Sporting Lisbon kilichowatupa nje ya EUROPA LIGI.
Kwenye Ligi Kuu, Everton imeshinda mechi zao mbili za mwisho kwa kuwafunga vigogo Chelsea na Manchester United.
Tottenham wako nafasi ya 4 na watataka kujichimbia hapo.
Uwanjani Anfield, Liverpool wataikwaa Blackburn Rovers ambao siku za hivi karibuni wamegangamara na kujikwamua kutoka chini na sasa wako nafasi ya 12 kwenye Ligi.
Liverpool wako nafasi ya 6 na watataka ushindi baada ya kufungwa na Arsenal kisha kutoka sare na Manchester City katika mechi zao za mwisho.
Mara ya mwisho Sunderland kushinda ilikuwa ni mechi 13 nyuma na Sunderland watacheza na Timu ngumu Fulham wikiendi hii wakiwa nyumbani Stadium of Light.
Ushindi huo wa mwisho wa Sunderland ulikuwa Novemba 21, 2009 walipoipiga Arsenal.
Fulham nao ni magoigoi wakicheza ugenini na hawajashinda katika mechi 12 za ugenini.
Van der Sar asaini mkataba mpya
Kipa nambari wani wa Manchester United Edwin van der Sar amesaini mkataba mpya wa mwaka mmoja utakaomweka Old Trafford hadi 2011 na atakuwa amefikisha umri wa miaka 40 wakati huo.
Van der Sar ametamka kwa furaha: “Hii ni Klabu kubwa na walinionyeshea utu na uungwana mwezi Desemba na Januari Mke wangu alipougua! Nina furaha hapa!”
Nae Bosi wa Manchester United Sir Alex Ferguson amesema: “Edwin ni mtu anaeheshimu kazi na amejitunza vizuri. Ana uzoefu mkubwa na tuna furaha kuwa nae.”
Skrtel avunjika!!
Difenda wa Liverpool kutoka Slovakia Martin Skrtel amethibitika amevunjika mfupa wa kidole cha mguu wa kulia kwenye mechi ya Alhamisi ya EUROPA LIGI huko Romania Liverpool walipoifunga Unirea Urziceni bao 3-1.
Skrtel anategemewa kuwa nje kwa wiki kadhaa kama ilivyothibitishwa na Meneja Rafa Benitez ambae pia alisema Beki wao wa kulia Glen Johnson aliekuwa majeruhi ameaanza mazoezi mepesi.
Johnson alikuwa ameumia goti na alikuwa nje ya uwanja tangu Desemba.

No comments:

Powered By Blogger