Tuesday 16 February 2010

Fergie azungumzia Mastaa wake wa zamani
Akihojiwa na Waandishi wa Habari kabla ya pambano lao la UEFA CHAMPIONS LIGI la leo usiku na AC Milan, Meneja wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, alijikuta muda mwingi akijibu na kuelezea kuhusu Wachezaji wake Mastaa walioihama Timu yake.
David Baeckham, kwa vile yupo AC Milan kwa mkopo, alitajwa sana na mwenyewe Beckham alishasema hata akifunga goli hatasherehekea.
Ferguson alitania kuhusu kauli hiyo ya Beckham: “Naomba asisherehekee!”
Akimaanisha Beckham asifunge goli.
Lakini akaongeza kwa kusema Beckham kwa vile amechezea zaidi ya mechi 100 na England na kuchezea Klabu za AC Milan, Real Madrid, Man United yupo sawa kama Wachezaji wazoefu wengine wa AC Milan kama vile Seerdof, Pirlo, Ambrossini, Nesta na Inzaghi na hilo ni manufaa kwa AC Milan katika mechi kubwa.
Ferguson alikiri Beckham bado ni shujaa kwa Mashabiki wengi wa Manchester United hasa kwa vile alikulia na kuendelezwa Klabuni hapo.
Kuhusu Ronaldo, Ferguson alisema huyo ni Mchezaji bora duniani na kumpoteza ni pengo kubwa lakini inabidi umsahau, usonge mbele na kuijenga upya Timu.
AC Milan iliifunga Manchester United miaka mitatu iliyopita na Ferguson amesema anajua walifungwaje na moja ya sababu ni uchovu wao lakini wao wikiendi hii hawakucheza mechi na hilo litawasaidia kwani watakuwa freshi.
EUROPA LIGI:
Everton v Sporting Lisbon
[saa 2 dak 45 usiku, saa za bongo]
Leo usiku Everton watashuka Uwanjani kwao Goodison Park kucheza na Sporting Lisbon ya Ureno katika mechi ya kwanza ya EUROPA LIGI na itawakosa Wachezaji wao bora kwa siku za hivi karibuni, John Heitinga na Marouane Fellaini.
Fellaini ni majeruhi na Heitinga haruhusiwi kucheza EUROPA LIGI kwa vile aliichezea Klabu yake ya zamani Atletico Madrid hapo awali.
Everton watalichukulia pambano la leo kwa tahadhari kubwa kwa sababu walishaonja joto ya jiwe walipocheza na Timu nyingine ya Ureno katika mechi za Makundi ya EUROPA LIGI mwanzoni, Benfica, iliyowafunga mechi zote mbili 5-0 na 2-0 na hivyo watakuwa makini na mechi hii na Sporting Lisbon ambao ni wapinzani wakuu wa Benfica.
Kikosi cha Everton kitatokana na: Howard, Neville, Distin, Baines, Senderos, Yobo, Cahill, Rodwell, Arteta, Osman, Pienaar, Bilyaletdinov, Coleman, Saha, Donovan, Yakubu, Vaughan, Duffy, Baxter, Nash.
Mourinho aibeza Chelsea
Jose Mourinho, aliewahi kuwa Kocha wa Chelsea lakini sasa yuko Inter Milan, ameibeza Chelsea na kutia utambi kabla ya Timu hizi kupambana wiki ijayo katika mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI kwa kudai yeye ndie aliefanikisha kuleta Vikombe vingi Klabuni hapo.
Mourinho aliachana na Chelsea Septemba 2007 na tangu wakati huo Klabu hiyo imechukua Kikombe kimoja tu cha FA mwaka jana wakati yeye katika miaka mitatu aliyokaa Stamford Bridge alitwaa Ubingwa wa England mara 2, Carling Cup mara 2 na FA Cup mara moja.
Mourinho amejigamba: “Chelsea wameathirika tangu niondoke mimi! Tulikuwa na uhusiano mzuri mimi, Wachezaji na Mashabiki na ukiuvunja uhusiano namna hiyo basi utaumia tu!”
Mourinho akaongeza: “Baada yangu wamekuwa na Makocha wengi na wengine hawakustahili kuwa hapo na pengine walitaka kuleta makubwa yasiyowezekana!”
Mourinho pia alidai kuwa Mmiliki wao Roman Abramovich ni mtu anaependa ushindi tu na usipofanikiwa upo nje.
Chelsea kwa sasa inafundishwa na Carlo Ancelotti ambae ametokea AC Milan ambao ni wapinzani wakubwa wa Inter Milan na Mourinho na Ancelotti washawahi kukwaruzana hapo nyuma.
Kuhusu hilo, Mourinho amesema: “Ancelotti si rafiki yangu na hili halibadiliki! Nchini England unaheshimiwa ukiwa kama Kocha mwenye ujuzi lakini Italia ukiwa mgeni hamna! Utaheshimiwa ukiwa Mtaliana tu na ndio maana nina furaha kufanya kazi England!”
Mourinho akabainisha kuwa yeye ni sehemu ya historia ya Chelsea na ana hamu kuona kama Ancelotti atamalizia muda wake hapo Chelsea akiwa na rekodi kama yake.

No comments:

Powered By Blogger