Monday 23 August 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Gallas aweka historia kuhamia Spurs
Beki kutoka Ufaransa, William Gallas, atakuwa Mchezaji wa kwanza kuzichezea Klabu tatu pinzani za Jijini London, Chelsea, Arsenal na Tottenham, baada ya kusaini Mkataba wa Mwaka mmoja na Tottenham hivi juzi.
Gallas, Miaka 33, amekuwa Mchezaji wa 14 kuhamia kutoka Arsenal kwenda Tottenham katika historia ya Karne moja lakini atakuwa Mchezaji wa kwanza kucheza Klabu zote 3 zenye upinzani mkubwa huko London.
George Graham aliwahi kuzichezea Chelsea na Arsenal Miaka ya 1960 na katika Miaka ya 1970 alikuwa Meneja wa Arsenal na Tottenham.
Clive Allen alizichezea Tottenham na Chelsea na akasaini kucheza Arsenal Juni 1980 lakini baada ya Miezi miwili, bila ya kucheza mechi hata moja hapo Arsenal, akahamia Crystal Palace.
Mashabiki wengi wa Tottenham mpaka leo wanamshutumu aliekuwa Nahodha wao Sol Campbell alieondoka Tottenham kuhamia Arsenal Miaka 9 iliyopita.
Katika Miaka 10 iliyopita, Gallas ni Mchezaji wa nne tu kuhamia Spurs akitokea Arsenal wengine wakiwa Rohan Ricketts, Jamie O’Hara na David Bentley.
UENYEJI KOMBE LA DUNIA 2018: Wakaguzi FIFA watua England
Leo FA ya England watakuwa wenyeji wa Wakaguzi wa FIFA wanaotembelea Nchi zinazogombea kuwa Wenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2018 ili kukagua maombi hayo ikiwemo miundombinu.
Fainali za Kombe hilo Mwaka huu zilifanyika huko Afrika Kusini Mwezi Juni na Julai na Spain kuibuka Bingwa wa Dunia na zile zinazofuata ni Mwaka 2014 na zitafanyika Brazil.
Wakaguzi hao wamekuwa wakitembelea kila Nchi ya muombaji kwa Siku 3.
Ziara hiyo ilianzia Japan, Korea Kusini, Australia na kisha kwa waombaji wa pamoja Uholanzi na Ubelgiji, halafu Urusi na sasa England, na baadae wataendelea kwa waombaji wengine wa pamoja Spain na Ureno, kisha USA na kumalizia Qatar.
Timu hiyo ya Wakaguzi inaongozwa na Rais wa Shirikisho la Soka la huko Chile, Harold Mayne-Nicholls.
FIFA itatoa amuse wa nani watakuwa Wenyeji Mwaka 2018 na 2022 baada ya mkutano wao huko Zurich, Uswisi Desemba 2, Mwaka huu.
RATIBA YA UKAGUZI:
-Julai 19-22: Japan [Wameomba 2022]
-Julai 22-25: Korea Kusini [Wameomba 2022]
-Agosti 9-12: Uholanzi & Ubelgiji [Waombaji wa pamoja]
-Agosti 16-19: Urusi
-Agosti 23-26: England
-Agosti 30-Septemba 2: Spain & Ureno [Waombaji wa pamoja]
-Septemba 6-9: USA
-Septemba 13-17: Qatar [Wameomba 2022]
Fergie: ‘Fulham walistahili!’
Meneja wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, amekiri kuwa matokeo ya sare ya 2-2 waliyopata jana huko Craven Cottage kwenye mechi ya Ligi Kuu yalistahili hasa kwa vile Fulham walicheza vyema Kipindi cha Pili.
Mara mbili Man United walikuwa mbele na mara mbili Fulham wakasawazisha.
Pia Man United, kwenye dakika ya 87, walikosa penalti iliyopigwa na Nani na kuokolewa na Kipa Stockdale na kama wangeifunga wangekuwa mbele 3-1 lakini dakika mbili baadae Fulham wakasawazisha na mechi kwisha 2-2.
Ferguson alisema: “Ukweli ni kuwa Fulham walistahili sare. Walicheza vizuri sana Kipindi cha Pili.”
Katika mechi hiyo, Nyota wa Man United Wayne Rooney hakucheza kwa kile kilichosemwa ni mgonjwa.

No comments:

Powered By Blogger