Thursday 25 September 2008


CHELSEA WAMSAINI KUNGO TOKA BRAZIL

Kiungo Mineiro raia wa Brazil mwenye umri wa miaka 33 amesainiwa na Chelsea kama Mchezaji huru.
Mineiro alimaliza mkataba na Klabu yake ya mwisho Hertha Berlin ya Ujerumani mwishoni mwa msimu uliopita.
Ingawa kipindi cha uhamisho kimeisha rasmi tarehe 1 Septemba 2008 Wachezaji huru huruhusiwa kusaini kwenye klabu baada ya muda huo. Vilevile kumchukua Mchezaji kwa mkopo pia inaruhusiwa.
Meneja wa Chelsea Luis Felipe Scolari ambae ni raia wa Brazil amefurahia hatua hii kwani ana pengo kubwa la viungo kwenya timu yake baada ya Kiungo Michael Essien kufanyiwa upasuaji wa goti utakaomweka nje ya uwanja kwa miezi 6. Pia Deco aliumia kabla ya kuanza mechi na Man U na inasemekana atakuwa nje ya uwanja kwa mwezi mmoja.
Mineiro ameshaichezea Timu ya Taifa ya Brazil mara 24 na alikuwa kwenye kikosi cha Brazil kilichocheza Kombe la Dunia mwaka 2006.
===============================================================

NAHODHA WA BORO AOMBA RADHI KWA KUMUUMIZA POSSEBON WA MAN U.

Nahodha wa Middlesbrough Emmanuel Pogatetz ameomba radhi kwa kumuumiza kiungo chipukizi wa Man U Rodrigo Possebon juzi huko Old Trafford kwenye mechi ya CARLING CUP ambayo Man U waliikung’uta Boro mabao 3-1.
Pogatetz alicheza rafu hiyo mbaya dakika ya 66 ya mchezo na kupewa kadi nyekundu kwa tukio hilo.
Possebon alipewa huduma ya kwanza hapo uwanjani iliyochukua dakika 6 na kisha kukimbizwa hospitali alikolazwa hadi asubuhi kwa uchunguzi ndipo ilipothibitika hakuvunjika wala hakuathirika goti na akaruhusiwa kutoka..
Pogatetz amekiri alikosea kwani alijitosa akidhani atauwahi mpira na mara baada ya kitendo hicho alibisha na kudai amecheza mpira tu lakini baada ya kuangalia video amekubali alicheza rafu mbaya na anaomba msamaha.
Pogatetz alisema: ‘Nitampigia simu Possebon na kumwomba anisamehe kwa kumuumiza. Naomba vilevile apone haraka.’

No comments:

Powered By Blogger