Tuesday 15 June 2010

PITIA: http://www.sokainbongo.com/


Bifu la Pele v Maradona!!
Edison Arantes do Nascimento, aka Pele, na Diego Armando Maradona ndio wanaosifika kuwa Wachezaji Bora kabisa katika historia ya Soka lakini Pele ndie anasifika kama ‘Mfalme wa Soka’ na mara nyingi Magwiji hawa wamekuwa na ‘Bifu la Mdomo’.
Huko Afrika Kusini limezuka ‘zozo’ jipya kati yao baada ya kudaiwa Maradona ametamka kuwa kuna ‘Muungwana Mweusi’ [ikatafsiriwa kuwa ni Pele] amehoji uwezo wa wa Afrika Kusini kuwa Nchi ya kwanza Afrika kuwa Mwenyeji wa Kombe la Dunia.
Alipohojiwa na Wanahabari, Pele alijibu mapigo: “Simwelewi huyu! Alipohitaji msaada kwangu alipoanzisha Programu za TV huko Argentina nilikwenda kumsaidia! Nikacheza nae mpira na nilimsaidia kila kitu! Baadae nilijaribu kumsaidia kutengeneza matangazo ya Progrmu zake za TV na akawa ama anachelewa kuja au haji kabisaa!”
Pele akaongeza kwa dhihaka: “Sasa kanikumbuka huku Afrika Kusini! Bila shaka ananipenda!”
Pele, aliewahi kuwa Waziri wa Michezo Brazil, alizungumza zaidi na kusema hawezi kuwa Kocha wa Brazil kwa sababu hataki kuteseka kama anavyoteseka Dunga, Kocha wa sasa wa Brazil.
Kisha Pele akamgeukia Maradona na kutamka: “Maradona alichukua Ukocha Argentina kwa sababu alikuwa hana kazi na alihitaji kazi na alikuwa anahitaji pesa pia! Najua Argentina imefuzu kuingia Fainali za Kombe la Dunia kwa matatizo! Lakini hilo si kosa la Maradona, hilo ni kosa la wale waliomchagua Kocha!”
Kocha Ureno akerwa na Drogba kucheza na gamba mkononi!
Kocha wa Ureno Carlos Queiroz amedokeza kukerwa kwake na uamuzi wa FIFA kumruhusu Nahodha wa Ivory Coast Didier Drogba kucheza huku akiwa na gamba gumu mkononi kulinda sehemu aliyovunjika Juni 4 na kufanyiwa upasuaji huko Uswisi baada ya kuumia katika mechi ya kujipima nguvu na Japan.
Drogba aliruhusiwa kucheza mechi ya Kundi G ya leo Juni 15 na Ureno iliyoisha 0-0 baada ya Kikao cha Jumatatu kati ya FIFA pamoja na Refa wa mechi hiyo Jorge Larrionda toka Uruguay pamoja na Timu hizo mbili Ivory Coast na Ureno
Lakini Queiroz, aliewahi kuwa Msaidizi wa Sir Alex Ferguson Manchester United, alihoji na kushangaa uamuzi huo kwa kusema: “ Si kazi yetu sisi kusema acheze au la ni FIFA! Jana FIFA wamesema ni juu ya Refa! Inashangaza, Wachezaji wanakatazwa kuvaa bangili, herini na plasta na huyu kavunjika mkono na kavaa gamba gumu karuhusiwa kucheza! Je angeumiza Wachezaji na hilo gamba? Labda watabadili sheria!”

No comments:

Powered By Blogger