Saturday 9 January 2010

KOMBE LA AFRIKA ANGOLA: Basi la Timu ya Togo lashambuliwa kwa risasi!
Waasi wa huko Jimbo la Cabinda Nchini Angola wamelishambulia kwa risasi basi lililobeba Wachezaji wa Timu ya Togo na kumuua Dereva wa basi hilo na kuwajeruhi Wachezaji wa Togo.
Washambuliaji hao walilipiga risasi basi hilo kwa kutumia bunduki aina ya “Mashine Gani” wakati likivuka mpaka kutoka Jamhuri ya Congo na kuingia Cabinda ambalo ni Jimbo la Angola lenye utajiri mkubwa wa mafuta.
Wachezaji wa Togo waliojeruhiwa ni Mlinzi Serge Akakpo, miaka 22, anaechezea Klabu ya Romania FC Vaslui na Kipa Kodjovi Obilale lakini hali zao zinasemekana sio mbaya.
Straika wa Manchester City Emmanuel Adebayor alikuwemo ndani ya basi hilo lakini alinusurika.
Togo wanategemewa kuanza kampeni yao Kombe la Afrika Jumatatu Januari 11 kwa kucheza na Ghana. Timu nyingine kwenye KUNDI lao B ni Ivory Coast na Burkina Faso.
Viongozi wa Angola wamesema mechi za Cabinda zitaendelea na walionyesha kushangazwa na hatua ya Togo kutumia usafiri wa ardhini badala ya kuruka na Ndege hadi Mji Mkuu Luanda halafu kuunganisha Ndege nyingine hadi Cabinda.
Waasi hao wa Cabinda, waliotangaza kusitisha vita mwaka 2006, wamedai ni wao waliofanya shambulio hilo na hatua yao ya kuanza mashambulizi jana imeishtua Angola.
Mechi za Hull v Chelsea na Liverpool v Tottenham nazo zaganda!!!!
Mechi ya Hull City v Chelsea ya Ligi Kuu iliyokuwa ichezwe leo Jumamosi Januari 9 imeahirishwa shauri ya hali ya hewa mbaya yenye baridi kali a kutanda kwa barafu na hivyo kuungana na mechi nyingine 3 za Ligi Kuu za leo zilizoahirishwa.
Mechi nyingine za leo ambazo hazitachezwa ni za Fulham v Portsmouth, Burnley v Stoke na Sunderland v Bolton.
Mechi ya Liverpool v Tottenham iliyokuwa ichezwe Jumapili tayari nayo imeahirishwa baada ya Liverpool kuviomba vyombo husika kuiahirisha mapema kutokana na kutokuwa na uhakika wa usalama wa Washabiki.
Giggs apewa “Uhuru wa Mji wa Salford”!!
Nyota wa Manchester United Ryan Giggs ametunukiwa Tuzo ya ‘Uhuru wa Mji wa Salford’ hapo juzi.
Mji wa Salford ndiko makazi ya Giggs.
Giggs, miaka 33, sasa anajumuika na watu maarufu kina Nelson Mandela na wengineo, waliowahi kupewa Tuzo hiyo.
Ingawa Giggs alizaliwa Cardiff lakini tangu utoto wake amekuwa akiishi Salford na kujiunga na Manchester United wakati bado akiwa shule.
Aliempendekeza Giggs kupewa Tuzo hiyo ni Diwani John Warmisham ambae amesema ni ‘furaha na sifa kubwa’ kumpendekeza Giggs kwa sababu Giggs si Mcheza Mpira tu bali ni mtu wa kuigwa na ni Balozi mzuri wa Salford.
Warmisham amesema: “Yeye ni Balozi wa Unicef na siku zote anaisaidia Salford!”
Siku hizi ukipewa ‘Uhuru wa Mji” unapata Shahada na utambuzi tu lakini enzi za kale ulimaanisha wewe ni Mtu Huru na si Mtumwa wa Mtajiri hivyo uko huru kufanya kazi na kupata pesa na pia kumiliki ardhi.

No comments:

Powered By Blogger