Wednesday 17 February 2010

UEFA CHAMPIONS LIGI: FC Porto v Arsenal
FC Porto ni wenyeji wa Arsenal Uwanjani Estadio do Dragao huko Porto, Ureno katika mechi ya kwanza ya mtoano ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya.
Fc Porto inaongozwa na Meneja Jesualdo Ferreira ambae alikuwa Mwalimu wa Jose Mourinho kwenye Chuo cha Elimu ya Viungo huko Lisbon, Ureno lakini baadae akapigwa stopu na Mourinho kuwa Meneja Msaidizi FC Porto wakati Mourinho ni Meneja hapo Klabuni.
FC Porto ina Wachezaji kadhaa mahiri akiwamo Nahodha wao Bruno Alves anaechezea Ureno, Kiungo Raul Meireles ambae pia yupo Timu ya Taifa ya Ureno.
Huko mbele wana Straika mkali ambae ashawahi kuchezea Brazil aitwae Hulk.
Arsenal wana tatizo kubwa la majeruhi ingawa wako Wachezaji wanaoweza kuziba vizuri mapengo hayo.
Majeruhi hao ni pamoja na wa muda mrefu Robin van Persie na kina Gallas, Eduardo, Song, Kipa Almunia na Arshavin.
Pia historia haiwapendi Arsenal huko Ureno kwani katika mechi 4 walizocheza huko wametoka suluhu 3 na kufungwa moja na kipigo hicho kikiwa msimu uliokwisha walipofungwa 2-0 kwenye mechi ya Makundi na FC Porto.
Magazeti Italia: “Milan wanatengeneza, Rooney anabomoa!”
Gazeti moja kubwa huko Mjini Milan, Italia limebeba bango kubwa likisema “Milan inatengeneza, Rooney anabomoa!” kufuatia kipigo cha jana cha 3-2 cha AC Milan mikononi mwa Manchester United huku Rooney akipachika bao mbili na kuwa mkuki moyoni mwa AC Milan katika mechi ya kwanza ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE iliyochezwa uwanja wa San Siro huko Milan, Italia.
Gazeti hilo limesema AC Milan walitawala pambano hilo lakini wamefungwa kwa sababu ya Wayne Rooney na sasa wanakabiliwa na kazi ngumu ya kushinda 2-0 huko Old Trafford kitu ambacho Gazeti hilo kubwa limedai hakiwezekani.
Gazeti jiingine limedai Manchester United, ikicheza kama Timu mahiri ya Italia, imeiteka San Siro kwa kutawala kipindi cha pili hasa kwa kazi ya Rooney.
Timu hizo Manchester United na AC Milan zitarudiana Old Trafford Machi 10.
Carrick astushwa na Kadi Nyekundu
Michael Carrick wa Manchester United amesema amestushwa sana na Kadi Nyekundu aliyopewa jana katika mechi waliyowafunga AC Milan 3-2 huko San Siro.
Kiungo huyo alionyeshwa Kadi ya pili ya Njano na hivyo kupewa Nyekundu na Refa kutoka Ureno Olegario Benquerenca katika dakika za majeruhi kwa kuupiga mpira baada ya Refa huyo kuashiria kuwa Evra alimchezea faulo Pato wa AC Milan.
Meneja wa Manchester United Sir Alex Ferguson amesema Carrick alifanya uzembe na Refa huyo alichofanya ni sahihi lakini mwenyewe Carrick, ambae hii ni mara ya kwanza kutolewa nje, amesema Refa amechukua uamuzi mkali kwa vile yeye aliubetua tu mpira na hakuna kitu kilichocheleweshwa.
Kwa Kadi hiyo Nyekundu, Carrick ataikosa mechi ya marudiano ya Timu hizo hapo Machi 10.

No comments:

Powered By Blogger