Tuesday 5 January 2010

CARLING CUP: NUSU FAINALI ZOTE MBILI ZAGANDA BARAFU!!
Mechi za kwanza za Nusu Fainali za Kombe la Carling zilizokuwa zichezwe leo kati ya Blackburn na Aston Villa na nyingine kesho kati ya Manchester City na Manchester United zimeahirishwa kutokana na hali ya hewa mbaya kufuatia baridi kali na barafu.
Ingawa Viwanja vya Ewood Park, Kiwanja cha Blackburn, na City of Manchester cha Man City vinaweza kuchezeka lakini Viongozi wa Maeneo hayo wameamua ni hatari kwa Watazamaji kusafiri na kwenda kushuhudia mechi hizo hasa baada ya raia wote kutangaziwa kupunguza safari zisizokuwa za lazima kutokana na kutanda kwa barafu.
Huko Manchester, Kiwanja cha Ndege kilifungwa leo kutokana na barafu kufunika sehemu zote za kuruka na kutua ndege.
Mpaka sasa mechi kati ya Blackburn v Aston Villa haijapangwa lini itachezwa lakini mechi kati ya Manchester City na Manchester United itachezwa Januari 19 Uwanjani City of Manchester na marudio ni Old Trafford Januari 27.
Boateng si ruksa kuhamia Blackburn!!!
Ligi Kuu England imethibitisha kuwa Mchezaji wa Portsmouth Kevin-Prince Boateng haruhusiwi kuchezea Klabu nyingine yeyote Msimu huu kwa mujibu wa Sheria za FIFA kwa sababu tayari ameshachezea Klabu mbili kwa msimu mmoja na haruhusiwi kujiunga Timu ya tatu Msimu huohuo mmoja.
Boateng, ambae ashaichezea Timu ya Taifa ya Ujerumani ya Vijana Chini ya Miaka 21 lakini asili yake ni Ghana, msimu huu ameshazichezea Tottenham na Portsmouth.
Boateng amekuwa akihusishwa na kuhamia Blackburn.

No comments:

Powered By Blogger