Friday 13 November 2009

England v Brazil
Doha, Qatar
Jumamosi, Novemba 14, Brazil na England, Mataifa yenye historia kubwa ya Soka yatacheza Doha, Qatar Uwanja wa Khalifa [pichani] wenye uwezo wa kuingiza Watazamaji 50,000.
Hii ni mechi ya kirafiki tu kwani Nchi zote hizi mbili zimeshatinga Fainali Kombe la Dunia Afrika Kusini lakini hapa Doha hii ni BIGI MECHI na matayarisho yake ni sherehe kubwa, furaha kubwa na ni pia kampeni kubwa kwani nao Qatar mwaka 2022 wanalitaka Kombe la Dunia hapa.
Hapa, nje ya Uwanja wa Khalifa, kuna ‘Kijiji cha Soka’ambacho kitawakaribisha Mashabiki wanaokuja kuona pambano hilo.
Kijiji hicho cha Soka kimegawanywa mara mbili.
Kuna Kijiji cha Brazil ambacho kina mfano wa Bichi maarufu huko Brazil iitwayo Copcabana na kina Kiwanja kidogo cha kuchezea Soka ya Bichi. Pia ipo Bendi iitwayo Batucada inayopiga muziki wa Brazil.
Kijiji cha England kina ile saa kubwa na maarufu Mjini London, Big Ben. Kuna ukuta mkubwa wa kuchezea ile gemu ya video, Playstation na pia yapo mashindano ya kupiga mpira danadana.
Wale Askari ambao ni kivutio kikubwa huko England kwenye Jumba la Malkia, Buckingham Palace, pia wapo. Muziki unaangushwa na Bendi toka England iitwayo Bootleg Beatles.
Timu zote mbili zimetua Doha Jumatano usiku na pichani ni Kaka wa Brazil akikaribishwa Uwanja wa Ndege wa Doha.
Washabiki watakaokwenda kushudia mechi hiyo Uwanja wa Khalifa wameombwa wafike masaa matatu kabla mechi kuanza hiyo Jumamosi Novemba 14 saa 2 usiku saa za bongo [Hapa Doha pia ni saa 2 usiku].
Imeripotiwa kuwa Hoteli zote za hapa zimejaa na wageni wametoka kila kona ya huku Arabuni toka Nchi kama Saudi Arabia, Bahrain, Kuwait, Oman na UAE.
Pia wapo washabiki kutoka England.
Brazil na England zimewahi kukutana mara 22 na Brazil kushinda mara 10 na England mara 3.

No comments:

Powered By Blogger